STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, October 16, 2013

Israel Nkongo kuzihukumu Simba, Yanga kiingilio Buku 5 tu

Simba, Yanga kuhukumiwa Jumapili na Nkongo
Na Boniface Wambura
KIINGILIO cha chini kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Simba na Yanga itakayochezwa Jumapili (Oktoba 20 mwaka huu) kitakuwa sh. 5,000. Kiingilio hicho ni kwa viti vya rangi ya kijani ambavyo ni 19,648.
Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu kiingilio ni sh. 7,000, viti vya rangi ya chungwa itakuwa sh. 10,000, VIP C kiingilio ni sh. 15,000, VIP B itakuwa sh. 20,000 wakati VIP A yenye viti 748 tu tiketi moja itapatikana kwa sh. 30,000.
Tiketi zitaanza kuuzwa siku moja kabla ya mchezo huo utakaoanza saa 10 kamili jioni katika vituo mbalimbali.
Vituo hivyo ni Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala, Uwanja wa Uhuru, na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.
Mechi hiyo namba 63 itachezeshwa na Israel Nkongo kutoka Dar es Salaam, ambapo atasaidiwa na Hamis Changwalu wa Dar es Salaam pia, na Ferdinand Chacha wa Bukoba. Mwamuzi wa akiba ni Oden Mbaga wa Dar es Salaam.
Kamishna wa mechi hiyo atakuwa John Kiteve kutoka Iringa wakati mtathmini wa waamuzi (referees assessor) ni Stanley Lugenge wa Njombe.
Wakti huo huo: Mechi tatu za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) katika kundi A na C zimesogezwa mbele kutokana na viwanja vya Kambarage, Shinyanga na Nangwanda Sijaona, Mtwara kuwa na shughuli nyingine za kijamii.
Katika kundi A, mechi kati ya Ndanda na Transit Camp iliyokuwa ichezwe Oktoba 19 mwaka huu sasa itafanyika Oktoba 21 mwaka huu kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona.
Stand United na JKT Kanembwa zilizokuwa zicheze Oktoba 19 mwaka huu, sasa mechi hiyo ya kundi C itafanyika Novemba 2 mwaka huu Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga. Nayo mechi ya Mwadui na Polisi Dodoma iliyokuwa ichezwe kwenye uwanja huo Oktoba 26 mwaka huu imesogezwa hadi Novemba 3 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment