STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, November 12, 2013

Ivo Mapunda, Waziri Salum watemwa Stars, Dida aula

Ivo Mapunda
WACHEZAJI watatu wa timu ya soka ya Taifa (Taifa Stars), akiwamo kipa wa Gor Mahia, Ivo Mapunda, hawajaripoti katika kambi ya timu hiyo inayojiandaa na mechi ya kirafiki ya kimataifa inayotarajiwa kufanyika Novemba 19 kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.
Kutokana na Mapunda kutofika kwenye kambi hiyo kama ilivyopangwa, tayari kipa wa Yanga, Deogratius Munishi 'Dida', ameitwa kujaza nafasi hiyo.
Meneja wa Taifa Stars, Tasso Mukebezi, alisema mpaka jana mchana hakuwa na taarifa zozote kuhusu Mapunda na kuwataja wachezaji wengine ambao hawajajiunga na kambi hiyo kuwa ni Wazir Salum kutoka Azam na Miraji Athumani wa Simba.
Mukebezi alisema kikosi hicho kinakabiliwa na majeruhi wawili ambao ni David Luhende anayeichezea Yanga na Khamis Mcha wa Azam.
"Wachezaji wengine walioitwa katika timu hiyo maarufu kama Future Young Taifa Stars, wako salama na kesho (leo) tutawapokea wale wengine wa Taifa Stars kwa ajili ya kujiandaa na mechi iliyoko kwenye Kalenda ya Fifa," aliongeza meneja huyo.
Alisema kesho kutakuwa na mechi ya kirafiki kati ya timu ya Yosso dhidi ya Taifa Stars ambayo itasaidia kupata kikosi kamili kuelekea kwenye michuano ya Kombe la Chalenji itakayofanyika Nairobi, Kenya kuanzia Novemba 27 hadi Desemba 12, mwaka huu.
Wachezaji wa Stars wanaotarajiwa kuingia kambini leo ni Mwadini Ally, Ally Mustapha 'Barthez', Aggrey Moris, Shomary Kapombe, Nadir Haroub 'Cannavaro', Erasto Nyoni, Vicent Barnabas, Salum Aboubakar 'Sure Boy', Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Athumani Iddi 'Chuji', Mrisho Ngasa, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samatta na John Bocco.

No comments:

Post a Comment