STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, February 25, 2015

Suarez aiangamiza Manchester City, Juve yaiua Dortmund

Suarez akishangilia bao lake la pili
Suarez akishangilia bao la kwanza

Lionel Messi akipambana kabla ya kukosa penati dakika za lala salama
MSHAMBULIAJI nyota wa zamani wa Liverpool, Luis Suarez amewadhihirishia Waingereza kuwa yeye bado ni moto wa kuotea mbali baada ya kufunga mabao mawili yaliyoiangamiza Manchester City kwenye uwanja wao wa nyumbani wa Etihad, mjini Manchester katika mechi ya mkondo wa kwanza ya mtoano wa 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.
Suarez aliyeibeba Liverpool msimu uliopitwa kabla ya kuuzwa kwa 'hasira' na klabu hiyo kwa Barcelona kutokana na tukio lake la utovu wa nidhamu alililolifanya katika Fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, aliiwezesha timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 na kujiweka nafasi nzuri ya kutinga Robo Fainali katika mechi yao ya marudiano baadaye mwezi ujao mjini Barcelona.
Nyota huyo wa kimataifa wa Uruguay, alianza kuwashtua wenyeji ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya England baada ya kufunga bao la kwanza dakika 16 akiwa ndani ya  'boksi' la lango la Manchester City kabla ya kuongeza jingine katika ya 30 akimalizia kazi nzuri ya Lionel Messi na kuifanya Barcelona iende mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 2-0.
Kipindi cha pili Manchester City ambao baadhi ya wachezaji wake walinukuliwa wakitamba haiwahofii Barcelona, walijitutumia na kupata bao la kufutia machozi lililofungwa na Sergio 'kun' Aguero katika dakika ya 69 kabla ya beki wake Gael Clichy kutolewa nje ya uwanja kwa kadi nyekundu katika dakika ya 74 baada ya kupewa kadi ya pili ya njano kutokana na kumchezea rafu Dani Alves.
Lionel Messi aliinyima Barcelona kuondoka na ushindi mnono zaidi baada ya mkwaju wake wa penati kuokolewa na kipa Joe Hart dakika za lala salama. Hiyo ilikuwa ni penati ya nne kwa Messi kukosa kati ya saba alizopiga katika msimu huu.
Kipigo hicho kinaifanya Manchester City kuwa na kazi yaziada ya kuhakikisha inapata ushindi usiopungua mabao 2-0 iwapo inataka kusonga mbele katia michuano hiyo iliyopenya hatua ya 16 Bora kibahati, vinginevyo mechi ya Machi 18 itakayochezwa Camp Nou huenda ikawa ndiyo ya kuagia michuano hiyo.
Katika pambano jingine la hatua hiyo ya mtoano, Juventus wakiwa uwanja wa nyumbani mjini Turin, Italia waliizabua Borussia Dortmund ya Ujerumani kwa mabao 2-1 na kuzidi kumpa wakati mgumu kocha Jurgen Klopp ambaye kikosi chake kimekuwa na matokeo mabaya msimu huu kwenye ligi ya nyumbani ya Bundesliga.
Carlos Tevez na Alvaro Morato ndiyo walioinusisha Juventus harufu ya kucheza robo fainali baada ya kila mmoja kufunga bao katika muda usiozidi nusu saa huku, wageni wakifuta machozi kwa bao la Marco Reus.
Tevez alitangulia kufunga katika dakika ya 13 kabla ya wageni wao kulisawazisha kupitia kwa Reus dakika tano baadaye na Morata kuongeza la pili dakika ya 42 akimaliza pasi nzuri ya Paul Pogba na kuifanya Juventus kujiweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele kabla ya mechi yao ya marudiano itakayochezwa nchini Ujerumani Machi 18.

No comments:

Post a Comment