STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, February 12, 2016

BASATA YAUPIGA STOP 'SHIKA ADABU YAKO'



YAMETIMIA. Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) hatimaye limeufungia rasmi wimbo mpya wa nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Nay wa Mitego uitwao 'Shika Adabu Yako'.
Basata ilitangaza hatua hiyo leo Ijumaa kupitia taarifa yake iliyosainiwa na Katibu Mtendaji wake, Godfrey Mngareza, ikiwa saa chache tangu kuzagaa kwa taarifa hizo baada ya wimbo huo kuwa gumzo kupitia mitandao ya kijamii.
Katika wimbo huo ulioachiwa mapema wiki hii, rapa huyo aliichana Basata katika moja ya mistari yake na taarifa hiyo ya Basata imesema imeufungia wimbo huo kwa mujibu wa mamlaka iliyonayo. Ikitumia kifungu cha 4 (1) (i) ya sheria  namba 23 ya mwaka 1984 na kifungu cha 4 (2) baraza hilo limetangaza kuupiga marufuku wimbo huo na kumpa onyo kali msanii huyo.
"Tunafahamu kuna wsanii wamekuwa wakifanya hivyo makusudi kutafuta umaarufu uchwara ambao wanadhani utakuja kutokana na kuzungumzwa sana. Tunapenda kusema wazi kuwa umaarufu hauji kwa upuuzi wa namna hiyo..."
Sehemu ya taarifa hiyo ya Basata ilisomeka hivyo, ikifafanua pia imechukua hatua hiyo dhidi ya wimbo huo kutokana na ukiukwaji mkubwa wa maadili, kashfa, uchochezi, kudhalilisha watu na kuhatarisha amani na utengani miongoni wa wasanii na jamii.
na kuzima tetesi zilizotapakaa tangu juzi kuwa wimbo huo uliorekodiwa na Mr T Touch umefungiwa kutokana na kuwa na mistari inayowananga wasanii mbalimbali akiwamo Wema, Ray, Ommy Dimpoz, Shetta, DJ Choka na hata Basata lenyewe.
"Ujumbe huu uwafikie Basata.....kazi kufungia nyimbo za wasanii, hivi mnajua tabu tunazopata, mmeshindwa kazi kama mngekuwa watoto tungeshawachapa..." 
Ni moja ya mstari uliopo kwenye wimbo huo ambao umelalamikiwa na wasanii waliombwa na kuwagawa mashabiki wengine wakiuponda na kuufagilia.
Basata imesisitiza pia kwa kumuonya msanii huyo kuwa makini katika kazi zake vinginevyo atachukuliwa hatua zaidi. Wa Mitego hakupatikana kusema lolote, lakini juzi alikakariwa kuwa hata kama wimbo utafungiwa basi wakubwa watakuwa wamechelewa kwa sababu kama ujumbe umeshafika kwa jamii na akitetea alichokiimba ni ukweli mtupu.

No comments:

Post a Comment