STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, September 26, 2012

Kamanda Kova ambadili Waziri Makalla pambano la Cheka, Nyilawila

Kamanda Kova
KAMANDA wa Polisi Kanda Maalum ya Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, amembadili Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Amos Makalla katika kuwa mgeni rasmi wa pambano la kimataifa la kuwania ubingwa wa UBO, kati ya Francis Cheka na Karama Nyilawila.
Mratibu wa pambano hilo litakalofanyika siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam, Robert Ekerege aliiambia MICHARAZO kuwa, kumekuwa na mabadiliko ya mgeni rasmi badala ya Waziri Makalla sasa atakuwa Kova ambaye ni mlezi wa ngumi Tanzania.
Ekerege alisema Kova amechukua nafasi ya Makalla kutokana na waziri huyo kupangiwa safari nje ya nchi ambayo itafanyika wakati pambano la Cheka na Nyilawila likifanyika PTA.
Mratibu huyo alisema kutokana na udhuru huo wameona ni vema nafasi hiyo achukue mlezi wao wa ngumi, Kamanda KOva ambaye ameshaitikia wito huo wa kuwa mgeni rasmi ambapo ndiye atakayemvisha mkanda mshindi wa pambano hilo la uzani wa Supermiddle la raundi 12 litakalochezwa na mwamuzi toka Malawi.
"Kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu, tumeamua kubadili mgeni rasmi wa pambano la jumamosi badala ya kuwa Waziri Makalla sasa ni Kamanda wa Kanda Maalum ya Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, Waziri atakuwa safarini na hivyo hataweza kuhudhuria kama tulivyotangaza awali," alisema Ekerege.
Aliongeza, ugeni wa Kova katika pambano lao limewaongezea uhakika wa ulinzi wa kutosha siku ya mchezo huo ambao unawakutanisha Cheka na Nyilawila kwa mara ya tatu katika safari yao ya ngumi baina yao.
Ekerege alisema maandalizi mengine yanaendelea kama kawaida ambapo mabondia wote watakaopanda ulingoni wanatarajiwa kupima afya na uzito wao kesho kwenye ukumbi huo tayari kwa pambano la Jumamosi ambalo linadhaminiwa na kinywaji cha Coca Cola na kondomu za Dume na litapambwa na burudani toka kwa Mashujaa Band waliopania kuwachezesha wapenzi wa ngumi mtindo wao wa 'Kibega'.


No comments:

Post a Comment