STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, March 19, 2013

Mohammed Banka akiri Ligi Kuu ya Kenya kiboko

Mohammed Banka (kushoto) akiwa na wachezaji wenzake wa Bandari Kenya

Mohammed Banka (kati) akijifua gym ya klabu yake
KIUNGO mahiri wa zamani wa Simba na Yanga anayecheza soka la kulipwa Bandari Kenya, Mohammed Banka amekiri Ligi Kuu nchini humo ni ngumu yenye ushindani  na ufundi mwingi kulinganisha na Ligi Kuu ya Tanzania.
Akizungumza na MICHARAZO kutoka Kenya, Banka anayeicheza Ligi Kuu ya Kenya kwa mara ya kwanza msimu huu baada ya kuipandisha Bandari toka Ligi Daraja la Kwanza alisema kwa muda fupi tangu waanze kucheza ligi hiyo ameona tofauti kubwa inayomshangaza.
Banka alisema moja ya tofauti ni namna wachezaji wanavyojitambua, wakijituma uwanjani na asilimia kubwa wakiwa na viwango sawia na kutumia nguvu kubwa, kiasi kila timu huwa na gym kuwaweka fiti nyota wake.
"Huku bana ki ukweli wametuzidi wapo vizuri hata uchezaji wao watu wanajua Ligi ya Kenya ni nguvu tu,  hapa licha ya viwango nguvu ni sehemu ya mchezo ndiyo maana hata sisi tuna gym na mwalimu ana siku zake na wachezaji kuingia gym, " alisema Banka.
Tofauti ya pili alisema ni namna klabu zinavyowathamini wachezaji wao na kuwapa kila wanachokihitaji kwa ajili ya kuzipa mafanikio timu zao.
Juu ya timu yake, Banka alisema mpaka sasa imecheza mechi nne ikishinda moja, kufungwa moja na Ulinzi na kutoka sare mbili.
"Sisi tunaendelea vyema tumecheza mechi nne, tukishinda na kupoteza moja na kupata sare mbili na Jumapili tunatarajia kuvaana na Sony Sugar kabla ya kuivaa mabingwa watetezi, Tusker wiki ijayo," alisema Banka.
Alisema mechi yao ya kwanza ilikuwa dhidi ya Ulinzi Stars na kunyukwa bao 1-0 kabla ya kupata sare mbili mfululizo dhidi ya Western Stima (1-1) na City Stars (2-2) na Jumapili walifanikiwa kuilaza Homeboyz kwa mabao 3-2 na kushika nafasi ya tano.

No comments:

Post a Comment