STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 30, 2013

Sumaye awapiga kijembe wapenda rushwa


Waziri Mkuu wa zamani, Mhe. Fredrick Sumaye

WAZIRI Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, ameibuka tena na kusema, wanaokerwa na karipio lake kuhusu rushwa, wanapaswa kuachana na vitendo hivyo viovu.
Hivi karibuni, Sumaye, alitoa karipio kwa viongozi wa dini hususani ndani ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), akionya kuhusu kasi ya wanasiasa kutumika katika harambee zake.
Sumaye, alikaririwa akisema miongoni mwa wanasiasa hao, wanatumia mwanya huo kama njia ya kuungwa mkono watakapotangaza kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Ingawa hakuwataja wanasiasa hao kwa majini, kauli yake ilitafsiriwa kumgusa Waziri Mkuu ‘aliyemrithi’ na baadaye kujiuzulu, Edward Lowassa.
Lowassa ameshiriki harambee mbalimbali nchini, hali inayoelezwa na baadhi ya wachunguzi wa mambo ya siasa kuwa ina lengo la ‘kujisafishia’ njia kuelekea urais wa 2015.
Lakini Lowassa amekanusha kushiriki harambee hizo kwa nia ya kutafuta urais, badala yake akasisitiza kwamba ana karama ya ushawishi inayomfanya afanikishe shughuli hizo kwa kupata fedha nyingi.
Jana, Sumaye alizungumza na vijana wa klabu za Jogging za Ukwamani na Islamic katika uwanja wa Tanganyika Packers jijini Dar es Salaam jana.
Alisema kama mtu anaumizwa na karipio lake dhidi ya vitendo vinavyoashiria rushwa, anapaswa kuachana navyo na si kumjibu kwa kejeli.
Sumaye alisema ushiriki wake katika vita dhidi ya vitendo viovu kama rushwa, umeanza muda mrefu na kwamba hata karipio lake kwa wanaousaka uongozi kwa njia zisizo sahihi ni sehemu ya kuisimamia imani na dhamira yake.
Alisema, “kama kuna mtu anayeumizwa kwa kauli zangu ninapokaripia uovu, nikipinga rushwa basi watoaji na walaji rushwa waache kujihusisha na vitendo hivyo, na kama hawataki kusemwa basi wapasuke.”
Sumaye alisema si rahisi akaacha kukemea vitendo viovu hasa vinavyofanywa na viongozi kwa sababu, ukimya ni sehemu ya kishawishi kwa waovu kuendeleza vitendo viovu.
Akimnukuu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliposema, serikali ya wala rushwa haiwezi kuleta maendeleo kwa wananchi wake.
Sumaye rushwa ikiachwa ishamiri, itakuwa vigumu kujenga nchi yenye usawa, hivyo kuifanya nchi kuwa katika hatari ya kuangamia.
“Hivi sasa imebaki miaka miwili ya kuingia katika Uchaguzi Mkuu, hivyo tutaanza kushuhudia namna kanga, kofia, fedha na vitu vingine vitakavyotembezwa kwa ajili ya kutafuta uongozi. Tusipolisema sasa, tutaangamia,” alisema.
Alisema wananchi wanapaswa kuwa makini na viongozi wanaotumia ushawishi wa fedha na rushwa, kwani hawafai kuongoza.
Alisema viongozi wa aina hiyo wana kundi la watu nyuma yao, wanaowafadhili hivyo pindi watakapopata uongozi, watalazimika kuwatumikia waliomo katika ufadhili huo.
Alipinga dhana kuwa vijana ni kama bomu linalongoja kulipuka, badala yake ameitaka serikali kuhakikisha wanapata fursa ili wazitumie kuliko kuwaita kwa majina hatarishi.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment