STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, October 21, 2013

Abdallah Juma: Aliyerudisha heshima ya hat-trick kwa wazawa Bara

Abdallah Juma alipokuwa Simba
 HALI aliyokumbana nayo akiwa na timu ya Simba msimu uliopita, ilimfanya mshambuliaji Abdallah Juma, kukaribia kutundika daluga na kuachana na soka.
Anasema alishaamua kuachana na soka na kwenda kufanya kazi za ufundi magari kutokana na alivyokatishwa tamaa na Simba iliyomsajili kutokea Ruvu Shooting.
Hata hivyo, baada ya ushauri wa watu wake wa karibu na mzuka wa soka alionao tangu utotoni, ulimbadili mawazo yake na kuamua kujiunga na Mtibwa Sugar.
Kitendo cha kujiunga Mtibwa kimeweza kumrejeshea furaha na hasa baada ya wiki iliyopita kufunga mabao matatu (hat-trick) na kuweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza mzawa kufanya hivyo tangu Juma Semsue aliyekuwa Polisi Dodoma kupiga hat-trick.
Semsue aliweka rekodi hiyo ya kufunga hat-trick msimu wa 2010-2011 wakati Polisi ilipoishindilia Villa Squad mabao 5-3, baada ya hapo ligi hiyo ilishuhudiwa ikiisha kwa misimu miwili mfululizo bila hat-trick nyingine.
Mwezi uliopita Mrundi Amisi Tambwe wa Simba ndiye aliyekuja kuvunja mwiko huo kwa kufunga mabao manne wakati timu yake ikiizabua Mgambo JKT 6-0 na ndiyo Juma akaifikia rekodi yake wakati Mtibwa ikiifunga Oljoro JKT 5-2.
"Nimejisikia furaha, sikutegemea na hii ni hat-trick yangu ya kwanza, pia imekuja nikitoka katika kipindi cha kukata tamaa cha kucheza soka," anasema.
Juma ambaye hufananishwa na wengi na Abdallah Juma mwenye asili ya Unguja aliyewahi kutamba Mtibwa akiweka rekodi ya kufunga mabao 25 katika msimu mmoja, yote ndani ya Uwanja wa Manungu, anasema tukio hilo litabaki kuwa historia kwake.
Anasema kinachomfanya achekelee ni namna alivyoweka rekodi katika Ligi Kuu Bara akiwa mzawa wa kwanza 'kutupia' hat-trick baada ya misimu miwili, pia namna alivyoibuka akiwa keshakata tamaa ya soka kwa mambo aliyofanyiwa Simba.
"Kitendo cha kuchezeshwa mechi mbili tena kwa muda usiozidi robo saa kwa msimu mzima Simba, kutokana na kutoaminiwa na kocha, kinanitia simanzi na siwezi kusahau maishani," anasema.
Mkali huyo aliyeanza kujipatia umaarufu wa kufumania nyavu akizichezea FC Kambarage, Polisi-Shinyanga na Mwanza Utd kabla ya kutua katika Ligi Kuu kupitia AFC Arusha, Kagera Sugar na Ruvu Shooting, anawashukuru makocha wa Mtibwa Sugar kwa kumrejeshea furaha yake.
"Wananiamini na wamenisaidia kurejea katika kiwango changu, nimecheza mechi tatu tu, lakini tayari nimeweka rekodi naamini nitaendelea kufanya vema zaidi," anasema.
Anaeleza kuwa, wakati mwingine makocha huchangia 'kuua' vipaji vya wachezaji kwa kuwakatisha tamaa kwa kutokana na kutowaamini na kushindwa kuwasaidia pale wanapotokea kukosea kutekeleza maagizo yao uwanjani.
"Namshukuru Mungu. Huu ni mwanzo kwani naamini nitaendelea kufumania nyavu ili kufikia lengo la kuitwa Taifa Stars na pia kucheza soka la kulipwa nje ya nchi," anasema.

Bendera
Mkali huyo anayependa kula ugali kwa dagaa na mboga za majani huku akishushia na maji na soda, anasema mafanikio yake kisoka licha ya kuchangiwa na makocha tofauti, lakini hawezi kumsahau Madaraka Bendera aliyemnoa akiwa AFC.
Anasema Bendera alimtengeneza akawa Juma 'Magoli' ndiyo maana alimezewa mate na kuhama timu moja hadi nyingine mpaka Msimbazi ambapo hata hivyo, waliishia 'kumchomesha mahindi'.
Shabiki huyo wa Arsenal  anayemzimia mshambuliaji wa zamani wa klabu hiyo ya England, Robin van Persie aliyepo Manchester Utd kwa sasa, anasema soka limemsaidia kwa mambo mengi japo hapendi yaanikwe gazetini.
"Nitakosa fadhila kama sitamshukuru Mungu jinsi soka lilivyonisaidia," anasema.
Juma analitaja pambano la Ligi Kuu Bara kati ya AFC Arusha dhidi ya Yanga misimu minne iliyopita kuwa ndilo gumu na asilolisahau.
"Mbali na kuwa la kwanza dhidi ya timu kubwa kama Yanga, lakini kitendo cha kuingia uwanjani dakika nane kabla ya mechi kwisha na kuisawazishia AFC bao, itabaki kumbukumbu ya milele kwangu" anasema.
Anasema katika pambano hilo Yanga ilitangulia kufunga mapema na kudumu hadi dakika ya 82 alipoingizwa na kocha Bendera na kufanikiwa kufunga bao la kusawazisha na kufanya matokeo kuwa 1-1.
Abdallah Juma
Msukuma
Abdallah Salum Juma, alizaliwa 1989 mkoani Shinyanga akiwa ni mtoto wa mwisho kwa tumbo la mama yake akitanguliwa na kaka yake kwenye familia ya watoto nane wa mzee Salum Juma.
Anasema soka lake lilianzia mkoani Shinyanga wakati akisoma Shule ya Msingi Mangejese. Anafafanua kuwa alikuwa akimudu nafasi nyingi uwanjani kuanzia ya ulinzi, kiungo, hadi ushambuliaji na timu yake ya 'chandimu' ikiwa ni Mwenge Stars kabla ya kusajiliwa Segese Stars ya Kahama kwa michuano ya Ligi.
Juma anasema alivutiwa kipindi hicho na Mashaka Ayoub aliyewahi kutamba timu mbalimbali za Ligi Kuu Bara na alipotoka Segese alisajiliwa Kambarage kisha AFC Arusha iliyovutiwa naye.
Aliichezea AFC kwa misimu kadhaa kabla ya kusajiliwa Kagera Sugar kisha kurudi tena AFC na kuteuliwa timu ya Mount Meru Warriors kwa michuano ya Kombe la Taifa na kuivutia Ruvu Shooting iliyomsajili kabla ya kutua Simba.
Abdallah Juma (kulia) akiwajibika uwanjani
Anasema soka la Tanzania linazidi kupiga hatua kubwa kwa vijana kuonyesha uhai wa kurejesha heshima ya Tanzania kimataifa, japo aliiomba serikali na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuongeza nguvu katika soka la vijana ili kuwaandaa mashujaa wa kesho.
Anasema hakuna kitu anachokitamani maishani mwake kama kulitumikia taifa lake kupitia timu ya taifa ambayo hajawahi kuinusa hata kidogo, huku akiota pia kucheza soka la kulipwa Ulaya na kuwataka wachezaji wenzake kujibidiisha kwenye mazoezi na kuzingatia nidhamu na miiko ya uchezaji wa soka.
Juma anayekiri kama siyo soka huenda angekuwa fundi magari mzuri kutokana na fani hiyo kuipenda na kuisomea kwa muda, anasema ligi kuu ya msimu huu ni ngumu na inayotoa changamoto kubwa kwa klabu pamoja na wachezaji wa timu shiriki.
"Ligi ya msimu huu kiboko, haitabiriki kutokana na ugumu wake, kitu ambacho ni kizuri kwa wachezaji na hata klabu kujipanga zaidi ili kupata matokeo mazuri," anasema.
Mchezaji huyo anasema anadhani timu bora itafahamika mwishoni mwa msimu pale itakapotwaa ubingwa na kupata uwakilishi wa mechi za kimataifa kwa sababu kwa sasa ni vigumu kutabiri kwa vile timu zote 14 zina nafasi sawa ya kutwaa taji hilo kwa kadri watakavyojipanga vema.

No comments:

Post a Comment