STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, October 21, 2013

Ushindi mfululizo waipa jeuri Mtibwa Sugar

Kocha wa Mtibwa Sugar, Mecky Mexime
USHINDI wa mechi tatu mfululizo ulioiwezesha kuingia kwenye Tano Bora, umeifanya klabu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro kujipa matumaini ya ubingwa.
Mabingwa hao wa zamani wa Tanzania ambao wamekuwa wakitoa dozi nene kwa wapinzani wao kwa mechi zake za karibu, wamesema ligi ya msimu huu haina mwenyewe hivyo hata wao wanaamini wanaweza kutwaa taji mwishowe.
Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mecky Mexime, alisema ligi ya msimu huu ni ngumu na isiyotabirika na hivyo hawawezi kujiondoa kwenye ubingwa wakati wanazidi kufanya vyema katika mechi zao.
Mexime alisema anachoamini ni vijana wake wazidi kutekeleza maagizo yake na kupata ushindi katika mechi zao ili kurejea mafanikio iliyowahi kupata klabu hiyo kwa kutwaa ubingwa wa Tanzania mara mbili mfululizo.
"Tunashukuru tumepata matokeo mazuri katika mechi zetu za karibuni na hii ni baada ya kurekebisha makosa na sasa tuna matumaini zaidi ya kuwa miongoni mwa timu zinaweza kutwaa ubingwa," alisema.
Kocha huyo aliyewahi kuwa nahodha wa Mtibwa na Taifa Stars, alisema pamoja na ushindi mara tatu mfululizo kwa timu yake hauwafanyi wabweteke badala yake wanajipanga zaidi ili kupata matokeo mazuri zaidi kwa mechi zao zilizosalia.
Kikosi cha timu hiyo yenye maskani yake katika mashamba ya Manungu, Turiani Morogoro, kinatarajiwa kushuka dimbani Jumamosi kwa kuumana na Coastal Union ya Tanga mechi itakayochezwa uwanja wa Mkwakwani na Mexime alisema wanajipanga ili wafanye vizuri katika mechi hiyo.
Kwa sasa Mtibwa inakamata nafasi ya tano ikiwa na pointi 16 sawa na za Yanga ila inazidiwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa na mabingwa watetezi hao waliopo nyuma ya mtani wao Simba yenye piointi 19.
Kileleni mwa msimamo mwa ligi hiyo kuna Azam na Mbeya City ambazo zote zina pointi 20 kila moja zikitofautiana uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa.

No comments:

Post a Comment