STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, October 21, 2013

KR Mullar: Mkali wa Mapanga Shaa anayefananishwa na Gervinho



KR Mulla akikamua jukwaani
MASHABIKI wa muziki wanamuita 'Jibaba' CD 700' kutokana na kuwa na 'mapafu' ya kuhimili jukwaa akiimba na kucheza kwa muda mrefu, huku wale wa soka wamembatiza jina la Gervinho kutokana uwezo wake kisoka na kule kushabihiana kwake na nyota wa Ivory Coast aliyewahi kutamba Arsenal, Gervais Lombe Yao Kouassi maarufu kama 'Gervinho'.
Hata hivyo majina yake halisi ni Rashid Ziada 'KR Mullah', mmoja wa wasanii wakongwe wa muziki wa kizazi kipya aliyeasisi makundi kadhaa ambaye kwa sasa ametuliza 'mtima' wake katika kundi la Wanaume Halisi akiungana tena na 'swahiba' wake, Juma Kassim 'Sir Juma Nature'.
KR Mullah, ambaye kitaaluma ni fundi magari fani aliyoisomea Chuo cha VETA na kuifanya kwa muda kabla ya kutumbukia kwenye muzuki, ni kati ya vijana wachache waliojaliwa vipaji lukuki akimudu kuimba, kutunga, kucheza na kupanga muziki, huku pia akiwa mahiri katika soka akimudu nafasi mbalimbali uwanjani kuanzia nafasi ya beki, kiungo, winga hadi ile ya ushambuliaji.
Akiwa amewahi kuzichezea timu mbalimbali za mitaani katika maeneo yao ya Temeke akishiriki pia Ligi Daraja la Tatu na Nne, KR Mullah kwa sasa ni mmoja wa wachezaji anayeunda kikosi cha timu ya Golden Bush Veterani akiungana na wakali wa zamani za klabu za Simba, Yanga na Mtibwa Sugar.
Kupenda kwake soka na muziki kulimsababisha akaamua kuachana na kuchezea spana na 'oil' ili kutumikia fani hizo na kukiri kwamba kwa kiasi fulani zimemsaidia kiuchumi na kimaisha, japo hajaridhika na mahali alipo.
"Soka nalicheza kwa vile nalipenda na limenisaidia kufahamiana na watu wengi pamoja na kunisaidia kuwa pumzi kubwa jukwaani, lakini muziki ndiyo zaidi kwa kunisaidia kiuchumi, naishi na familia yangu kwa sababu ya muziki, japo sijaridhika," anasema.
Anasema japo anafarijika kuona muziki wa kizazi kipya ukikubalika mbele ya jamii tofauti na siku za nyuma, furaha yake itafikia kilele siku atakapoitwa kwenda kutumbuiza 'duniani' kama mastaa wengine wanaoletwa nchini.
"Siku nitakapoalikwa na kwenda kufanya kazi katika nchi zilizoendelea kimuziki sambamba na wakali wanaong'ara duniani, ndipo nitakapoona kweli sasa nipo juu na ndoto zangu za kuutangaza muziki wetu kimataifa imefanikiwa," anasema.
KR Mullah, aliyepewa jina hilo la Mullah akifananishwa na kiongozi aliyewahi kuvuma wa kundi la Taleban, Mullah Omar Mohammed kutokana na uwezo wa kutawala jukwaa na kuwaongoza wenzake kuwaburudisha mashabiki wao.
KR Mulla akionyesha umahiri waka katika soka
CHUJI
KR Mullah anayependa kula ugali kwa samaki na mboga za majani na kunywa maji na siku moja moja 'maji ya mende' anasema hakuna tukio la furaha kwake kama kukubalika kwa ubunifu wake wa staili ya kucheza ya 'Mapanga Shaa' inayotumiwa na kundi la TMK Wanaume Family.
"Hili ndilo tukio la furaha kuona ubunifu wangu ukitumika kama nembo ya kundi letu popote tulio na ninalizwa na matukio ya wasanii wenzetu kutangulia mbele ya haki wangali wadogo, inauma na kunitoa machozi," anasema.
Mkali huyo ambaye anajiandaa kupakua albamu yake ya pili binafsi itakayokuwa na zaidi ya nyimbo 10 ni shabiki mkubwa wa Yanga akimzimia kiungo mshambuliaji, Athuman Idd 'Chuji' na kimataifa anaishabikia Manchester United, japo anadai alijikuta akiipenda Arsenal kutokana na Gervinho, pia akidai anapenda soka la Cristiano Ronaldo.
"Kwa kweli Chuji ananikosha kwa soka lake, ni moja ya wachezaji wenye vipaji vikubwa vya soka ambao Tanzania tunapaswa kuwaringia, pia nakunwa na Ronaldo jamaa anakila kitu. Anastahili kuwa mchezaji bora wa dunia,"anasema.
Msanii huyo aliyetumbukia kwenye fani ya muziki miaka ya 1990  akianzia kwenye kundi la GMW- Mazimwi anasema lau kama siyo muziki huenda angebobea kwenye soka  kutokana na kuupenda mno mchezo huo akianza kucheza tangu akisoma Shule ya Msingi.
Anasema baada ya kutamba shuleni alizichezea timu kadhaa wakati huyo akifahamika kwa jia la utani kama 'Zico' baadhi ya timu hizo ni Sumu ya Mamba, Inter Milan, Gaza Fc katika michuano ya ligi na ile ya mchangani kabla ya sasa kutulia Golden Bush Veterani.

MUZIKI
KR Mullah aliyezaliwa zaidi ya miaka 30 iliyopita, alianza kupenda muziki tangu akiwa kinda kwa kupenda kusikiliza nyimbo za wasanii nyota wa zamani kama akina MC Hammer, Kriss Kross kabla ya kujumuika na vijana wenzake kuunda kundi la GMW Mazimwi wakati huo akisoma chuo cha ufundi VETA.
Baadaye aliungana na Juma Nature na kuunda kundi la Wachuja Nafaka kabla ya mwaka 2003 kushirikiana pamoja kuasisi kundi la TMK Wanaume Family ambalo hata hivyo lilikuja kugawanyika na kuzaliwa makundi matatu tofauti, likianza la Wanaume Halisi, kisha Temeke Unity.
Katika mgawanyiko huo huo KR Mullah aliamua kusalia TMK Wanaume Family akiwa na akina Chegge, Mhe Temba, Stico na wengine kabla ya mwishoni mwa mwaka jana kuamua kumfuata Sir Juma Nature katika kundi la Wanaume Halisi na kutoa kazi moja iitwayo 'Umemponza Mdomo'.
Mkali huyo ameshiriki albamu kadhaa za karibu makundi yote aliyowahi kufanya kazi, lakini pia alishatoa albamu yake binafsi iliyofahamika kama 'Kamua kwa Uwezo' na sasa anajiandaa kupakua albamu yake ya pili ambayo imeshatambulishwa na nyimbo kama 'Choo cha Kike' na 'Kelele'.
Nyimbo mbili ambazo anatarajiwa kuzitoa hivi karibuni ni 'Wivu' na 'Masela na Machizi' ambazo zote zitakuwa kwenye albamu hiyo.
KR Mulla akiwa na Rais Jakaya Kikwete
KR Mullah, anasema wimbo huo wa Wivu ndiyo utakaokuwa wa kwanza kutoka amaurekodia katika studio ya kundi lao ya Halisi Records kabla ya baadaye kufuatiwa na Masela na Machizi.
Mkali huyo anayelia na wizi wanaofanyiwa wasanii na kuiomba serikali iwasaidie, anasema hakuna akichukiacho kama 'bifu' za kijinga zifanywazo na wasanii wenzake alizodai zinachangia kurudisha nyuma maendeleo ya muziki.
Anasema siyo vibaya ukawapo ushindani na changamoto za kukuza muziki na siyo bifu za kuwekeana uhasama na hata kufikia wasanii kupigana au kuwa maadui, kwani haisaidii ingawa alikiri jambo hilo lipo hata kwa nyota wa dunia.
Mkongwe huyo anaiasa jamii kupambana kwa vitendo na ugonjwa wa Ukimwi kwa madai mabango na juhudi za serikali na wahamasishaji yameshatosha, huku akiwataka wasanii wenzake kupunguza kutumia dawa za kulevya.
Anasema wasanii hawazuiwi kutumia vilevi kama pombe kiasi kujiburudisha, lakini siyo kuvuka mipaka na kubwia unga au kuvuta bangi kama wehu kwani huwafanya wakose umakini wa kazi yao na kujiingiza katika vitendo viovu.

No comments:

Post a Comment