STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 5, 2014

Taifa Stars yaifuata Burundi ikiwa na hasira ya 3-0

http://www.eatv.tv/sites/default/files/styles/detailpageimg/public/stars%20jezi.jpg?itok=YI5JETByhttp://www.eatv.tv/sites/default/files/styles/detailpageimg/public/field/image/team-stars.jpg?itok=qYvzIZN8KIKOSI chenye wachezaji 20 cha timu ya taifa (Taifa Stars) kimeondoka nchini leo alfajiri kwenda Bunjura, Burundi huku kocha wa timu hiyo, Mholanzi Mart Nooij akiahidi kulipa kisasi cha kufungwa 3-0 dhidi ya taifa hilo katika mechi yao ya kimataifa ya kirafiki dhidi ya 'Etamba Murugamba' itakayopigwa nchini humo Jumapili.
Katika mechi iliyopita ya kirafiki iliyozikutanisha timu hizo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Aprili 26, mwaka huu, kikosi cha Taifa Stars kilichokuwa "kimefinyangwafinyangwa" na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kulazimisha waanze wachezaji watano wa 'maboresho', kililala 3-0 dhidi ya Warundi na kuharibu pilau la sherehe zilizokuwa zimefana za Miaka 50 ya Muungano.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam wakati wa kuagwa kwa Taifa Stars, Nooij alisema amekiandaa vyema kikosi chake kuhakikisha kinaibuka na ushindi ili kulipa kisasi cha kufungwa nyumbani na pia kujihakikishia kinapanda katika viwango vya soka vya kimataifa vinavyotolewa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
"Ninatambua Burundi ina wachezaji wazuri na wa kimataifa kina (Amisi) Tambwe, (Pierre) Kwizera na (Didier) Kavumbagu lakini kwa kikosi tunachokwenda nacho, tuna uhakika wa kushinda ugenini na kulipa kisasi maana walitufunga kwetu," alisema Nooij.
Aliwataja wachezaji 20 anaokwenda nao Bunjumbura kuwa ni pamoja na makipa Mwadin Ally (Azam FC) na Deogratias Munishi 'Dida' (Yanga).
Wengine ni Shomari Kapombe (Azam FC), Oscar Joshua (Yanga), Said Morad (Azam FC), Nadir Haroub 'Canavaro' (Yanga), Kelvin Yondani (Yanga), Joram Mgeveke (aliyesajiliwa Simba kutoka kikosi cha maboresho ya Taifa Stars), Simon Msuva (Yanga), Erasto Nyoni (Azam FC), Himid Mao (Azam FC), Amri Kiemba (Simba), Haruna Chanongo (Simba), Salum Abubakary 'Sure Boy' (Azam FC), Mwinyi Kazimoto (Al Markhiya ya Qatar), Hamis Mcha (Azam FC), Juma Luizio (Zesco FC ya Zambia), Mrisho Ngasa (Yanga), Mbwana Samata na Thomas  Ulimwengu (wote TP Mazembe ya DRC).
Nooij alisema mshambuliaji na nahodha wa Azam FC, John Bocco 'Adebayor', beki kisiki Agrrey Morris na kipa Aishi Manula wameachwa katika msafara wa Burundi kwa sababu mbalimbali zikiwamo majeraha na kutokuwa na uhakika wa kucheza Jumapili.
Alisema Bocco na Morris ni majeruhi huku akieleza kuwa makipa Dida na Mwadini wanatosha kwa mechi hiyo, hivyo haoni sababu ya kwenda na Manula.
Stars itaingia uwanjani mwishoni mwa wiki ikiwa na kumbukumbu ya kutolewa na Zimbabwe kwenye mbio za kuwania kushiriki fainali zijazo za Mataifa ya Afrika (Afcon) zitakazofanyika Morocco mwakani.
Naye Somoe Ng'itu anaripoti kuwa washambuliaji wawili wa kimataifa wa Simba, Amissi Tambwe, Pierre Kwizera na Didier Kavumbagu wa Azam, waliondoka nchini jana na kuelekea kwao Burundi kwa ajili ya kujiunga na timu yao ya taifa inayojiandaa kuivaa Taifa Stars keshokutwa.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, kocha msaidizi wa Simba, Selemani Matola, alisema kuwa Tambwe, Kwizera na nyota wengine wa Taifa Stars walipewa ruhusa jana kwa ajili ya kujiunga na timu zao za taifa.
Matola alisema kuwa hata hivyo, kuondoka kwa nyota hao hakutaharibu programu ya mazoezi kwa sababu huko wanapokwenda pia wanakwenda kucheza mechi ya kimataifa.
"Kwa upande wetu tuko vizuri, kikosi kimeiva na msimu ujao tutatoa ushindani kwa kila tutakayekutana naye," alisema Matola.
Taifa Stars na Burundi zinakutana katika mchezo unaotambuliwa na kalenda ya FIFA.
Tayari wachezaji wanaocheza nje ya nchi, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Mwinyi Kazimoto anayecheza klabu ya Al Markhiya ya Qatar wameshawasili nchini.
Awali Stars ilitarajia kucheza dhidi ya Morocco lakini Waarabu hao waliikacha wakidai kwamba wamewakosa nyota wao wanaocheza nje ya nchi hiyo.

No comments:

Post a Comment