STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, January 3, 2015

Simba yaona mwezi Mapinduzi, Mtibwa yabanwa

Kikosi cha Simba

Hekaheka katika pambano la Mtibwa na JKT (Picha: ZanziNews)
BAO la shuti kali la umbali wa mita 40 lililowekwa kimiani na kiungo Said Ndemla limeiwezesha Simba kufufua matumaini yao katika michuano ya Kombe la Mapinduzi baada ya kuibuka na ushindi mbele ya Mafunzo.
Simba ambao ilitoka kupokea kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Mtibwa katika pambano lao la kwanza ilishuka dimbani ikiwa inaongozwa na kocha wake mpya, Mserbia Goran Kapunovic na ilienda mapumziko ikiwa suluhu dhidi ya timu hiyo ya visiwani Zanzibar.
Katika kipindi cha pili kilikuwa chenye kasi zaidi kwa timu zote na Simba ilipata bao pekee lililofungwa na Ndemla katika dakika ya 54 baada ya kuipokea pasi ya Hassan Kessy na kufumua shuti kali lililomshinda kipa Hashim Haruna na kuwapa faraja mashabiki wa Msimbazi ambao walikuwa hawana raha baada ya timu yao kupokea kipigo cha Mtibwa ikiwa ni siku chache tangu ilale kwenye ligi kuu dhidi ya Kagera Sugar.
Katika pambano jingine la michuano hiyo lililochezwa mapema, Mtibwa Sugar na JKU zilishindwa kutambiana baada ya kwenda sare ya 1-1 huku Mtibwa ikijilaumu kwa kukosa penati iliyopotezwa na Mussa Hassan Mgosi aliyetangulia kuifungia Mtibwa bao kabla ya JKU kurejesha kupitia kwa Amour.
Michuano hiyo itaendelea tena kesho kwa pambano la mapema litakalowakutanisha mabingwa watetezi KCCA ya Uganda dhidi ya Mtende kisha Yanga kuvaana na  Polisi Zanzibar jioni na usiku kushuhudia Azam ikipepetana na KMKM.

No comments:

Post a Comment