STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 18, 2013

Samatta, Ulimwengu kutua Stars leo

Mbwana Samatta (kushoto waliosmama) akiwa na kikosi cha Stars
WASHAMBULIAJI Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaochezea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemorasia ya Congo wanatarajiwa kutua nchini leo usiku kujiunga na kambi ya timu ya Taifa Stars inayojiandaa kuikabili Morocco katika mechi ya Kundi C la kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Jumapili.
Kwa mujibu wa afisa habari wa shirikisho la soka nchini (TFF), Boniface Wambura, kikosi cha Stars kitakamilika kesho Jumanne asubuhi baada ya wachezaji walio katika kikosi cha Azam nchini Liberia kwenye mechi ya Kombe la Shirikisho kurejea.
Taifa Stars ilianza kambi juzi jioni ambapo wachezaji 14 kati ya 23 walioitwa waliripoti na kufanya mazoezi jana asubuhi chini ya kocha Kim Poulsen.
Wachezaji walioripoti ni nahodha Juma Kaseja kutoka Simba na msaidizi wake Aggrey Morris wa Azam, Erasto Nyoni (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Nadir Haroub (Yanga), Nassoro Masoud 'Cholo' (Simba), Shomari Kapombe (Simba) na Salum Abubakar (Azam).
Wengine ni Athuman Idd 'Chuji' (Yanga), Amri Kiemba (Simba), Frank Domayo (Yanga), Mwinyi Kazimoto (Simba), Mrisho Ngasa (Simba) na Simon Msuva (Yanga).
Wachezaji Hussein Shariff, Issa Rashid na Shabani Nditi ambao timu yao ya Mtibwa Sugar juzi ilicheza mechi ya Ligi Kuu ya Bara mjini Turiani waliripoti kambini jana jioni.
Wakati huo huo, Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limeteua waamuzi kutoka Angola kuchezesha mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Morocco (Lions of the Atlas).
Mechi hiyo ya kundi C itachezwa Machi 24 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Ivory Coast ndiyo inayoongoza kundi hilo ikiwa na pointi nne na kufuatiwa na Taifa Stars yenye pointi tatu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na TFF jana, mwamuzi wa mechi hiyo ni Helder Martins de Carvalho wakati mwamuzi msaidizi namba moja ni Inacio Manuel Candido huku Ricardo Daniel Cachicumi akiwa mwamuzi msaidizi namba mbili. Mwamuzi wa mezani (fourth official) ni Antonio Muachihuissa Caxala.
Waamuzi hao watawasili nchini saa 1.20 usiku Machi 22 mwaka huu kwa ndege ya Kenya Airways wakitokea Luanda, Angola kupitia Nairobi, Kenya.
Kamishna wa mechi hiyo atakuwa David Fani kutoka Botswana anatarajiwa kuwasili Ijumaa Machi 22 saa 1:45 usiku kwa ndege ya South African Airways.
Naye mtathmini wa waamuzi (referee assessor) Neermal Boodhoo kutoka Afrika Kusini atawasili nchini Ijumaa pia saa 1:45 usiku kwa ndege ya South African Airways.

No comments:

Post a Comment