STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 18, 2013

Chove: Kipa ajiandaaye kutua As Vita baada ya kutemwa Coastal


Kipa Jackson Abraham Chove akiwa katika pozi

 IMEKUWA ni desturi kwa wachezaji wengi nchini wanapobahatika kupata nafasi ya kuzichezea timu kubwa za hapa Tanzania au kucheza soka la kulipwa nje ya nchi huridhika na kujiona wamefikia kilele cha mafanikio na kubweteka.
Kwa golikipa Jackson Abraham Chove aliyewahi kucheza soka la kulipwa katika klabu kadhaa za Afrika Mashariki na Kati na kuzidakia Yanga, JKT Ruvu, Prisons-Mbeya, Azam na Moro United, hali ni tofauti.
Kipa huyo aliyeidakia Coastal Union ya Tanga katika mechi za duru la kwanza la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu kabla ya kutemwa, anasema bado hajaridhika licha ya kucheza soka la kulipwa mara kadhaa na kurejea nyumbani.

Oyaaa mambo gani sasa! Chove akimuonya Felix Sunzu wa Simba wakati wa mechi ya Coastal Union na Simba duru la kwanza iliyoisha kwa suluhu ya kutofungana.

Kwa sasa, nyota huyo anayefahamika kama 'Mandanda' akifananishwa na kipa wa Ufaransa mwenye asili ya Kongo, Steve Mandanda, anajiandaa kwenda nchini DR Congo kucheza soka la kulipwa katika klabu ya As Vita.
"Kila kitu kimekamilika kwa ajili ya safari hiyo ya Kinshasa ambayo nilikuwa niondoke wiki mbili zilizopita kabla ya kuibuka baadhi ya mambo ambayo yamenifanya nikawie kwenda huko," anasema.
Chove, shabiki mkubwa wa Mtibwa Sugar na Manchester United, anasema wakati wowote mambo yake yakikaa vizuri ataondoka nchini kwenda kujiunga na timu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu ya nchi hiyo.
Anasema anaamini ana uwezo wa kucheza soka katika klabu hiyo ya Vita na kwamba umahiri aliouonyesha wakati akicheza soka la kulipwa katika klabu ya As Dolpine ya huko ndiyo 'tiketi' iliyomfanya uongozi wa klabu hiyo kumsaka.
"Unajua nilishawahi kucheza nchini humo miaka ya mwanzoni ya 2000 katika klabu ya As Dolphine ndiyo maana As Vita wamenifuata," anasema.

MKALI
Chove aliyezaliwa miaka 30 iliyopita, akiwa shabiki mkubwa wa muziki wa Kicongo akiizimia bendi za Mapacha Watatu na Akudo Impact, ni mmoja wa makipa hodari nchini waliozichezea timu nyingi ndani na nje ya nchi.
Kitu cha ajabu ni kwamba kabla ya kuwa kipa alikuwa mmoja wa mabeki hodari na pia alipata kucheza kama mshambuliaji wa kati kabla ya kubadilisha namba na kuhamia kwenye nafasi anayoichezea kwa miaka kadhaa sasa.
Chove anayependa kuwa mfanyabiashara mkubwa mara atakapotundika glovu zake, alianza makeke yake tangu shuleni mjini Dodoma akiitaja klabu iliyokuza kipaji chake kuwa ni Job Lusinde chini ya kocha Shaaban Tall.
Baada ya kutoka Lusinde alihamia Vijana Airport aliyocheza na nyota kama Athuman Idd 'Chuji' na wengine na baadaye kutua Makore FC, Zulphat na Mji Mpwapwa na kukimbilia Singida United kabla ya kuichezea Milambo ya Tabora.
Milambo ilimuita akazibe nafasi ya kiungo Mohammed Banka aliyekuwa amehamia Moro United.
Mwaka 2003 alitua Tukuyu Stars na miaka miwili baadaye alitua Kahama United, kisha kwenda Twiga Sports aliyoitema na kuhamia CDA Dodoma kabla ya kutimkia Malawi kuidakia Mzuzu Medical.
Aliporejea nchini  mwaka 2007 aliidakia Friends Rangers ikicheza Ligi ya TFF Kinondoni na kuivutia Yanga iliyomnyakua msimu wa 2007-2008 kabla ya miamba hao kumtema msimu uliofuata ambapo alienda kujiunga na Prisons ya Mbeya.
Chove anayemmwagia sifa kocha Stewart Hall kama mmoja wa makocha bora kuwahi kukutana nao, alikaa na Prisons kwa muda mfupi kabla ya kutimkia Rwanda kukipiga katika klabu ya Marine na baadae AS Dolpine ya DR Congo.
Aliitwa SC Villa na kuichezea kidogo sambamba na akina Steve Bengo na Emmanuel Okwi, kabla ya kurudi Marine na kuisaidia kuinyima ubingwa timu ya Atraco iliyotaka kumsajili kabla ya kughairi.
Baada ya kutoswa na Atraco alihamia Kiyovu na mwishoni mwa msimu wa 2009-2010 alisajiliwa JKT Ruvu kwa mkataba mfupi na kabla ya kuisha alitua Azam iliyokuja kumtema baada ya msimu mmoja na kuhamia Moro Utd.
Msimu huu alisajiliwa Coastal Union na kucheza kwa nusu msimu kabla ya kutemwa pamoja na wachezaji wengine kwa pendekezo la kocha, Hemed Morocco.

Chove (kati walio mbele) akiwa na kikosi cha Coastal Union


MAFANIKIO
Chove aliyeanza kucheza kama beki kabla ya kuhamia kwenye ushambuliaji na baadaye kuhamia kwenye ukipa hadi sasa, anajivunia soka kumpa mafanikio yakiwamo ya kumiliki maduka ya nguo na saluni za kiume.
"Siyo siri soka limenisaidia mengi kimaisha na kiuchumi. Mbali na kunipatia marafiki wengi na kusafiri nchi nyingi, limeniwezesha kumiliki miradi yangu ya kuniingizia pesa," anasema.

Chove akiwa ndani ya Pipa wakati akiichezea Taifa Stars
Kipa huyo mwenyewe mbwembwe anaitaja mechi kati ya Yanga na JKT Ruvu msimu wa 2008-2009 kuwa ngumu kwake na asiyoisahau.
Anasema anaikumbuka mechi hiyo kwa vile ilikuwa pambano lake la kwanza kuidakia Yanga katia Ligi Kuu na kuisaidia kushinda bao 1-0.
"Naikumbuka kwa ugumu wake, lakini kubwa kuwa mechi yangu ya kwanza kuidakia Yanga kwenye ligi na tulishinda bao 1-0," anasema.

STARS
Chove anayependa kula wali kwa njegere na kunywa soda ya Fanta, anaitabiria timu ya taifa (Taifa Stars) kufika mbali ikiwa chini ya kocha Kim Poulsen lakini amewataka wachezaji wanaoichezea 'kukaza' ili kuipa mafanikio hayo.
"Stars chini ya Poulsen ni kama ilivyokuwa na Marcio Maximo, muhimu wachezaji wajitume ili kuzidi kuwapa raha Watanzania. Naamini wakikomaa tunaweza kufuzu fainali kubwa tunazoshiriki," anasema.

Jackson Chove (kulia) akiwa na Marcio Maximo
Stars inatarajiwa kushuka dimba wiki hii kucheza dhidi ya Morocco katika mechi ya kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2014 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ikiwa inashika nafasi ya pili nyuma ya Ivory Coast katika Kundi C.
Chove ambaye aliwahi kuichezea Stars kwa nyakati tofauti chini ya makocha Maximo na Jan Poulsen, anasema kama wachezaji watajitoa mhanga uwanjani ni wazi wanaweza kupata pointi tatu muhimu zitakazowaweka pazuri zaidi.
Kipa huyo mwenye watoto wawili, Senior na Junior, wenye umri wa miaka sita, anasema soka la Tanzania limepiga hatua kubwa ila ni vema viongozi wa klabu wakaondoa ubabaishaji kuweza kuwasaidia wachezaji.
Anasema kama viongozi wakiwa watu wa 'longolongo' ni vigumu wachezaji kupata moyo wa kujituma uwanjani na akawataka waache tabia ya kubadilisha makocha ovyo akidai inachangia kuwachanganya wachezaji.
Juu ya wachezaji wenzake anawasihi wasibweteke na kucheza ndani badala yake wachangamkie fursa wanazozipata za kwenda kucheza soka la kulipwa nje kama anavyofanya yeye kila mara.


----------

No comments:

Post a Comment