STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 18, 2013

Wajanja wasiitumie 'Kanumba Day' kujinufaisha

Steven Kanumba enzi za uhai wake
 
MWEZI ujao mashabiki wa sanaa hasa wale wa filamu wataadhimisha mwaka mmoja tangu wampoteze kipenzi chao na nyota wa fani hiyo nchini, Steven Kanumba 'The Great' aliyefariki ghafla nyumbani kwake Aprili 6, mwaka uliopita.
Kanumba alifariki kwa kile kilichoelezwa alianguka na kubamiza kichwa wakati wa mzozo kati yake na aliyekuwa mpenzi wake ambaye ni muigizaji nyota, Elizabert Michael 'Lulu' na kuwaachia majonzi W`atanzania waliokuwa wakimfuatilia.
Hakuna ubishi kwamba msanii huyo alikuwa gwiji na mmoja wa wasanii wachache waliokuwa wakielekea kwenye mafanikio ya kimataifa kupitia kazi mbalimbali alizocheza enzi za uhai wake.
Kifo chake kilitokea wakati akijiandaa kwenda Ghana na Marekani kwa ajili ya kurekodi kazi kulingana na mkataba aliokuwa amepata wiki chache kabla ya kukumbwa na mauti.
Pia alifariki wakati Watanzania wakiendelea kumhitaji katika kuwapa burudani kupitia fani aliyokuwa akiifanya kwa nidhamu ya hali ya juu kiasi cha kuwaacha wenzake mbali kimafanikio.
Pengo la msanii huyo bado linaonekana halipata mtu wa kuliziba licha ya kuwepo kwa baadhi ya wasanii kufurukuta kutaka kuvaa 'viatu' vyake ndani ya faani hiyo ya filamu nchini ambayo imekuwa ikielezwa ilitetereka kisoko tangu alipofariki.
Kifupi ni kwamba Watanzania wanaendelea kukumbuka na kumlilia Kanumba kwa yale aliyoyafanya kama msanii mwenye weledi na anachojua alichokuwa akikifanya.


Hata hivyo, wakati watanzania wakielekea kwenye kuadhimisha mwaka mmoja tangu mkali huyo kufariki, tayari kumekuwa na taarifa za maandalizi ya maadhimisho hayo ya kumuenzi Kanumba yatakayofanyika mwezi ujao hususani siku aliyofariki ya Aprili 6, nilikuwa natoa tahadhari juu ya wanaotaka kutumia siku hiyo kutaka kujinufaisha.
Kwa uzoefu nilionao kama mdau wa sanaa, wapo baadhi ya watu hutumia mwanya wa kuwepo kwa shughuli fulani kujinufaisha kimasilahi huku ndugu, jamaa na wanafamilia husika wakiachwa solemba, ndiyo maana natoa angalizo hilo mapema.
Ni vema maadhimisho ya kumuenzi Kanumba yatumiwe kwa nia ya dhati ya kuenzi yote aliyokuwa akiyafanya marehemu Kanumba ikiwemo kupenda haki, usawa na uaminifu.
Wanaoratibu shughuli zozote za maadhimisho hayo ya mwaka mmoja wa Kanumba maarufu kama Kanumba Day iwe jijini au kwingineko nchini, wafanye kwa lengo la kuenzi juhudi za msanii huyo na kuwashirikisha wanafamilia ili kuepuka manung'uniko.
Inakumbukwa mara alipofariki msanii huyo, wajanja walitengeneza fulana, kofia na hata vitabu bila kuwashirikisha wanandugu mpaka familia ilipokuja kushtuka na kupiga marufuku, hivyo hata katika kuelekea huko hilo lazima lizingatiwe.
Naamini haya yakifanyika Kanumba Day itakuwa na maana halisi kinyume cha hapo itakuwa ni sawa na wizi, utapeli na kutoitendea haki familia ya msanii huyo na hata Kanumba mwenyewe japo hayupo nasi kimwili, lakini kiroho tu pamoja nasi.

No comments:

Post a Comment