STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 19, 2013

Azam wamtengea Shomari Kapombe kiasi cha Sh Mil.90/-


Shomari Kapombe

Na Somoe Ng'itu
KATIKA kuhakikisha mwakani inakuwa na ukuta imara, klabu ya Azam imeanza mikakati ya kumnasa beki tegemeo wa Simba na timu ya soka ya Tanzania (Taifa Stars), Shomary Kapombe na tayari imetenga kiasi cha Sh. milioni 60.
Mbali na kiasi hicho cha fedha pia Azam imepanga kumpatia beki huyo kiraka gari jipya la thamani ya Sh. milioni 30.
Azam inataka kutumia udhaifu wa Simba kushindwa kumpatia mkataba mpya beki huyo ambaye mkataba wake wa sasa unamalizika Desemba, jambo linalomaanisha anaweza kuondoka bure iwapo atakataa kusaini mkataba mpya Msimbazi na pesa zote kutoka katika klabu itakayomsajili zitaingia mifukoni mwake.
Hata hivyo, beki huyo amemweleza rafiki yake wa karibu kwamba kiasi hicho ni kidogo kwa kiwango alichonacho hivi sasa.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana jijini Dar es Salaam, uongozi wa Azam, timu pekee nchini ambayo kwa sasa inashiriki mashindano ya kimataifa, imetenga kiasi cha Sh. milioni tatu kama mshahara wa kila mwezi wa beki huyo aliyesajiliwa na Simba akitokea timu ya Polisi Morogoro.
Chanzo kililiambia gazeti hili kuwa Azam wakifanikiwa kumpata Kapombe, mikakati yao itakuwa ni kwa chipukizi Haruna Chanongo na Ndembla Ibrahim.
"Wameanza maandalizi ya kumshawishi asisaini mkataba mwingine wa Simba na wao watamsainisha ifikapo mwezi Agosti mwaka huu," kilisema chanzo hicho.
Kapombe alishindwa kusema lolote kuhusiana na kuwapo kwa mazungumzo dhidi ya Azam na kuongeza kwamba yeye kwa sasa ni mchezaji wa Simba hivyo anajipanga kuisaidia timu yake ifanye vizuri katika mechi zilizosalia.
Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala, Kapombe ni mmoja wa wachezaji mihimili wa klabu hiyo na hawatakuwa tayari kuona wanasajiliwa na klabu nyingine.
Mtawala alisema kwamba Kapombe ni mchezaji muelewa na kamwe hataweza kukurupuka na kukubali kuiacha Simba iliyomchukua hali ya kuwa klabu yake imeshuka daraja.
"Anafahamu ana kiwango cha kucheza soka Ulaya na Simba ni sehemu pekee inayoweza kutimiza ndoto zake, tutakaa naye na kumpa mkataba mnono ndani ya muda muafaka," alisema katibu huyo mwenye taaluma ya sheria.
Viongozi wa Azam, katibu mkuu Nassor Idrissa na meneja Patrick Kahemele, hawakupatikana jana katika simu zao za mikononi kuzungumzia mipango hiyo ya kumnasa Kapombe.
Hata hivyo, Azam imekuwa na kawaida ya kufanya usajili wake kimya kimya na hutangaza mchezaji mpya baada ya kukamilisha taratibu zote zinazotakiwa iwe kwa mchezaji wa ndani au nje ya nchi.

Chanzo:NIPASHE

No comments:

Post a Comment