STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 19, 2013

Niyonzima ‘abomoka’ pua


Haruna Niyonzima dimbani

Na Sanula Athanas, Tanga
WACHEZAJI watatu wa Yanga akiwamo kiungo wao wa kimataifa Mnyarwanda Haruna Niyonzima ‘Fabregas’, waliumia vibaya katika mechi yao ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara dhidi ya ‘maafande’ wa Mgambo JKT iliyomalizika kwa sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini hapa juzi, imefahamika.
Akizungumza na NIPASHE wakati wa mazoezi ya Yanga kwenye uwanja huo jana asubuhi, Daktari wa timu hiyo, Nassoro Matuzya alisema kuwa Niyonzima aliumia vibaya pua yake alipogongana na beki 'kisiki' wa Mgambo, Bashiru Chanacha dakika 12 kabla ya mechi hiyo kumalizika.
Matuzya, ambaye pia aliwahi kuwa daktari wa timu ya taifa ya vijana (Serengeti Boys), alisema kuwa kugongana kwa wawili hao kulisababisha kupasuka kwa jipu dogo alilokuwa nalo nyota huyo puani kwake.
Mwandishi alishuhudia pua ya Niyonzima aliyekuwa amekaa kwenye benchi wakati wachezaji wengine wa Yanga wakiendelea na mazoezi jana, ikiwa ‘imebomoka’ sehemu ya juu na baadhi ya nyama zikining’inia kwa chini ndani ya matundu ya pua.
Hata hivyo, maofisa wa Yanga waliokuwa uwanjani waliwakataza waandishi kumpiga picha kwa sababu jeraha alilokuwa nalo lilikuwa linatisha.
Akizungumza kwa tabu, Niyonzima aliliambia gazeti hili kuwa alikuwa akijisikia maumivu makali usiku wa kuamkia jana, lakini anaamini kidonda hicho kitapona haraka ili arejee uwanjani kupambana kuwania ubingwa wa 23 wa ‘Wanajangwani’.
“Kwa kweli mechi ya jana (juzi) ilikuwa ngumu. Wapinzani (Mgambo) walikuwa wameikamia, walikuwa wanacheza rafu za kutisha. Angalia pua yangu ilivyo. Usiku nimehangaika sana kupata usingizi. Kinachouma zaidi marefa hawakutoa adhabu yoyote licha ya kufanyiwa faulo mbaya kama hii,” alisema Niyonzima huku akishika pua yake.
“Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kupata pointi moja kwa sababu tulicheza katika uwanja usiokuwa na hadhi na waamuzi hawakutenda haki kwetu kwa kiasi kikubwa,” aliongeza mchezaji huyo wa zamani wa klabu ya maafande wa APR ya Rwanda.
Mbali na Niyonzima, ambaye mkataba wake na Yanga unamalizika mwishoni mwa msimu huu, kiungo Frank Domayo na mshambuliaji Mganda Hamis Kiiza pia wanasumbuliwa na majeraha baada ya kuumia katika mechi ya juzi.
Kwa mujibu wa daktari wa Yanga (Mtuzya), Kiiza ambaye alishindwa kufanya mazoezi ya jana, aliumia kifundo cha mguu wa kulia dakika moja kabla ya mapumziko ya mechi yao ya juzi na nafasi yake kuchukuliwa na mfungaji bora wa Kombe la Kagame mwaka jana, Said Bahanunzi.
“Kiiza ameshindwa kufanya mazoezi kwa sababu jana (juzi) aliumia kifundo cha mguu. Domayo nililazimika kumshona nyuzi mbili usoni baada ya kupasuka,” alisema Matuzya.
Yanga waliondoka jijini hapa jana saa 5:24 asubuhi kurejea Dar es Salaam kujiandaa kwa mechi yao ya 24 ya ligi msimu huu dhidi ya JKT Ruvu itakayopigwa Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa jijini humo.
Kabla ya kuondoka jijini hapa jana, meneja wa timu hiyo, Hafidh Saleh alisema kuwa baada ya kutua Dar es Salaam, wachezaji watapewa mapumziko ya saa 12 kabla ya kuingia tena kambini jijini humo kujiandaa kwa mechi dhidi ya JKT Ruvu.
Mabingwa wa Afrika Mashariki na Kati Yanga wanaongoza msimamo wa ligi ya Bara wakiwa na pointi 53, sita juu ya mabingwa wa Kombe la Mapinduzi, Azam wanaokamata nafasi ya pili. Yanga wanahitaji pointi nne tu kutawazwa mabingwa pasipo kujali matokeo ya Azam katika mechi tatu zilizobaki.

CHANZO:NIPASHE

No comments:

Post a Comment