STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, June 8, 2013

LICHA YA HUJUMA, STARS YAAPA KUIFANYIZIA MOROCCO

Straika wa Taifa Stars, John Bocco (wa pili kulia) akimiliki mpira huku akichungwa na Athuumani Idd 'Chuji' nyuma yake wakati wa mazoezi yao kuelekea mechi yao ya leo usiku ya kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Morocco mjini Marrakech.

Beki wa Stars, Erasto Nyoni (kulia) akikokota ngoma huku akichungwa na Frank Domayo huku Kelvin Yondani ( wa tatu kulia) na Mrisho Ngasa (kushoto) wakishuhudia wakati wa mazoezi yao kuelekea mechi yao ya leo usiku ya kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Morocco mjini Marrakech.

Straika wa Stars, Mbwana Samata (kushoto)akimiliki mpira wakati wa mazoezi yao kuelekea mechi yao ya leo usiku ya kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Morocco mjini Marrakech.

Ulimwengu (kushoto), Aggrey Morris, Mwinyi Kazimoto wakiwania mpira  wakati wa mazoezi yao kuelekea mechi yao ya leo usiku ya kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2014 dhidi ya Morocco mjini Marrakech.
TIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars usiku wa kuamkia leo ilifanyiwa kilichoonekana kuwa hujuma baada ya kufanyiwa vurugu na kuzimiwa taa ishindwe kufanya mazoezi kwenye uwanja wa utakaotumika kwa mechi ya leo, siku moja kabla ya mchezo wao dhidi ya wenyeji wao Morocco ya kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia 2014.

Sheria za FIFA zinasema timu mgeni, itapewa fursa ya kufanya mazoezi katika uwanja utakaotumika kwa mechi dhidi ya wenyeji katika muda ambao mechi itachezwa, lakini jana msafara wa Stars ulipofika Uwanja wa Marakech ulizuiwa kuingia ndani na askari wa uwanjani hapo.

Juhudi za kocha wa Stars, Kim Poulsen kuwaelewesha askari wa uwanja huo sheria ili wairuhusu timu kuingia uwanjani hazikuzaa matunda na ikabidi viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) waingilie kati, nao pia wakachemsha.

Ikawadia zamu ya viongozi wa Kamati ya Ushindi ya Stars, inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premum Lager, ambao nao walichemsha, ndipo baadhi wa Watanzania waishio hapa na wachache waliosafiri kutoka Dar es Salaam walipoongeza nguvu.

Walikwenda kufungua geti kwa nguvu, wakawaweka kando askari waliokuwa wanawazuia na kuiingiza timu uwanjani kufanya mazoezi.

Hata hivyo, Stars ilipofika uwanjani ililazimika kusubiri tena, kwani wenyeji Simba wa Atlas walikuwa wakiendelea na mazoezi.

Baada ya nusu saa, Morocco walimaliza awamu yao na Stars wakaanza kupasha misuli moto. Hata hivyo, baada ya dakika 34, taa za uwanja huo zilizimwa na uwanjani kuwa giza totoro, lakini viongozi wa TFF wakaenda kuomba, zikawashwa na timu ikafanya mazoezi kwa dakika 10 zaidi.

Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Amos Makalla aliyekuwapo wakati wa vurumai zote hizo, alisikitishwa mno na kitendo hicho akisema si cha kiungwana na si cha kiunamichezo.

Makamu wa Rais wa TFF, Athumani Nyamlani alisema Morocco walikuja kucheza Dar es Salaam walipokewa vizuri na wakahudumiwa vizuri hadi wanaondoka, ajabu leo wanaifanyia ‘unyama’ Tanzania.

Mkuu wa Msafara wa Stars hapa, Crescentius John Magori alisema watapeleka malalamiko FIFA, waandaji wa michuano ya kufuzu kwa Kombe la Dunia na kwa kuwa ushahidi upo, anaamini Morocco watachukuliwa hatua.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe alishauri Stars icheze chini ya angalizo kwa kuwasilisha barua FIFA mapema ili wakae wanajua kuhusu hali halisi Morocco.

Kwa ujumla kilichotokea leo kimewatia woga Watanzania wengi waliopo hapa kuelekea mchezo wa leo, ambao Stars inahitaji ushindi ili kujiimarisha katika mbio za kuelekea Brazil 2014.

Hata ulinzi wa msafara wa Stars kutoka hotelini hadi uwanjani hakuwa wa kutosha na ilishuhuidiwa mara kadhaa ukiingiliwa na magari mengine barabarani wakati timu ikienda uwanjani kwa mazoezi.

Wenyeji nchini Morocco wanasema inapowadia mechi, huwa wanaogopa kwa sababu mara nyingi hutokea vurugu ya damu kumwagika.

Kwa ujumla Stars inaingia katika mchezo wa leo katika hali ya wasiwasi na woga mkubwa.

Stars itashuka dimbani saa 3:00 usiku leo kwa saa za hapa sawa na saa 5:00 za Tanzania kucheza na Morocco.

Stars inashika nafasi ya pili katika Kundi C, ikiwa na pointi sita nyuma ya Ivory Coast yenye pointi saba, ambayo kesho itakuwa ugenini ikimenyana na Gambia katika mchezo mwingine wa kundi hilo.

Stars ilitua hapa Jumatatu ikitokea Ethiopia ambako iliweka kambi ya wiki moja na kucheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Sudan, ulioisha kwa sare ya bila mabao.

Kabla ya kuja hapa, Stars iliweka kambi ya wiki moja katika hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam ikijifua Uwanja wa Karume na siku chache kabla ya kuondoka ilialikwa Ikulu na Rais Jakaya Kikwete, aliyewapa hamasa kwa hotuba nzuri.

No comments:

Post a Comment