KATIBU mkuu wa Tanzania Professional Boxing Organisation (TPBO), Ibrahim Kamwe ambaye anajulikana kwa jina la bigright amejitoa  katika uongozi wa chama cha ngumi kama kiongozi.

Bigright ambae ukiondoa mambo ya kichama mara nyingi amekuwa akiwaongoza maofisa wa chama hicho katika shughuli mbalimbali na mapambano mengi kama jaji mkuu ,mhifadhi rekodi za mabondia na mshauri katika shughuli za kiufundi.

Akizungumza na MICHARAZO, Kamwe amesema ameamua kupumzika shughuli za TPBO na kurudi kwenye ufundishaji wa vijana na kuendelea na kampuni yake ndogo ya bigright promotion ambayo inajihusisha na utayarishaji wa matamasha na uandaaji wa mapambano ya ngumi.
"Kwa kuwa naupenda mchezo wa ngumi  nimefanya shughuli hii kwa muda mrefu kukiwa   na utatautata wa hapa na pale   na yote hii kwa ajili ya kuuendeleza mchezo wa ngumi nchini lakini imekuwa ni ngumu kwangu kuendelea na wadhifa huo," alisema na kuongeza;
"Nawashukuru maofisa wenzangu wamekuwa wakinipa ushirikiano wa karibu. Ila kwa sasa najitoa katika uongozi na nitajihusisha na ngumi kivingine ikiwemo kuwaendeleza vijana na kuandaa mapambano madogomadogo ya kukuza vipaji," alisema.