STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, February 4, 2015

MWANASHERIA MKUU AKATA MZIZI WA FITINA MAHAKAMA YA KADHI

http://www.thecitizen.co.tz/image/view/-/2604484/highRes/932159/-/maxw/600/-/d4xms2z/-/AG_Masaju.jpg
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju akizungumza na wanahabari
http://mtanzania.co.tz/wp-content/uploads/2015/01/5.jpg
Viongozi wa Kiislam wakizungumza na wanahabari kupinga tamko la Jukwaa la Wakristo waliopinga Mahakama ya Kadhi kujadiliwa bungeni hivi karibuni
TEC
Viongozi wa Jukwaa la Wakristo wakitoa msimamo wao wa kupinga Mahakama ya Kadhi kujadiliwa bungeni ikiwa kama sehemu ya msimamo wao wa kuikata tamaa mahakama hiyo ianzishwe nchini
WAKATI viongozi wa Kikristo wakiendelea kushupaa na kuipinga kwa nguvu Mahakama ya Kadhi inayoliliwa na Waislam nchini Tanzania, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju ameweka wazi kwamba hakuna jambo baya juu ya uwepo wa mahakama hiyo kama inavyolazimishwa kuaminishwa.
Kwa mujibu wa gazeti la NIPASHE, limedokeza kuwa wakati muswada wa kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi ukitarajiwa kujadiliwa katika mkutano wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, amesema haitakuwa na athari yoyote hasi nchini.
Masaju alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza katika mahojiano maalum na NIPASHE jijini Dar es Salaam akifafanua juu ya muswaa huo hasa baada ya kuwapo kwa dalili za mvutano kuhusu uanzishwaji wa mahakama hiyo.
Alisema tatizo lililopo ni kwamba serikali haijachukua hatua madhubuti kuwaelimisha wananchi namna ambavyo mahakama hiyo itakuwa inaendesha kazi zake.
“Suala la Mahakama ya Kadhi limekuwapo tangu zamani na ilikuwa ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, Serikali hatuoni kwa nini suala hili lisifanikiwe,” alisema.
Masaju alisema Watanzania lazima watambue kuwa Mahakama ya Kadhi itahusu mambo ya Waislamu wenyewe ambayo ni mirathi, ndoa na talaka.
“Sioni kwa nini isifanikiwe kwa sababu mahakama hii haiwahusu watu ambao siyo Waislamu na pia haitakuwa ya kulazimisha,” alisema.
Alisema Mahakama hiyo kwa sababu itakuwa inashughulikia masuala binafsi kama ndoa na talaka ambayo serikali haishughuliki nayo.
Alisema serikali imekuwa ikishughulika na masuala ya jinai kama vile wizi, watu wanaokula rushwa hivyo mambo binafsi kama ya talaka haishughuliki nayo.
Aliongeza kuwa kujiunga katika Mahakama ya Kadhi itakuwa ni hiari hata miongoni mwa Waislamu na gharama za uendeshaji wake serikali haitahusika.
Masaju alisema suala hilo kama wananchi wakielimishwa haliwezi kuleta mgogoro kwa kuwa ni kitu cha kawaida na linafanyika katika baadhi ya nchi.
Alisema kimsingi suala hilo linakuzwa na baadhi ya vyombo vya habari na kusisitiza kuwa Watanzania ni wamoja na watabaki kuwa wamoja.
Aliongeza kuwa watu ambao hawataki mahakama hiyo wataenda kwenye mahakama nyingine za kawaida.
“Pamoja na Mahakama ya Kadhi kuamua masuala hayo, mahakama za kawaida zitabaki kuwa na mamlaka ya kusikiliza masuala ya talaka, mirathi na ndoa,” alisema.
Alisema wakati wa Bunge Maalum la Katiba Waislamu walitaka suala hili liingizwe katika Katiba mpya, lakini serikali iliona yasiingizwe kwa sababu ni ya imani za dini na hivyo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliahidi serikali itapeleka muswada bungeni.
Akijibu swali la kwamba huenda kuwasilishwa bungeni kwa muswada huo sasa kunalenga kuvuruga Watanzania kuacha kufikiri masuala muhimu yaliyopo mbele kama uchaguzi mkuu, Masaju alisema siyo kweli.
Alifafanua kuwa masuala yote kama ya kura ya maoni kuamua Katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu yote yana umuhimu na yataenda sambamba.
“Wakristo ni majirani wa Waislamu, Waislamu na Wakristo wanaishi pamoja, katika baadhi ya familia wengine kuna Waislamu na Wakristo, mwanasheria mmoja aliniuliza ni amri ipi iliyokuu kuliko yote akasema, mpende Mungu wako kwa moyo wako wote, mpende jirani yako kama nafsi yako, Waislamu ni jirani zetu,” alisema.
Masaju alisema kutugwa kwa sheria hii ni kuwezesha Mahakama ya Kadhi kufanya kazi kwa kufuata utaratibu bila kuingilia mambo mengine ya serikali.
“Hii siyo mara ya kwanza kutunga sheria. Mtusaidie kama taifa, sioni sababu Watanzania kupigana na kupinga suala la Mahakama ya Kadhi na kusababisha kuvunjika kwa amani,” alisema.
Aliongeza kuwa Zanzibar wana Mahakama ya Kadhi, hivyo itakuwa jambo la kushangaza kwa nini Tanzania Bara kusiwe na mahakama hiyo hali ambayo italeta manung’uniko kwa Waislamu waliopo bara.
Alisema kwa waliosoma Chuo Kikuu cha Sheria Dar es Salaama suala la mahakama ya Kadhi hufundishwa kwa mwaka mzima ili kulielewa vizuri.
Alisema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inatumika hata Zanzibar, hivyo siyo jambo zuri bara kusiwe na Mahakama ya Kadhi kwani itawafanya Waislamu waliopo bara wasononeke.
“Tumeona Waislamu wanaona na Wakristo, hiki ni kitu cha kawaida kabisa hakuna sababu ya kulipinga, sisi wote tunategemeana, sisi ni ndugu, binadamu tunaoishi pamoja.
Suala la Mahakama ya Kadhi limekuwa likizungumzwa sana bungeni tangu Augustino. Mrema alipopeleka hoja binafsi akidai Mahakama hiyo mwaka 1998.
Tangu wakati huo mwaka 1998 - 2000 iliundwa kamati ndogo ya Bunge kulishughulikia suala hilo chini ya Mwenyekiti wa wakati huo, Arcado Ntagazwa, aliyekuwa mbunge wa Muhambwe  na baadaye liliibuliwa tena mwaka 2002 na Thomas Ngawaiya aliyekuwa mbunge wa Moshi Vijijini na likashughulikiwa na Kamati ya Katiba, Utawala na sheria chini ya Mwenyekiti wa wakati huo, Athumani Janguo akiwa mbunge wa Kisarawe.
Baadaye suala hilo lilirudishwa serikalini chini ya Tume ya Kurekebisha Sheria kati ya 2006 -2008. Tume hiyo ilikuwa chini ya Mwenyekiti Profesa Ibrahimu Juma.
Viongozi wa Kikristo wamekuwa wakipinga kuwepo kwa Mahakama hiyo, huku Waislam wakiililia kwa kudai ni haki yao katika kushughulikia kesi zinazowahusu waumini wake ambao misingi yao ipo kwa muongozo wa Qur'an na Mafundisho ya Mtume Muhammad SAW.
Msimamo wa AG Masaju unaendana na ukweli kuwa yapo mataifa yenye waislam wachache lakini yana Mahakama hiyo ya Kadhi na kuwa wanachama wa OIC jambo jingine linalopingwa nchini na viongozi wa Kikristo na mambo yao yanaendelea bila ya hofu wala tatizo kama inavyoelezwa kama njia ya kukwamisha jambo hilo nchini.

No comments:

Post a Comment