STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, September 26, 2011

Anti Fifi: Jimama linalotesa Bongo Movie, sasa ageukia utunzi wa vitabu







WAKATI mastaa wenye majina na umaarufu mkubwa kama wake nchini hupenda kuishi maisha 'bandia' ya kuhofia kujishughulisha na kazi au kujichanganya na watu
wengine wa kawaida, kwa Tumaini Biligimana au 'Anti Fifi', hali ni tofauti.
Licha ya umaarufu alionao kupitia sanaa aliyoanza kuifanya zaidi ya miaka 20 akianzia kama promota wa urembo, disko na muziki wa kizazi kipya, Anti Fifi anauza 'genge' la chakula eneo la Mwananyamala, alipika na kuuza mwenyewe.
Pia, nyota huyo haoni aibu kula 'chips dume' (mihogo ya kukaanga) au kupanda daladala katika mizunguko yake jijini Dar, licha ya kumiliki gari zuri la kisasa.
"Siwezi kuhofia kuishi nilivyozoea kwa sababu ya jina kubwa, kuishi 'bandia' ndiko kunakoponza mastaa wengi kuishia kwenye machafu wakitafuta mkato ya maisha ili waonekane bab'kubwa," alisema.
Alisema, tangu alipoanza kupata umaarufu hajawahi kuona aibu kujichanganya na watu wengine, jambo alilodai limemrahisishia mambo yake mengiu kimaisha na kisanii.
Anti Fifi, aliyefanya kazi na madansa wa nyota wa zamani kama Black Mosses, Master
Flash na wengine, alisema kitendo cha kupika na kuuza chakula katika mgahawa wake kumemfanya apate wateja wengi, baadhi wakienda ili kujiridhisha kama kweli ni yeye au wanamfananisha na mtu wanayemuona kwenye filamu.
Msanii huyo alisema anavyofahamu yeye, ustaa wa mtu kujizuia na matendo machafu na ya aibu mbele ya jamii, ila sio kuogopa kujichanganya au kuishi vile mtu apendavyo au alivyozoea.
"Ustaa ni kujiheshimu, kujithamini na kujichanganya na watu ili kujifunza mengi toka kwao yanayoweza kumsaidia msanii katika kukuza sanaa yake, sio kuishi maisha bandia ya hadhi ya juu, ilihali uwezo huo mtu hana," alisema.
Muigizaji huyo ambaye pia, ni mtunzi, mtayarishaji na mwandishi wa vitabu, alisema mbali na kuuga mgahawa, pia anajiuza mayai ya jumla katika nchi jirani, sambamba na nguo na vipodozi vya wanawake na watoto.
Alisema anaamini wasanii wakiamua kuishi jinsi walivyo kabla ya kupata umaarufu wanaweza kujiepusha na skendo chafu ambazo zimekuwa ni mazoea kwao na kuitia doa sanaa yao kwa ujumla.
"Sijisifii, ila mie ni baadhi ya wasanii wanaojiheshimu kwa vile naishi jinsi nilivyo, hivyo sikumbwi na skendo kwa kusaka umaarufu, bali kazi zangu ndizo zinazonipa 'ujiko' mbele ya jamii, kama unavyojua majuzi tu filamu niliyotunga ya 'Senior Bachelor' ilitwaa tuzo ZIFF."
Anti Fifi anayependa kula ugali kwa samaki na dagaa na kunywa juisi ya karoti na passion, alisema tangu atumbukie kwenye sanaa amenufaika kwa mengi, ikiwemo umaarufu, kujenga nyumba, kumiliki gari na kiwanja alichoanza kukijenga nyumba nyingine eneo la Mbezi.
"Najivunia sanaa pia, imenisaidia kuweza kutunga na kuuza hadithi za filamu, huku kwa sasa nikiwa nimetumbukia kwenye utunzi wa vitabu, nikijiandaa kutoa kitabu kiitwacho 'Migogoro ya Ndoa na Suluhisho Lake'," alisema.
Anti Fifi, aliyewahi kuishi maisha ya ndoa ya kiislam kuanzia mwaka 1989-2001 alipoachika, alisema matarajio yake ni kutaka kujitofautisha na wasanii wengine nchini akitaka kuwa mtunzi mahiri wa vitabu na filamu kwa ujumla.
Anti Fifi, aliyeokoka kwa sasa, alisema kama angekutana na Rais angemuomba asaidie kuiinua sanaa nchini na kukomesha uharamia, ili inawanufaishe wasanii.
"Hata mimi ningekuwa Rais ningeyafanya hayo, pamoja na kuondoa kero ya umeme nchini, kwani ni aibu kwa Tanzania yenye vyanzo vingi vya kuzalisha nishati hiyo kuwa na tatizo la ukosefu wa umeme na kuliingiza taifa kwenye hasara kubwa,: alisema.
Tumaini Biligimana, aliyezaliwa Julai 17, 1965 mjini Kigoma, akiwa mtoto wa sita kati ya 13 wa Mzee Biligimana, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama aliposhiriki filamu ya Dar es Salaam akiigiza kama Jimama la Kikongo, linaloendesha genge la mabinti wahalifu, kiasi cha kufuatiliwa na Polisi, waliodhani huenda ndivyo alivyo.
"Huwezi amini nilifuatiliwa na Polisi kwenye duka na saluni yangu wakinipeleleza kwa kile walichokiona kwenye filamu hiyo niliyoiigiza mara nilipotua Dar nikitokea Kigoma," alisema.
Kisanii, Anti Fifi mwenye watoto watatu, Mohamed, 24 anayesoma kidato cha tano nchini Uganda, Omari, 21 anayesomea ufundi VETA na Zamda, 17 aliyepo kidato cha pili Shule ya Sekondari Kunduchi Beach, alianza tangu shuleni akicheza ngoma, kuimba na kupiga filimbi.
Alisema pia alikuwa mahiri wa kuchora, kubinuka sarakasi wakati wakisoma Shule ya Msingi Muungano na baadae Ujiji Sec, kabla ya kuajiriwa serikalini kama Mhasibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.
Baada ya miaka tisa ya utumishi wa umma, aliacha kazi hiyo na kujikita katika biashara akiwa promota wa fani ya urembo na disko, hadi mwaka 2001 aliposhiriki uzinduzi wa filamu ya Girlfriend na kupata kiu ya kuwa muigizaji baada ya kukutana na George 'Tyson' Otieno.
Alianza fani hiyo kwa kutunga na kuigiza filamu ya kwanza iitwayo Haraka ya Maisha ya mwaka 2002 kabla ya kuja Dar miaka miwili baadae kujiunga na kundi la Fukuto Arts na kushiriki filamu ya Dar es Salaam iliyomfungulia neema ya mafanikio.
Kazi nyingine alizoshiriki ni pamoja na Copy, Sound of Death, Senior Bachelor, I Deserve It, Kaburi la Mapenzi, Kizungumkuti, Fake Smile, Daddy, na nyinginezo baadhi akizitunga.
Anti Fifi anayechizishwa na rangi ya zambarau na pinki, alisema anawazimia Jacob Stephen 'JB', Irene Uwoya na Aunty Ezekiel, aliwaasa wasanii wenzake wajitume na kujichanganya kusaka maisha nje ya sanaa zao, kwa lengo la kuepusha kutumiwa ovyo.

No comments:

Post a Comment