STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, September 26, 2011

Golden Boy, kuzinyuka na Miyeyusho

BINGWA wa UBO-Mabara, Mbwana Matumla 'Golden Boy' anatarajia kupanda ulingoni mwezi ujao kuzipiga na bondia Francis Miyeyusho katika pambano la kutetea taji lake litakalofanyika jijini Dar es Salaam.
Pambano hilo la uzani wa Bantam litakalokuwa la raundi 10, litafanyika Oktoba 30 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, likisindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Kwa mujibu wa kocha msaidizi wa kambi ya Kinyogoli Foundation inayowanoa mabondia watakaosindikiza pambano hilo la Matumla na Miyeyusho, Rajab Mhamila ni kwamba maandalizi ya pigano yanaendelea vema.
Mhamila, alisema pamoja na kwamba pambano hilo ni la kuwania taji la UBO, lakini pia limewagawa mashabiki wa ngumi kulingana na mahali wanapotoka mabondia hao nyota, ambapo Matumla yeye anatokea Temeke na Miyeyusho akitokea Kinondoni.
"Pambano la Matumla na Miyeyusho ni kama la watu wa Temeke na Kinondoni, huku yale ya utangulizi yatahusisha mabondia wa pande hizo mbili, hali inayofanya pigano hilo lijalo kuwa na msisimko wa aina yake," alisema Mhamila.
Mhamila, alisema pambano hilo la UBO limeratibiwa na Mood Bawazir wa kampuni ya Dar World Links na litasindikizwa na michezo ipatayo mitano ya utangulizi kati ya hiyo ni pigano linalosubiriwa kwa hamu kati ya Ramadhani Shauri wa Kinondoni dhidi ya Issa Sewe kutoka Temeke.
Pigano hilo la Matumla, linakuja miezi minne tangu bondia huyo alipopanda ulingoni na kulitetea taji lake hilo kwa kumchakaza Mkenya, Gabriel Ochieng katika pambano lililofanyika Mei Mosi, kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
Mabondia wote wawili yaani Matumla na Miyeyusho kwa sasa wapo kambini wakijifua kwa ajili ya pambano hilo, kila mmoja akitamba kuibuka na ushindi siku ya pigano hilo.

Mwisho

No comments:

Post a Comment