STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, September 26, 2011

CBP yataka mrithi wa Shaaban Robert apatikane




WATUNZI na waandishi wa kazi za Fasihi nchini, wamepewa changamoto ya kujibidiisha katika fani zao, ili kumpata 'Shaaban Robert' mpya miongoni mwao atakayeendeleza na kudumisha fasihi katika kiwango alichokuwa nayo gwiji huyo.
Aidha jamii imeaswa kujenga utamaduni wa kuwanunulia na kuwasomea vitabu vya hadithi watoto wao kama njia ya kuchochea uwezo wao kuelewa na akili ambao utawasaidia katika masomo ya kitaaluma.
Katibu Mtendaji wa Mradi wa Vitabu vya Watoto Tanzania, CBP, Pili Dumea, ndiye aliyetoa wito huo kwa waandishi wakati wa ufungwaji wa semina ya siku tatu ya Waandishi wa Vitabu Kanda ya Mashariki, EZAA, iliyofanyika Mlandizi, mkoani Pwani.
Dumea, alisema watunzi na waandishi chipukizi wa kazi za fasihi wanapaswa kufanya kazi zao kwa umahiri, ili waweze kuja kumrithi Shaaba Robert, ambaye licha ya kufariki kitambo kirefu, bado amekosa wa kufikia umahiri wake katika fani hiyo.
"Semina na mafunzo haya yawe chachu kwenu katika kujibidiisha na kujituma katika fani hii mkiwa na lengo la kutaka kuwa warithi wa Shaaba Robert, ambaye licha ya kutokuwepo kazi zake zimeendelea kudumu milele," alisema Dumea.
Katibu huyo alisema CBP, ipo kwa ajili ya kuwasaidia watunzi na waandishi wa vitabu kufikia lengo la kuendeleza fasihi hasa vitabu vya hadithi vitakavyochochea maendeleo ya nchi kuanzia kwa watoto hadi watu wazima.
Pia, alisema jamii ni lazima iwe na utamaduni wa kuwasomea na kuwanunulia watoto vitabu kuwazoesha kusoma na kuchochea ufahamu wao na uwezo wao wa kimasomo darasani, akidai kusoma ni njia ya kusaidia uelewa na akili za mtu.
Naye Katibu Mkuu wa EZAA, Jackson Kalindimya, aliwaasa waandishi hao watumie vema uwezo wao wa 'kimungu' walionao katika kuchochea maendeleo ya nchi pamoja na kuijenga jamii katika maadili mema.
Kalindimya, alisema watunzi wa vitabu ambao wana uwezo wa kuumba dunia yao na viumbe wengine wakiwapa pumzi, tabia na uhusika unaoweza kuibadilisha jamii kutoka mahali pamoja hadi kwingine kimaendeleo na hata kimaadili kupitia kazi zao.
"Lazima mjivunie uwezo wa kimungu mlionao, kwa kuisaidia jamii kubadilika mahali ilipo hadi kwenye maendeleo, cha muhimu ni kutoa kazi nzuri zenye mvuto ambazo zitawafanya watu wazinunue na kuzisoma, kisha kuwabadilisha," alisema.

Mwisho

No comments:

Post a Comment