STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, July 27, 2013

Kazi ataka wajumbe TFF wakamilishe Kazi aanze Kazi

Osman Kazi akiwa kazini katika pambano la Wabunge wa Simba na Yanga
MWAMUZI wa zamani wa kimataifa, Osman Kazi amewaomba wajumbe wa mkutano mkuu wa uchaguzi wa shirikisho la soka (TFF) kuhakikisha wanachagua viongozi bora ambao wataleta maendeleo ya mchezo huo nchini.
Aidha mwamuzi huyo amesema anajiandaa kurejea tena kwenye kazi yake baada ya kujiondoa kimya kimya tangu alipokumbwa na adhabu ya kifungo cha miezi mitatu kwa tuhuma za rushwa.
Akizungumza na MICHARAZO, Kazi alisema anawaomba wapiga kura wa TFF kutofanya makosa katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Septemba.
Kazi alisema kosa lolote litakalofanywa na wajumbe hao wa TFF kunaweza kuirejesha nyuma nchi kama ilivyokuwa miaka iliyopita kabla ya uongozi wa Rais anayemaliza muda wake, Leodger Tenga.
Alisema wapiga kura wahakikishe wanachagua viongozi ambao watakuwa na maono ya mbele ili nchi irejeshe heshima yake katika medani ya kimataifa katika mchezo huo ikiwemo kutoa waamuzi katika michuano ya kimataifa.
"Rai yangu kwa wajumbe wa TFF wahakikishe hawafanyi makosa kwa kuchagua viongozi watakaoturejesha nyuma, wawachague viongozi bora na makini na wenye uchungu wa kweli na mchezo wa soka badala ya kushinikizwa kuchagua watu kwa uwezo wao kifedha," alisema.
Kuhusu hatma yake ya uamuzi, Kazi alisema anajiandaa kurejea tena dimbani ila itategemea na aina ya viongozi watakaoingia madarakani TFF.
Alidai kama watakuwa ni wababaishaji, ni bora aendelee na uratibu wake wa matamasha na kama watakuwa ni wenye weledi atashiriki Copa Test ya Desemba.
"Bado nina miaka sita mbele kabla ya kustaafu rasmi kwa sheria za kimataifa za urefa, hivyo kama viongozi watanivutia kwa uwezo wao nitarejea kwa kuanza Cooper Test ya Desemba ili mwakani niwanie beji ya FIFA niliyovuliwa kimizengwe tangu mwaka 2005," alisema Kazi.

No comments:

Post a Comment