STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, October 6, 2013

Mauaji ya Sheikh Rogo na wenzake yaiweka Mombasa roho juu

Sheikh Abou Rogo enzi za uhai wake. Mwanaharakati huyu wa Kiislama aliuwawa mwaka jana na juzi mrithi wake Ibrahim Rogo na wenzake waliuwawa kama alivyouwawa yeye kwa kupigwa risasi
HALI ya amani katika mji wa Mombasa imezidi kuwa tete, kutokana na makundi ya vijana wenye hasira kali kuendeleza machafuko katika viunga mbalimbali vya mji huo. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na BBC, jumla ya watu wanne wamepoteza maisha katika machafuko hayo, baada ya makundi ya vijana hao kupambana na askari wa kutuliza ghasia.


Habari kutoka nchini humo zinaeleza kuwa machafuko hayo yametokea siku moja baada ya kifo cha Sheikh Ibrahim Omar ‘Rogo’, aliyeuawa kwa kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana.

Katika shambulizi hilo, pia washirika watatu wa Sheikh Rogo nao wamepoteza maisha papo hapo, huku Salim Adbi akinusurika katika shambulizi hilo.

Kwa mujibu wa taarifa zaidi kutoka mjini Mombasa, vijana wenye hasira kali wameteketeza kanisa moja katika ghasia za juzi. 

Sheikh Ibrahim Rogo alikuwa mhubiri katika msikiti ambao ulikuwa unatumiwa kwa mahubiri na marehemu Sheikh Aboud Rogo, ambaye pia aliuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana mwaka jana.

Sheikh Aboud Rogo alishutumiwa kutoa mafunzo yenye itikadi kali yaliyowashawishi vijana kujiunga na kikundi cha kigaidi cha Al Shabaab.

Kabla ya kifo chake, marehemu Aboud Rogo alidaiwa kuwa na uhusiano na kundi la kigaidi la Al Shabaab.

Tukio la kifo cha Sheikh Ibrahim Omar ‘Rogo’ limetokea ndani ya kipindi cha wiki mbili baada ya shambulizi la kigaidi la Westgate Mall, ambapo jumla ya watu 67 walipoteza maisha.

Ibrahim Rogo alionekana kama mrithi wa marehemu Aboud Rogo, alipohutubu katika msikiti huo.

No comments:

Post a Comment