STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, December 30, 2013

Oscar Joshua 'aigwaya' Al Ahly Ligi ya Mabingwa Afrika

Oscar Joshua
BEKI kisiki wa timu ya Yanga, Oscar Joshua ameibuka na kuitahadharisha klabu yake kwa kuitaka kuwa makini na kujiandaa vyema kwa ajili ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ili ising'olewe mapema kwenye michuano hiyo.
Joshua, beki wa pembeni alisema mechi ambayo Yanga inapaswa kuwa makini nayo ni ile dhidi ya mabingwa watetezi wa michuano hiyo, Al Ahly ya Misri watakaocheza nao iwapo watafanikiwa kuing'oa Komorozine ya Comoro.
Joshua alisema Al Ahly ndiyo timu pekee inayoonekana kuwa kikwazo kwa Yanga na kama itajipanga na kuitoa itajifungulia njia ya kufanya vyema kwenye michuano hiyo itakayoishiriki mwakani.
Akizungumza na MICHARAZO, Joshua alisema Al Ahly ni hatari sana kwa Yanga, lazima klabu yao ijiandae na kujipanga vyema.
"Al Ahly ni hatari sana wale, ni muhimu kwetu kujipanga vyema ili kuweza kuwatoa. Hii ndiyo timu tishio kwa Yanga michuano ya mwakani," alisema.
Beki huyo anayemudu nafasi nyingi uwanjani mbali na kucheza kama beki wa kushoto alisema, kwa kikosi kilichopo Yanga ikijipanga inaweza kufanya maajabu.
Yanga inatarajiwa kuvaana na Al Ahly katika mechi ya raundi ya kwanza mapema mwezi Machi, na hii ni iwapo tu watafanikiwa kuindosha mashindanoni Komorozine ya Comoro wanaotarajiwa kuanza nao kwenye hatua ya awali kati ya Februari 7-9 na kuridiana nao wiki mbili baadaye.
Rekodi pekee ya Yanga ya kujivunia kwenye michuano hiyo ya Afrika ni kucheza hatua ya makundi mwaka 1998 na kucheza Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika mara mbili mfululizo 1969 na 1970.

No comments:

Post a Comment