STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, January 24, 2014

Mtibwa Sugar yaikamia Azam


Kocha wea Mtibwa Mecky Mexime
KOCHA wa Mtibwa Sugar, Mecky Mexime amesema vijana wake wapo tayari kuvaana na Azam kwenye mechi ya fungua dimba la duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara inayoanza kesho akisema ama zao au za Azam.
Mexime alisema maandalizi waliyofanya na mechi chache za kujipima nguvu walizocheza yamewafanya wachezaji wake kuiva tayari kuipigania timu yao ili iweze kufanya vyema kwenye duru hilo aliloliita la 'kufa au kupona'.
Mtibwa waliomaliza kwenye nafasi ya sita katika duru la kwanza watakuwa wageni wa Azam kwenye uwanja wa Azam Complex, huku wakiwa na rekodi ya kutoka sare ya 1-1 katika mzunguko wa kwanza.
"Tunashukuru vijana wangu wote wapo fiti, hakuna majeruhi hata mmoja na tunamalizia maandalizi ya mwisho kabla ya kuja Dar kuvaana na Azam. Tumepania kupata ushindi ili kujiweka pazuri," alisema Mexime.
Nahodha huyo wa zamani wa Mtibwa na Taifa Stars, alisema anafahamu Azam ni timu nzuri na imekuwa ikiwapa upinzani wanapokutana nayo, lakini safari hii wanakuja kivingine kuhakikisha wanapata ushindi mechi zao za ugenini.
"Ingawa Azam ni timu ngumu na isiyotabirika, lakini wajiandae kwa kipigo kwa sababu tumepania duru la pili tufanye vizuri zaidi na ilivyokuwa duru la kwanza," alisema Mexime anayesaidiana na wachezaji wenzake wa zamani, Zuberi Katwila na Patrick Mwangata.

No comments:

Post a Comment