STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, January 6, 2012

Bella awang'onga wasanii Bongo



RAIS wa bendi ya Akudo Impact, Christian Bella, amewataka wasanii wa Kitanzania kujenga mazoea ya kuwashirikisha wasanii wenye majina makubwa wa kimataifa na wanaoimba miondoko tofauti na yao kwa lengo la kuteka soko la kimataifa.
Pia, amesema bila bendi za Tanzania kubadilika na kuachana na kuiga kazi za wasanii wa nje hasa wakongo, ni vigumu kuweza kutamba katika soko la kimataifa kwa vile watu wanaowaiga tayari wameshajiwekea mizizi ya kutosha karibu kila kona ya dunia.
Bella, alisema mtindo anaoutumia AY kuwashirikisha wasanii mbalimbali wa kigeni unapanua wigo wa kazi za msanii huyo kufahamika kimataifa na kumtangaza vema.
Alisema jambo hilo linapaswa kuigwa na wengine, ambao wamezoea kufanya kazi na wasanii wenzao wa nyumbani au wanaoimba miondoko inayofanana.
"Unaona nimemshirikisha Isha Mashauzi katika kazi yangu 'Kilio cha Maskini' kwa lengo la kuteka mashabiki wa taarab, ila kwa kujitangaza kimataifa, lazima tuwashirikishe wasanii wa kigeni wenye majina makubwa tujitangaze," alisema.
Alisema wasanii wa Bongo wajiulize inakuwaje, Fally Ipupa aimbe na nyota wa Nigeria na miondoko yao haifanani, kisha wamwangalia AY na jitihada zake kisha wafuate nyayo hizo kwani zitawatangaza kimataifa tofauti na sasa.
Aliongeza, bendi za muziki wa dansi nchini ziache tabia ya kuiga kazi za wasanii wa nje hasa wakongo badala yake wabuni kazi zao wenyewe ili waweze kuteka soko la kimataifa.
Bella alisema bendi za Kibongo haziwezi kutamba soko la kimataifa kwa kupiga kama Koffi au JB Mpiana wakati kazi za wasanii hao zinatambulika karibu kila kona ya dunia.

Mwisho

No comments:

Post a Comment