STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, January 6, 2012

Oswald, Njiku, Palasa kuwasindikiza akina Cheka

MABONDIA wanaotamba kwenye mchezo wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Oswald, Chaurembo Palasa na Deo Njiku wa Moogoro wanatarajiwa kupanda ulingoni kuzichapa kusindikiza pambano la Francis Cheka dhidi ya Karama Nyalawila.
Cheka na Nyalawila wanatarajiwa kupigana Januari 28 kwenye pambano lisilo la ubingwa litakalofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri, Morogoro ambapo mratibu wa pambano hilo, Philemon Kyando 'Don King' ametangaza michezo ya utangulizi.
Kyando, ambaye ni Mkurugenzi wa Don King Kyando Promotion, alisema kabla ya Cheka na Nyalawila kupanda ulingoni kupigana, mabondia 10 tofauti watawasindikiza ambapo Chaurembo Palasa anatarajiwa kuzichapa na Deo Njiku.
Mabondia wengine watakaopigana katika pambano hilo la akina Cheka litakalokuwa na raundi 10 uzani wa Super Middle ni mkongwe Maneno Oswald aliyeambulia sare hivi karibuni mbele ya mkongwe mwenzake, Rashid Matumla atakayepigana na Hamis Ally wa Morogoro.
"Mapambano mengine ya utangulizi yatawahusisha, JUma Idd wa Dar dhidi ya JUma Afande wa Morogoro, pia kutakuwa na pambano jingine litakalowakutanisha mabondia wa kike watakaoonyeshana kazi siku hiyo," alisema Kyando.
Promota huyo aliyekuwa kimya kwa muda mrefu, alisema michezo hiyo ya Januari 28 itakuwa maalum kwa uzinduzi wa kampuni yake sambamba na kumpongeza Mbunge wake wa Jimbo la Morogoro, Aziz Abood kwa kusaidia maendeleo ya jimbo hilo.
"Unajua mie natokea eneo la Kihonda na nimekuwa nikivutiwa na kasi anayofanya mbunge huyo katika kuleta maendeleo ndio maana nimeandaa pambano hili la Cheka na Nyalawila lifanyike Morogoro kama kuunga mkono juhudi zake," alisema Kyando.
Kyando, aliyetamba miaka ya 1980 na 2000 kabla ya kuzimika, alisema ujio wake mpya utaenda sambamba na kuwainua mabondia chipukizi waliopo kila kona ya nchi badala ya kufuata mkumbo wa mapromota wengine kung'ang'ania mabondia wa mijini tu.
Cheka anayefahamika kama SMG na Nyalawila maarufu kama 'Captain' watapigana likiwa pambano lao la pili kwani walishawahi kukutana na kushindwa kutambiana kwa kutoa sare, ingawa kila mmoja kwa sasa anashikilia mataji makubwa duniani.
Nyalawila ni bingwa wa dunia wa WBF, huku mpinzani wake akishikia mataji ya UBO, ICB na Kamisheni ya Ngumi ya WBC.

Mwisho

No comments:

Post a Comment