STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 16, 2013

Hatari!

  Fedha za serikali zabebwa bila ulinzi TFF
  Ni mamilioni yatokanayo na makato U/Taifa
 
Viongozi wakuu wa TFF, Rais Leodger Tenga (kulia) na Angetile Osiah (kushoto)
 
WIZARA inayoshughulikia michezo nchini imekuwa ikifanya kitendo hatari cha kutuma maafisa wake kwenda kubeba mamilioni ya fedha zitokanazo na mgawo wake utokanao na makato ya Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam bila ya ulinzi wowote ule kama taratibu za usafirisha fedha zinavyoelekeza, imefahamika.
 
Aidha, malipo ya mamilioni hayo ya fedha za serikali kutoka katika ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) hufanywa kwa fedha taslim na wala siyo kwa njia nyingine salama kama ya hundi, huku anayehusika kuzibeba ni afisa mmoja tu ambaye ni wazi kwamba anahatarisha usalama wake binafsi na pia wa fedha za umma.
 
Uchunguzi uliofanywa kwa siku kadhaa na NIPASHE umebaini kuwa utaratibu huo unaopingana pia kwa kiasi kikubwa na taratibu za malipo ya fedha za umma umekuwa ukifanyika kwa muda mrefu, hata kabla ya kuanza kutumika kwa Uwanja wa Taifa.
 
 
MAMILIONI YANGA v OLJORO
Juzi (Jumapili), mwandishi alishuhudia mmoja wa maafisa wa Wizara ya Michezo akifika katika ofisi za TFF na kubeba kienyeji (bila ya kusindikizwa na askari yeyote mwenye silaha) kiasi cha Sh. 7,552,500 zilizotokana na asilimia 15 ya uwanja katika mapato ya mechi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kati ya Yanga na Oljoro JKT iliyochezwa Jumamosi na kuingiza Sh. milioni 63.17.
 
Afisa huyo alionekana akitinga kwenye ofisi za TFF zilizopo Karume jijini Dar es Salaam saa 4:38 asubuhi, akiwa peke yake kwenye gari aina ya Suzuki Vitara (namba tunazihifadhi) na kuondoka peke yake pia kwenye gari hilo mishale ya saa 5:22 asubuhi.
 
Kibaya zaidi, afisa huyo aliyekuwa amevaa shati la mikono mifupi lenye rangi nyeupe, kaptula yenye mifuko mingi na viatu vya raba vyenye mchanganyiko wa rangi nyeupe na nyeusi, hakuwa na ulinzi wowote wakati akiingia na kutoka kwenye ofisi ya fedha ya TFF.
 
"Ofisi imefunguliwa leo Jumapili kwa sababu kuna mechi ya Simba dhidi ya Azam. Ni kweli afisa wa wizara amechukua fedha za mgawo wa uwanja. Mtafute afisa habari (Boniface Wambura) au katibu mkuu (Angetile Osiah)... wao wanaweza kuzungumzia kwa kina sababu za uchukuaji fedha kwa mtindo huu wa malipo ya fedha taslim," alisema mmoja wa watu waliokutwa katika maeneo ya ofisi za TFF kwa sharti la kutotajwa jina lake. 
 
MAMILIONI SIMBA v AZAM
Kwa kutambua kuwa juzi kulikuwa na mechi kali ya ligi kati ya Simba na Azam, NIPASHE ilipiga tena kambi jana asubuhi kwenye ofisi za TFF ili kuona kama utaratibu wa kuchukua mamilioni hayo ya serikali kwa malipo taslim utaendelea, na tena bila ya mbebaji kuambatana na askari wa kumlinda.
 
Ilipofika saa 3:11 asubuhi, afisa yule yule aliyejihatarisha Jumapili ndiye aliyetinga tena kwenye ofisi za TFF akiwa peke yake kwenye gari lilelile aina ya Suzuki Vitara.
 
Mwandishi alifuatilia kwa karibu nyendo za afisa huyo. Ni kwamba, baada ya kupaki gari lake, alionekana akisalimiana na maafisa kadhaa wa TFF, akiwamo kocha wa timu ya taifa (Taifa Stars), Mdenmark Kim Poulsen. IIimchukua takriban dakika 26 afisa huyo kukamilisha zoezi hilo maana saa 3:57 asubuhi ndipo alipoingia ndani na kwenda moja kwa moja kwenye chumba cha malipo na kubeba mamilioni yanayokadiriwa kuwa ni Sh.
 7,925,600, kiasi ambacho ni sawa na asilimia 15 ya mgawo wa uwanja kwani mechi hiyo ya Simba dhidi ya Azam iliyochezwa juzi iliingiza Sh. milioni 66.855.
 
Baada ya kubeba fedha hizo, afisa huyo alionekana akifungua mlango wa nyuma wa gari alilokuwa nalo na kuweka begi linalodhaniwa kuwa na fedha hizo kabla ya kuondoka. 
 
Hiyo ilikuwa ni saa 4:03 asubuhi. Mwandishi alijaribu kumfuatilia kwa nyuma. Saa 4:07, afisa huyo aliingia ndani ya Shule ya Sekondari Benjamin William Mkapa iliyopo umbali mfupi kutoka TFF.
 
Saa 4:12, afisa huyo aliondoka kwenye shule hiyo na kurejea tena TFF na kuingia ndani ambapo akiwa na begi lake dogo lenye fedha, bila kuwapo na ulinzi wowote, alikaa kwa dakika 23, baadaye alitoka na kuingia kwenye gari na kuondoka saa 4:35.
 
TFF wanena
Akizungumza na gazeti hili jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa TFF, Osiah alikiri kuwa serikali hutuma maafisa wake kubeba fedha hizo kwa malipo taslim kila siku moja baada ya mechi na utaratibu huo umekuwapo kwa muda mrefu.
 
"Ni kweli kwamba hata sisi tunatambua kuwa si vizuri kuwalipa pesa taslimu, tena ni kinyume cha sheria... lakini utaratibu huo umekuwapo kwa miaka mingi na sasa imekuwa kama desturi yetu," alisema Osiah.
 
Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema kuwa hata fedha za klabu zinachukua mgawo wake kwa njia hiyo, licha ya kuwapo kwa taarifa za tukio la kuporwa kwa Sh. milioni 10 za Simba katika eneo la Sinza Makaburini.
 
MICHAEL WAMBURA
Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Tanzania (FAT sasa TFF), Michael Wambura alisema jana kuwa utaratibu wa TFF kutoa fedha taslimu badala ya hundi kwa serikali ni kosa, lakini akasema kuwa imezoeleka hivyo na kwamba hata wakati wa uongozi wao (FAT), walikuwa na mfumo huo ambao anaamini kwamba siyo sahihi.
 
"Wakati tukiwa madarakani, tuliwahi kuamua kutumia utaratibu wa hundi lakini ulileta matatizo. Kuna watu hawakutaka kabisa utaratibu huo. Nafikiri kuna haja ya kufanya uchunguzi kujua ni kwanini hawataki utaratibu huo," alisema Wambura.

KAMANDA WA POLISI 
Alipotafutwa na NIPASHE jijini Dar es Salaam kuzungumzia taratibu za usafirishaji wa fedha, Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Charles Kenyela, alisema ni kosa kwa mtu yeyote kusafirisha kiasi kikubwa cha fedha za umma bila kuwa na ulinzi.
 
"Ni kosa kusafirisha fedha za umma na hata za watu binafsi pasipokuwa na ulinzi wa polisi ama vyombo vingine vya usalama vya serikali au kampuni za ulinzi za watu binafisi zinazotambuliwa kisheria," alisema Kenyela.
 
"Inashangaza kuona TFF na wizara hawatumii utaratibu wa benki (hundi) kulipana. Kulipana fedha taslimu, tena mamilioni ya fedha ni kuhatarisha usalama wa fedha na watu wanaozisafirisha," aliongeza Kenyela.
 
Wakati wa tukio la kudaiwa kuporwa kwa fedha za Simba baada ya mechi yao dhidi ya Black Leopards ya Afrika Kusini iliyochezwa Desemba 29, 2012, aliwahi kuonya kuwa hivi sasa, likitokea tukio lolote la kuporwa fedha huku wahusika wakiwa hawajaomba ulinzi, watakuwa wakianza kwa kuwakamata watu hao
waliobeba fedha hizo kiholela.
 
Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, alisema jana kuwa hawezi kulizungumzia suala hilo kwa sababu hakuwa katika mazingira mazuri ya kuzungumza kupitia simu kwa kuwa alikuwa safarini kuelekea jijini Dar es Salaam.
 
Hivi karibuni, watu kadhaa waliuawa katika tukio la uporaji wa Sh. milioni 150 
zilizokuwa zikisafirishwa bila ulinzi wa askari rasmi katika eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam.
 
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment