STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, November 5, 2013

Juventus yapatwa mchecheto kwa Real Madrid Ligi ya Mabingwa Ulaya

Wakali wawili wanaoipasua kichwa Juve kuweza kuwazuia wasilete maafa kwao
KOCHA wa Real Madrid, Carlo Ancelotti anaweza kuielekeza mlango wa kutokea klabu yake ya zamani ya Juventus sambamba na kocha wao, Antonio Conte wakati timu hizo zitakapokutana kwenye mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya huko Turin leo.
Hata hivyo, wasiwasi mkubwa kwa Juventus ni namna ya kuzima mashambulizi ya kushitukiza kutoka kwa nyota wa Real, Angel Di Maria, Cristiano Ronaldo na Gareth Bale."
Kiungo wa Juventus, Claudio Marchisio juzi alisema: "Tutachukua tahadhari dhidi ya mashambulizi ya kushtukiza kutoka kwa Di Maria, Ronaldo na Bale."
Timu hizo mbili kwa pamoja zimeshinda ubingwa wa michuano hiyo mara 11, Real mara tisa na Juve mara mbili, na zote zinatarajia kupata tiketi ya kusonga mbele hatua ya 16 bora kutoka Kundi B.
Lakini baada ya kutoka sare na Galatasaray na Copenhagen kabla ya wiki mbili zilizopita kupoteza 2-1 dhidi ya Madrid, Juventus sasa inaonekana kupumulia mashine ikisaka nafasi ya kusonga mbele.
Ancelotti hapendi kulikubali hilo, lakini ataonekana katika mtazamo tofauti kama atatoa mchango wa kuiondosha michuanoni timu hiyo.
Alikuwa na wakati mgumu katika miaka miwili aliyoiongoza Juventus, kwani licha ya kuiwezesha kumaliza nafasi ya pili mara mbili kwenye Series A, alitimuliwa siku ya mwisho mwishioni mwa msimu wa 2000-01.
Conte, ambaye ameiongoza Juventus kutwaa ubingwa wa Serie A, alikuwa nahodha wakati huo kabla ya kuibuka na kuwa miongoni mwa makocha bora barani Ulaya, ingawa kuna muda alikumbana na tatizo la kiuchumi klabuni hapo.
Kushinda kwa Real, ambayo katika rekodi za hivi karibuni za kuifunga Juve ugenini ilikuwa miaka 51 iliyopita, kutaiwezesha kutinga hatua ya 16 bora ikiwa na mechi mbili mkononi huku ikiiacha miamba hiyo ya Italia katika nafasi ya tatu na pointi zao mbili baada ya kucheza michezo minne.
Kama Galatasaray itashinda leo ugenini dhidi ya FC Copenhagen katika moja ya mechi za Kundi B, itajikuta ikibaki pointi tano nyuma ya mabingwa hao wa Uturuki huku ikiwa inasubiriwa na safari ya Istanbul mechi inayofuata.
Juventus imeshindwa kuibuka na ushindi mechi tano zilizopita za Ligi ya Mabingwa Ulaya, mbio hizo zikianzia ilipopoteza mechi zote mbili za robo fainali dhidi ya Bayern Munich msimu uliopita.
Hofu kubwa ni kwamba kati ya mechi hizo, tatu ilipoteza ikiwa uwanja wao wa nyumbani, wakati wakitarajia kusonga mbele.
Katika hatua nyingine, imeshinda mechi zake tatu za Serie A bila kuruhusu bao langoni mwao, jambo ambalo linatoa matumaini kwao kwamba huenda mabeki wa Real watakuwa na kazi ngumu kutokana na kuruhusu mabao matano kwenye mechi mbili zilizopita za La Liga.
"Real inawachezaji wazuri na bora katika safu yao ya ushambuliaji ambao mara nyingine wanasababisha presha kubwa kwa mabeki," alisema Kiungo wa Juventus, Claudio Marchisio juzi.
"Tulimudu kuzuia vema tulipocheza Hispania, na kufurahia umiliki wa mpira na kuwasababishia matatizo."
Juventus itamkosa beki Giorgio Chiellini, ambaye alitolewa nje kwa kadi wiki mbili zilizopita wakati wakicheza Uwanja wa Bernabeu, kutokuwapo kwake kunamfanya Marchisio kuwa mchezaji pekee katika timu ambaye alicheza wakati wakiifunga Real walipokutana Turin miaka mitano iliyopita.
"Hata tulipobaki 10, tulicheza vizuri kama timu na kutengeneza nafasi, lazima Jumanne (leo) tulifanye hilo tena wakati huo huo tukichukua tahadhari dhidi ya mashambulizi ya kushtukiza kutoka kwa Angel Di Maria, Cristiano Ronaldo n Gareth Bale."
"Pia, tukiwa Turin, tutapata sapoti kubwa kutoka kwa mashabiki wetu."

No comments:

Post a Comment