STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, February 13, 2014

Simba kuifuata Mbeya City kesho, kuvuna nini Sokoine?

Wachezaji wa Simba watashangilia kama hivi kwa Mbeya City au....!

Kinara wa mabao, Amissi Tambwe atawanyamazisha mashabiki wa Mbeya City Jumamosi uwanja wa Sokoine?
WEKUNDU wa Msimbazi, Simba inatarajiwa kuondoka kesho kwenda Mbeya kwa ajili ya kuwahi pambano lao dhidi ya wenyeji wao Mbeya City, ambayo imekuwa ikielezwa inajifua mchana wa jua kali ili kutafuta mbinu za kuendelea kuwatia machungu vijana wa Zdrakov Lugarusic.
Simba iliyotota kwa Mgambo JKT Jumapili iliyopita uwanja wa Mkwakwani kwa kufungwa bao 1-0, ilirejea jijini kwa ajili ya wachezaji kupata wasaa wa kukutana na Mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage ili kuweka mambo sawa kabla ya kuondoka kesho kwa ndege kuwa ajili ya mechi hiyo na Mbeya City.
Mbeya City inayonolewa na kocha Juma Mwambusi, ilitoshana nguvu na Simba kwa kytoka sare ya 2-2 katika pambano lililochezwa jijini Dar es Salaam mwaka jana, itaikaribisha Simba Jumamosi kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya ambayo umekuwa 'machinjio' kwa timu wapinzani.
Pambano hilo la Simba na Mbeya City linatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na nafasi ilizokuwa timu hizo ambapo Mbeya wameitangulia Simba kwa pointi tatu ikiwa nafasi ya tatu, nyuma yao 'mnyama' anafuata akiwa na pointi 31.
Vijana wa Msimbazi ambao tangu waanze kucheza mechi za ugenini kwenye duru la pili wamekuwa wakiyumba baada ya kunusurika kulala kwa Mtibwa Sugar waliotoka nao sare ya 1-1 kisha kwenda kuzama Mkwakwani, watalazimika kupata ushindi kwa Mbeya City ili kurejea nafasi ya tatu na kuwapumulia  watani zao Yanga. wanaoakamta nafasi ya pili nyuma ya Azam wanaoongoza ligi hiyo.
Simba ikiongozwa na kinara wa mabao katika ligi kwa msimu huu Amissi Tambwe na wakali wengine kama Ramadhani Singano 'Messi', Haruna Chanongo, Ali Badru, Awadh Juma, Jonas Mkude na kipa Ivo Mapunda hawatapenda kuona wakiteleza Jumamosi kwa Mbeya City iliyopanda ligi msimu huu.
Mbali na mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu siku hiyo pia kutakuwa na mechi nyingine kadhaa ikiwamo ya Mgambo JKT kuvaana na Rhino Rangers mjini Tabora, Ashanti United itaumana na Kagera Sugar uwanja wa Chamazi, jijini Dar na Oljoro JKT iliyokimbiwa na kocha wake Hemed Morocco itaikaribisha JKT Ruvu ambao jana waliteleza kwa ndugu zao wa Ruvu Shooting kwa kufungwa mabao 2-1.
Mechi nyingine siku hiyo ni Ruvu Shooting dhidi ya Coastal Union pambano litakalochezwa uwanja wa Mabatini-Mlandizi  mkoani Pwani.

No comments:

Post a Comment