STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, November 26, 2014

MTIKITISKO TENA! RIPOTI YA PAC NOUMA

http://www.bongo5.com/wp-content/uploads/2012/08/Zitto-Kabwe.jpg
MWENYEKITI wa PAC, Mhe. Zitto Kabwe
PRO. MUHONGO
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI JAJI WEREMA
MH.WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA
PROF. ANNA TIBAIJUKA
ZITTO: Kamati imebaini kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa barua yenye Kumb Na. AGCC/E.080/6/70 ya tarehe 18 Novemba, 2013 alimthibitishia Gavana kuwa hakukuwa na kodi ya Serikali katika fedha zilizokuwa kwenye Akaunti ya Tegeta ESCROW na kwamba fedha hizo zihamishiwe IPTL ili Serikali ijinasue na mashauri yasiyo na tija kwake.


Kutokana na mahojiano kati ya Kamati na Kamishina Mkuu wa TRA ilibainika kwamba Kampuni ya Piper Links haijulikani sio tu British Virgin Islands bali hata nchi nyingine. 



Kamati haielewi ni jinsi gani taasisi kubwa kama Benki Kuu ya Tanzania, Wizara ya Nishati na Madini, Wizara ya Fedha, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na nyingine zilizohusika katika suala hili, na ambazo tunaamini zimesheheni Watendaji wenye weledi, zimewezaje.


Wakati mahojiano ya Kamati na Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Kamishna Mkuu wa TRA pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU tarehe 19 Novemba, 2014 waliithibitishia Kamati kuwa kutokana na makubaliano wa Akaunti ya Tegeta ESCROW, sehemu ya fedha au fedha yote katika Akaunti hiyo ilikuwa ni fedha ya umma.


FILIKUNJOMBE: Kamati imethibitisha bila chembe ya mashaka kwamba mchakato mzima wa kutoa fedha katika akaunti ya Tegeta ESCROW uligubikwa na mchezo mchafu na haramu wenye harufu ya kifisadi ulioambatana na udanganyifu wa hali ya juu ambao kwa kufuata sheria tu ungeweza kugundulika na kuzuiwa.


BONYEZA MANENO HAYA KUSOMA RIPOTI YA ESCROW ILIYOWASILISHWA NA ZITTO KABWE BUNGENI

Kama unaona uvivu basi hata ni mapendekezo ya KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI (PAC) yaliyotolewa jioni hii Bungeni


3.2 Kamati inapendekeza kama ifuatavyo: -
3.2.1 Mheshimiwa Spika, Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) mara moja wachukue hatua ya kumkamata Bwana Harbinder Singh Sethi na
kumfikisha mahakamani kwa makosa ya Anti money laundering, ukwepaji kodi na wizi. Kamati pia inaelekeza Serikali kutumia sheria za Nchi, ikiwemo sheria ya ‘Proceeds of Crime Act’ kuhakikisha kuwa Bwana Harbinder Singh Sethi anarejesha fedha
zote alizochota kutoka Benki Kuu ya Tanzania. Kwa kuwa suala hili ni suala la utakatishaji wa fedha haramu, Mamlaka ziwasiliane na mamlaka za Nchi nyingine kuhakikisha mali za Bwana huyu
zinakamatwa na kufidia fedha hizo.97
3.2.2 Mheshimiwa Spika, Kamati imethibitsha kuwa Bwana James Rugemalira aliuza hisa ambazo Kampuni yake ya VIP inamiliki katika IPTL na kulipwa na Bwana Sethi kutoka katika Fedha za Akaunti ya Tegeta ESCROW. Kamati imethibitisha kuwa fedha
kutoka akaunti za Kampuni ya PAP katika Benki ya Stanbic zilizofunguliwa maalumu kwa ajili ya kupokea fedha kutoka Akaunti ya Tegeta ESCROW iliyokuwa Benki Kuu zilipelekwa katika Akaunti nambari 00151002368801 na Akaunti nambari 00151002368802 za Kampuni ya VIP ziliyopo Mkombozi Commercial Bank.
Kwa mujibu wa Taarifa ya CAG na kuthibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU fedha hizo pia ziligawiwa kwa watu mbalimbali binafsi. Kamati haina tatizo na watu wawili kuuziana makampuni yao kwa thamani wajuazo wenyewe, au jinsi ya kuzitumia fedha zao, ama kuwachagulia watu wa kuwagawia,
lakini Kamati imejidhihirishia kuwa fedha iliyotumika kulipia manunuzi hayo ni fedha ambayo sehemu yake ni ya umma iliyochotwa bila huruma wala aibu, kutoka Benki Kuu. Hivyo, Kamati inazitaka mamlaka za uchunguzi kuhakikisha kuwa fedha hizo zinarudi Benki Kuu hata ikibidi kwa kufilisi mali za watu wote 98
waliofaidika na fedha hizo kwa thamani ya fedha walizopewa na Bwana Rugemalira.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya waliofaidika na fedha hizo ni Viongozi wa Umma ambao wanapaswa kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma (Sheria namba 13 ya Mwaka 1995) ambayo inawataka kutoa taarifa ya zawadi wanazopokea au malipo wanayolipwa. Vyombo vya uchunguzi vifanye uchunguzi kutambua kama walifuata matakwa ya sheria na hatua mahsusi zichukuliwe, ikiwemo kuvuliwa nyadhifa zao zote za kuchaguliwa na/au kuteuliwa, kufilisiwa mali zao na kushtakiwa mahakamani kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara ya 132 (1) – (6).
3.2.3 Mheshimiwa Spika, Kamati pia imethibitisha kwamba fedha zilizolipwa kwa Watu binafsi zilitokana na Akaunti ya Tegeta ESCROW zilizolipwa kwa PAP ambayo si mmiliki halali wa IPTL.
Kwa maana hiyo fedha hizo zilitolewa kwa watu hao kama rushwa na kuzitakatisha fedha hizo haramu. Aidha, kamati inapendekeza kwamba Akaunti zote zilizohusika na miamala hii haramu ya Akaunti ya Tegeta ESCROW, akaunti zao zifungwe (freeze) na 99
wenye akaunti hizo walazimishwe kurejesha fedha hizo kwa mujibu wa Sheria (Anti Money Laundering) ikiwa ni pamoja na mali zao kufilisiwa. Kwa upande wa viongozi wa Kisiasa wawajibike na Watumishi wa umma wafukuzwe kazi.
3.2.4 Mheshimiwa Spika, Kamati imejiridhisha kwamba, suala la akaunti ya Escrow ni jambo la utakatishaji wa fedha (Money Laundering), kama alivyosema Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU
katika mahojiano yake na Kamati. Kamati inazitaka mamlaka zinazohusika, ikiwemo Benki Kuu kuzitangaza benki za Stanbic na Mkombozi Commercial Bank kama asasi za utakatishaji fedha
(Institutions of Money Laundering Concern).
3.2.5 Mheshimiwa Spika, Aidha, Kamati inalikumbusha Bunge lako tukufu pendekezo muhimu lililotolewa na Kamati Teule ya Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe kuhusu sakata la maarufu la Richmond. Kamati ilipendekeza:
“Mkataba kati ya TANESCO NA Richmond Development Company LLC na sasa Dowans Holdings S.A. kama ilivyo mikataba kati ya TANESCO na IPTL, SONGAS, AGGREKO 100 na Aistom Power Rentals inatoa unafuu usiostahili kwa makampuni hayo ya umeme na kuiumiza TANESCO na hatimaye watumiaji na walipa kodi kimapato, k.m. mikataba hiyo kuwa na vipengele vya kuibana TANESCO kuyalipa makampuni hayo kodi zinazohusika na uendeshaji (operations) matengenezo/marekebisho ya mara kwa mara ya mitambo (maintenance) gharama za bima, ada za mawakili na washauri elekezi (consultants)
gharama za mafuta na gesi ya kuendeshea mitambo,
gharama za ukodishaji mitambo (capacity charges)
ambazo TANESCO hulipa kila mwezi si chini ya wastani wa shilingi bilioni 2 kwa kila kampuni, izalishe au isizalishe umeme. Kamati Teule inatoa rai kwa Serikali kuwa mikataba yote hii ipitiwe upya mapema
iwezekanavyo kama ambavo mikataba ya madini
knavyopitiwa upya sasa na Serikali. Bila kufanya hivyo, mzigo mkubwa wa gharama za umeme utawaelemea wananchi na kushindwa kufikia azma ya Serikali ya maisha bora kwa kila Mtanzania.”101
Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kwamba, azimio hili litekelezwe kwa kupitia upya mikataba yote ya umeme ambayo inalitafuna Taifa letu.
3.2.6 Mheshimiwa Spika, Kamati imejiridhisha kuwa Bodi ya Shirika la Ugavi wa Umeme Nchini (TANESCO) bila sababu zozote za msingi ilikataa mapendekezo ya Menejimenti ya Shirika ya kutoruhusu uchotwaji wa fedha kutoka Benki Kuu akaunti ya Tegeta ESCROW
na hivyo kusababisha kulikosesha Shirika fedha zake inazohitaji sana kutokana na hali mbaya ya Shirika. Ikumbukwe kuwa Shirika la TANESCO lilipata hasara ya shilingi bilioni 467.7 katika mwaka wa fedha unaoishia Desemba 31, 2013. Hasara hiyo imekuwa
ikiongezeka mwaka hata mwaka toka mwaka 2010 (bilioni 5), 2011 (bilioni 43), 2012 (bilioni 177) na hivyo hadi kufikia Desemba 31, 2013, jumla yote kuu ya hasara (accumulated loss) ilikuwa imefikia shilingi trilioni 1.45.
Kamati pia imethibitisha kuwa Bodi ya TANESCO mpaka sasa haijatekeleza hukumu ya ICSID 2 na kukokotoa upya viwango vya malipo ya ‘capacity charges’ na hivyo kupelekea TANESCO na Serikali kuendelea kuilipa IPTL/PAP kila mwezi shilingi Bilioni 4.5 102 ($2.6m kila mwezi) izalishe au isizalishe umeme. Kamati inaitaka Serikali kuvunja mara moja Bodi ya TANESCO na TAKUKURU iwafungulie mashtaka ya matumizi mabaya ya ofisi wajumbe wote
waliohusika kupitisha maamuzi hayo ya kifisadi, ili iwe fundisho kwa wajumbe wengine wa bodi za Mashirika ya Umma kwamba watahukumiwa kwa maamuzi mabovu wanayoyafanya.
3.2.7 Mheshimiwa Spika, Kamati imethibitisha kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini aliingia makubaliano ya kutoa fedha katika Akaunti ya Tegeta ESCROW bila kujiridhisha kikailifu kuwa
maamuzi ya hukumu ya ICSID 2 yalikuwa bado kutolewa na hivyo kusababisha fedha kutolewa bila kukokotoa upya gharama za ‘capacity charges’, jambo ambalo limesababisha kupoteza fedha za umma.
Vile vile, Kamati imebaini kuwa, Katibu Mkuu hakufanya uchunguzi wa kina (due diligence) kujiridhisha uhalali wa Kampuni ya Mechmar kuuzwa kwa Piperlink na baadaye kuuzwa kwa PAP, na hivyo kusababisha fedha za akaunti ya Tegeta ESCROW kulipwa kwa asiyestahili na kinyume cha Mkataba wa akaunti ya Escrow.
Kwa maana hiyo, Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini, 103 pengine kwa uzembe wake ama kwa kukusudia kwa sababu
anazozijua yeye mwenyewe zaidi, amesaidia uchotwaji na hatimaye utakatishaji wa fedha haramu.
Mheshimiwa Spika, Kamati pia imethibitisha uzembe wa hali ya juu uliofanywa na Katibu Mkuu huyo, kushindwa kujiridhisha kama masharti ya Sheria ya kodi ya Mapato Sura ya 333, Kifungu cha 90(2) yalitekelezwa. Kifungu hicho kimsingi kinaitaka mamlaka ya ‘approval’’ ya uhamishaji wa Makampuni kutotambua Kampuni mpaka kwanza kodi za uhamishaji ziwe zimelipwa na hati za malipo ya kodi zimetolewa na mamlaka ya kodi.
Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa Katibu Mkuu huyu utenguliwe, na TAKUKURU wamfikishe mahakamani mara moja, kwa kuikosesha Serikali Mapato, matumizi mabaya ya ofisi na kusaidia utakatishaji wa fedha haramu.
3.2.8 Mheshimiwa Spika, Kamati imethibitisha kuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini alisema uongo Bungeni kwa kutamka kauli ambazo zilizokuwa na lengo la kupotosha umma kuhusu akaunti ya Tegeta ESCROW ikiwemo kutoa kauli ambazo zingeweza 104
kusababisha Nchi kuingia kwenye mgogoro wa kidiplomasia na nchi ya Uingereza.
Kamati inapendekeza kuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini (Madini) achukuliwe hatua kali za kinidhamu ikiwemo kutenguliwa  uteuzi wake. Kamati pia inapendekeza kuwa Naibu Waziri huyu afikishwe mbele ya Kamati ya Bunge ya Maadili ili aadhibiwe kama Mbunge kwa kusema uwongo Bungeni ili liwe fundisho kwa wabunge wengine kuhusiana na kauli wanazotoa ndani ya Bunge lako tukufu.
3.2.9 Mheshimiwa Spika, Kamati imethibitisha kuwa Waziri wa Nishati na Madini amekuwa, mara kwa mara, akilipotosha Bunge lako tukufu na Taifa kwa ujumla kuhusiana na Fedha za Akaunti ya Tegeta ESCROW kwamba ndani ya fedha hizo hakukuwa na fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, hata mtu wa kawaida angeweza kujua kwamba washirika wa ‘Tegeta Escrow Account’ ni akina nani na masharti ya kutoka kwa fedha hizo kwenye akaunti ni yapi kwa mujibu wa Mkataba wa uendeshaji wa akaunti hiyo. 105  Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, aidha kwa makusudi ama kwa sababu anazozijua vizuri zaidi mwenyewe, Waziri wa Nishati ananukuliwa kwenye kumbukumbu rasmi za Bunge, Kwa nguvu kubwa na kwa kujiamini, akitetea uchotwaji wa fedha hizo kinyume na masharti ya Mkataba wa Escrow.
Aidha, Kamati imebaini kuwa Waziri wa Nishati na Madini ndiye alikuwa dalali mkuu aliyewakutanisha Bwana Harbinder Singh Sethi na Bwana James Rugemalira, tena katika ofisi ya Umma; na pengine hii ndiyo iliyokuwa sababu ya upotoshaji huu. 

Waziri wa Nishati na Madini alifanya udalali huo akijua dhahiri kuwa Bwana Sethi hana uhalali wa kisheria kufanya biashara kwa jina la IPTL.
Iwapo Waziri wa Nishati na Madini angetimiza wajibu wake ipasavyo, Fedha za Tegeta ESCROW zisingelipwa kwa watu wasiohusika, na Nchi ingeweza kuokoa mabilioni yaliyopotea kama kodi za VAT, Capital Gain Tax na Ushuru wa Stempu ambazo ni
sawa na takribani shilingi bilioni 30. 106 Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kuwa Mamlaka yake
ya uteuzi itengue uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini kutokana sababu hizo zilizoelezwa.
3.2.10 Mheshimiwa Spika, Kutokana na kukua na hivi sasa kukomaa kwa vitendo haramu vya wizi wa fedha ama mali za umma na kukua ama kukomaa kwa vitendo vya rushwa kubwa na uhujumu uchumi, inapendekezwa kwamba Bunge lako Tukufu
liridhie kuitaka Serikali kuanzisha kitengo maalumu cha kushughulikia rushwa kubwa (grand corruption) kitakachokuwa na nguvu ya kuendesha mashtaka kwa uhuru kamili, na kwamba Bunge lako Tukufu liridhie kuanzishwa kwa Mahakama Maalum ya kushughulikia Rushwa kubwa itakayoshughulikia kesi za rushwa
zitakazokuwa zikipelekwa kwake na kitengo maalum cha kushughulikia rushwa kubwa.
3.2.11 Mheshimiwa Spika, Kamati imethibitisha kuwa
Mwanasheria Mkuu wa Serikali alitoa ushauri ulioipotosha Benki Kuu ya Tanzania kuhusiana na hukumu ya Jaji Utamwa J. Kwa kutumia madaraka yake vibaya, Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliagiza kodi ya Serikali yenye thamani ya shilingi 21 bilioni isilipwe 

107 na hivyo kuikosesha Serikali mapato adhimu. Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kujua na kwa makusudi alilipotosha Bunge na Taifa kwamba mgogoro uliopelekea kufunguliwa kwa Akaunti ya
ESCROW ulikuwa ni mgogoro wa Wanahisa wa IPTL badala ya mgogoro kati ya TANESCO na IPTL. Kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali utenguliwe mara moja na kisha afikishwe mahakamani kwa matumizi mabaya ya Ofisi
yaliyopelekea Serikali kupoteza mabilioni ya fedha.
3.2.12 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Waziri Mkuu kuhusiana na suala hili, Kamati iliipitia kwa umakini Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 iliyoainisha Kazi na Mamlaka ya Waziri Mkuu na kubaini kuwa, kwa mujibu wa Ibara ya 52 (1):
“Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti,
usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na
shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.”
Na, Ibara ya 52 (2), inayosema; 


108
“Waziri Mkuu atakuwa kiongozi wa shughuli za Serikali
Bungeni.”
Kisha Kamati ikajiuliza maswali kadhaa. Kwa mfano katika kutaka kubaini ukweli na kujiridhisha Kamati ilijiuliza maswali yafuatayo kuhusu Waziri Mkuu:
(a) Je, Waziri Mkuu alikuwa anajua sakata la utoaji wa
fedha katika Akaunti ya Tegeta ESCROW?
(b) Je, Waziri Mkuu alitimiza wajibu wake kwa mujibu wa Ibara ya 52(1)?
(c) Je, Waziri Mkuu wakati akitoa matamshi yake Bungeni alikuwa akitimiza wajibu wake kwa mujibu wa Ibara ya 52 (2)?
(d) Je, nini maana, uzito na ukweli wa matamshi ya mara kwa mara ya Waziri Mkuu ndani na nje ya Bunge
kuhusiana na suala hili?
(e) Je, Waziri Mkuu alitoa maamuzi au maelekezo yoyote ya kuzuia jambo hili lisifanyike?

109
Mheshimiwa Spika, Baada ya kupitia vielelezo vilivyomo kwenye ripoti ya CAG, Kamati imejiridhisha pasipo mashaka kuwa, Waziri Mkuu, alikuwa ana taarifa zote kuhusiana na mchakato mzima wa
kuchotwa fedha kutoka katika akaunti ya ESCROW.
Ushahidi ulioletwa na ofisi ya CAG kwenye Kamati unaonyesha kuwa Waziri Mkuu alikuwa akipata taarifa za jambo hili. Na Kamati imesikitishwa kuona kuwa Waziri Mkuu hakuchukua hatua zozote kuzuia muamala huu usifanyike.
Mheshimiwa Spika, Kamati, kwa kuzingatia kielelezo namba 22, inathibitisha bila shaka kwamba, Waziri Mkuu alikuwa analijua jambo hili vizuri na kwamba aliridhia muamala huu ufanyike. Ndiyo maana katika maelezo yake ya Bungeni mara kadhaa Waziri Mkuu
alithibitisha kuwa fedha za Escrow hazikuwa fedha za Umma. 

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Julius Nyerere katika kitabu chake cha Uongozi Wetu na Hatma ya Tanzania aliandika:
“…kubadili Waziri Mkuu sio jambo la ajabu. Ndugu
Rashid Mfaume Kawawa alikuwa Waziri Mkuu wangu 110 kwa muda mrefu. Hakuwa amefanya kosa lolote; lakini nilitaka kumbadili na kuteua Waziri Mkuu mwingine.
Nilimwita, nikamwambia hivyo. Tukakaa pamoja mimi
na yeye, tukashauriana na kukubaliana nani anafaa
kushika nafasi yake. Nikamteua Hayati Edward Moringe Sokoine. Najua kuwa watu wa aina ya Rashidi Kawawa ni adimu sana Duniani, hawazaliwi kila siku; hata hivyo ni jambo la kushangaza kidogo kwamba viongozi wetu wa Mageuzi, hata bado hatujafa, wanaona kuwa ni kosa kuwakumbusha kuwa vyeo walivyonavyo ni dhamana. Wanadhani kuwa Uwaziri ni Usultani; ukishakuwa Sultani utakufa sultani! Nadhani
kumbadili Waziri Mkuu sio jambo la ajabu. Anaweza
kujiuzulu, anaweza kufukuzwa Nchi isitikisike. Lakini
huwezi kumtimua Rais wa Nchi bila kuitikisa Nchi
yenyewe. Ni vizuri jambo hili likatamkwa waziwazi na
likaeleweka sawasawa. Maana watu wengine
wananong’ona nong’ona kuwajibika kwa Rais kana 111
kwamba ni jambo la mchezo mchezo tu. Kulazimika
kumchukulia hatua Rais wa nchi ni mkasa na balaa kwa Nchi yeyote ile.” Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba viongozi wenye mamlaka makubwa wanapaswa kila wakati kukumbuka kauli ya muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar na Muasisi wa Muungano, Sheikh Thabit Kombo, ambaye alikuwa akipenda kusema ‘weka akiba ya maneno’.
Ni wazi kwamba maneno ya Waziri Mkuu hapa Bungeni yaliuaminisha umma kuwa fedha zile siyo fedha za umma kiasi kwamba gazeti la Serikali la Daily News la tarehe 1 mwezi Mei, 2014, likachapisha habari yenye kichwa kikubwa cha habari ‘IPTL clean Deal – Pinda’. Na ofisi ya Waziri Mkuu haikukanusha.
Mheshimiwa Spika, ni jambo la kushangaza kuona kwamba, jambo kubwa na zito kama hili lingeweza kufanyika bila ya mamlaka za juu, hususan Mhe. Waziri Mkuu kufahamu. 

112
Mheshimiwa Spika, kwa uzito na unyeti wa jambo hili, kwa vyovyote vile, Waziri Mkuu anapaswa kuwajibika kwa kauli zake na kwa kutokutekeleza wajibu wake wa kikatiba ipasavyo, ili kurejesha imani ya wananchi kwa serikali yao na viongozi wao wa kisiasa.
3.0 HITIMISHO
Mhesimiwa Spika, napenda kukushukuru sana kwa kuiamini Kamati yetu kwa kuikabidhi jukumu hili nyeti. Nakuhakikishia kwamba kazi hii imetekelezwa kwa haki iliyojengwa katika msingi wa Taarifa ya Ukaguzi Maalum wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, na vyanzo vingine muhimu vikijumuisha maelezo ya Ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(TAKUKURU) na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA).
Mheshimiwa Spika, Kamati inatoa shukrani za dhati kwa vyombo vya habari kwa kuwapasha habari Watanzania kuhusiana na suala hili. Kwa namna ya pekee kabisa Kamati inalipongeza gazeti la
The Citizen kwa msimamo wake thabiti bila kujali vitisho.

113 Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inayo imani na Bunge Lako Tukufu kwamba litaitumia Taarifa hii ipasavyo katika kutekeleza Wajibu wake wa kuisimamia na kuishauri Serikali itekeleze wajibu
wake katika misingi ya haki, uadilifu, uzalendo, usawa, uwazi na uwajibikaji. Tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwani katika kipindi chote cha kuandika Taarifa hii mlitutia moyo
kwa kuonesha dhahiri kwamba mnaihitaji Taarifa yetu ijadiliwe Bungeni.
Mheshimiwa Spika, naomba pia kuishukuru Ofisi ya Spika kwa maelekezo thabiti ya namna ya kutekeleza jukumu hili.
Naomba pia kumshukuru Katibu wa Bunge, Dkt. Thomas D. Kashillilah na Wajumbe wa Sekretarieti yake kwa ushauri makini katika kipindi chote ambacho Kamati ilikuwa ikitekeleza jukumu hili. Kipekee nawashukuru pia Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ndg. Francis Mwakapalila, Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Dkt. Edward Hoseah na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini, Bw. Rished Bade kwa ushirikiano walioipatia Kamati.

114
Mwisho, nawashukuru Watumishi wote wa Bunge na vyombo vingine vya kiusalama vilivyohusika katika kuisaidia Kamati kutekeleza jukumu lake.
Mheshimiwa Spika, naomba Bunge lako tukufu lipokee Taarifa hii, lijadili na kupitisha mapendekezo yote tuliyoyatoa kuwasilisha.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
Zitto Zuberi Kabwe, Mb.
MWENYEKITI
KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI (PAC)
26 NOVEMBA, 2014

No comments:

Post a Comment