STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, February 5, 2013

BFT yafurahia mafanikio ngumi za taifa

KATIBU Mkuu wa BFT Makore Mashanga

UONGOZI wa Shirikisho la Ngumi Tanzania (BFT) limesema limefurahishwa na mafanikio iliyopatikana katika michuano ya klabu bingwa ya mchezo huo nchini yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Michuano hiyo iliyoanza rasmi Januari 27 na kumalizika Februari 2 kwenye uwanja wa Ndani wa Taifa, kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa BFT, Makore Mashaga ilifanyika kwa ufanisi mkubwa tofauti na michuano iliyopita.
Katibu huyo alisema tangu ilipoanza mpaka ilipomalizika michuano yao ilifana na kushuhudia vipaji vipya toka klabu zilizoshiriki ambao alidai baadhi yao huenda wakaongezwa kwenye timu ya taifa ya mchezo huo.
"Tunashukuru michuano ya mwaka huu imekuwa na ufanisi mkubwa kukiwa hakuna malalamiko ya aina yoyote kama miaka miliyopita, huku vipaji vipya katika ngumi vikiibuka na kutuma matumaini," alisema Mashaga.
Mashaga alisema katika michuano hiyo kulikuwa na jopo la wajumbe wa kamati ya utendaji ambao ilikuwa ikifuatilia wachezaji kwa ajili ya kuteua wachezaji wa kujiunga timu ya taifa kwa michuano ijayo ya kimataifa.
Katika hatua nyingine, Mashaga alisema kozi ya ukocha wa awali ya ngumi imeanza jana chini ya mkufunzi mkuu, Meja Mstaafu Michael Changarawe.
Zaidi ya washiriki 20 wanatarajia kuchukua mafunzo hayo ya ngumi ya muda wa wiki moja ambapo wahitimu watatunukiwa vyeti sambamba na kutambuliwa rasmi na kupata kibali cha kufundisha kokote ngumi nchini.

Mwisho

Salum Telela akata tamaa Yanga, kisa...!

Salum Telela

KIUNGO mkabaji wa klabu ya Yanga, Salum Telela ametangaza kuachana na soka kwa kile alichodai kukatishwa tamaa na hali ya majeruhi ya muda mrefu.
Nahodha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya vijana U23, aliiambia MICHARAZO kuwa, ameona bora afanye shughuli nyingine ikiwamo kurejea shuleni kutokana na ndoto zake katika soka kukatishwa na majeraha yasiyopona.
Telela alisema jeraha lake la kifundo cha mguu kimekatisha ndoto zake kwa vile limeshindwa kupona licha ya juhudi kubwa zilizofanyika kujitibia na kuona ni bora sasa afanye mambo mengine na kusahau soka.
"Ndugu yangu nimeamua kuachana na soka kabisa kwa sasa kutokana na kuona hali ya majeraha kuniandama na kuchukua muda refu kupona," alisema.
Mchezaji huyo aliyewahi pia kung'ara Moro United na aliyetua Yanga ikiwa chini ya kocha Kostadin Papic na kuaminiwa katika kikosi cha timu hiyo alisema haoni sababu ya kuendelea na soka kama hapati nafasi ya kucheza.
"Kwa kweli nimekataa tamaa na soka, nilikuwa na ndoto nyingi katika mchezo huu lakini majeraha yamenifanya nichukue maamuzi haya magumu," alisema.
Kabla ya kuibukia Yanga na Moro United, Telela alilelewa kisoka na Shule ya Sekondari ya Makongo na kuonyesha makali yake akiwa pamoja na Omega Seme ambao waliaminiwa na kiocha Papic na kutamba timu za taifa za vijana.
Msimu uliopita aliichezea kwa mkopo Moro United iliyokuwa imerejea ligi kuu kabla ya kushuka tena na kurejeshwa Jangwani, msimu huu ambapo hakuweza kucheza mechi yoyote tangu Ligi Kuu ilipoanza Agosti mwaka jana.

Mwisho

TIKETI STARS, CAMEROON ZAANZA KUUZWA 


TIKETI kwa ajili ya pambano la kimataifa la kirafiki kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Cameroon (Indomitable Lions) zimeanza kuuzwa leo (Februari 5) katika vituo mbalimbali jijini Dar es Salaam.

Mashabiki wa soka wanaopenda kuliona pambano hilo la kukata na shoka lililopo katika kalenda ya Shirikisho la Sioka Duniani, FIFA, wanahimizwa kuzichangamkia mapema.


Kikosi cha Stars kitakachovaana na akina Samuel Et'oo kesho
Viingilio katika pambano hilo litakalochezwa kesho Jumatano kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 jioni ni sh. 5,000 (viti vya kijani), sh. 7,000 (viti vya bluu), sh. 10,000 (viti vya rangi ya chungwa), sh. 15,000 VIP C, sh. 20,000 VIP B na sh. 30,000 VIP A.

Vituo vitakavyouzwa tiketi hizo kuanzia saa 2 asubuhi ni Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko Mtaa wa Samora/Ohio, Oilcom Ubungo, Dar Live Mbagala na kituo cha mafuta Buguruni.

Vilevile tiketi zitauzwa uwanjani siku ya mechi, na milango itafunguliwa saa 8 kamili mchana.

Wakati huo huo, kundi la kwanza na la pili la wachezaji wa Cameroon tayari limetua jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mechi dhidi ya Tanzania (Taifa Stars) itakayochezwa keshokutwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Cameroon chini ya Kocha Jean Paul Akono itafanya mazoezi kesho saa 11 jioni Uwanja wa Taifa. Nayo Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager yenyewe itafanya mazoezi Uwanja wa Taifa leo saa 11 jioni.

UCHAGUZI WA FRAT SASA KUFANYIKA FEBRUARI 14


Uchaguzi wa viongozi wa Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) uliokwama kufanyika mara mbili, sasa utafanyika Februari 14 mwaka huu mjini Morogoro.

Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa FRAT wanatakiwa kufika Morogoro siku moja kabla ya tarehe ya uchaguzi. Pia wapiga kura na wagombea wanatakiwa kulipia ada za uanachama kwa mwaka 2013 kabla ya uchaguzi.

Wagombea ni Army Sentimea na Said Nassoro (uenyekiti) wakati wanaoomba nafasi ya Makamu Mwenyekiti ni Juma Chaponda, Juma Mpuya na Tifika Kambimtoni.

Abdallah Mitole, Charles Ndagala na Hamis Kisiwa wanawania ukatibu mkuu, nafasi ya Mhazini inagombewa na Jovin Ndimbo. Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ni Kamwaga Tambwe wakati nafasi ya uwakilishi wanawake yupo Isabela Kapera.

Wagombea wa nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Emmanuel Chaula na Samson Mkotya.

MABINGWA TPBC WACHIMBWA MKWARA

Rais wa TPBC, Onesmo Ngowi

KAMISHENI  ya Ngumi za Kulipwa Nchini TPBC inewataka mabingwa wake wote wawe wametetea mikanda yao ya ubingwa ifikapo tarehe 30 Marchi kwaka huu ili kuepuka kunyanganywa.
 

Kwa kipindi kirefu mabingwa kadhaa wamekuwa wanakaa na mikanda bila kuitetea. Tunataka ieleweke kuwa muda wa kukaa na ubingwa wa TPBC ni miezi sita (6) tu na sio mwaka mmoja.

Bingwa wa kweli anatakiwa awe anafuata sheria, kanuni na taraibu za ubingwa alionao na sio kujiita bingwa wakati hufuati masharti yaliyowekwa.

Katika kipindi hiki cha mwaka 2013 tunawataka mabondia waheshimu sheria za mikataba wanayotiliana sahihi na mapromota. Tunataka ngumi ziboreshwe kakini pamoja na changamoto nyingi zilizoko, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa wadhamini, mabondia wakiheshimu mikataba yao mchezo wa ngumi utakua na kuwavutia wadhamini.

Tunapenda pia kuwaomba wenye mapenzi mema na nchi hii wajitolekeze kwa wingi ili kushirikiana na sisi tuiweke Tanzania kwenye chati ya dunia kama zilivyo nchi nyingine.

Imetolewa na:

ONESMO NGOWI

RAIS WA TPBC

 

MASKINI MICHAEL WAMBURA ATUPWA TENA UCHAGUZI TFF

TAARIFA KWA UMMA

 UCHAGUZI WA VIONGOZI WA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

NA TANZANIA PREMIER LEAGUE BOARD (TPL BOARD)

04/02/2013
Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inawataarifu wananchi wote kwamba baada ya kufanya usaili kwa waombaji uongozi wa TFF  na Tanzania Premier League Board (TPL Board), Kamati imefanya maamuzi yafuatayo:

1.       TANZANIA PREMIER LEAGUE BOARD

(a)                 Waombaji uongozi wafuatao wamekidhi matakwa ya Kanuni za uendeshaji za TPL Board na Kanuni za Uchaguzi za TFF. Kamati inawatangaza kuwa wagombea wa nafasi walizoomba kama ilivyoonyeshwa hapa chini:
NAFASI INAYOGOMBEWA
S/N0.
JINA
MWENYEKITI WA TPL BOARD
1.
Hamad Yahya Juma
2.
Yusufali Manji
MAKAMU MWENYEKITI WA TPL BOARD
1.
Said Muhammad Said Abeid (Kupitishwa kwake kutategemea matokeo ya uhakiki wa vyeti vyake)
MJUMBE –KAMATI YA UENDESHAJI (Management  Committee)
1.
Kazimoto Miraji Muzo
2.
Omary Khatibu Mwindadi
(b)                Mwombaji uongozi Ndg. Christopher Peter Lunkombe hakukidhi matakwa ya Kanuni za uendeshaji za TPL Board  Ibara ya 28(2)  kwa kuwa cheti chake cha Elimu ya Sekondari kina utata. Kamati ya Uchaguzi ya TFF imemwondoa kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya uendeshaji (Management Committee) ya TPL Board.

2.       SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

(a)     Waombaji uongozi wafuatao wamekidhi matakwa ya Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za TFF. Kamati inawatangaza kuwa wagombea wa nafasi walizoomba kama ilivyoonyeshwa hapa chini:
NAFASI
S/No.
JINA
RAIS WA TFF
1.
Athumani Jumanne Nyamlani
2.
Jamal Emily Malinzi
MAKAMU WA RAIS WA TFF
2.
Ramadhan Omar Nassib           
3.
Wallace Karia
MJUMBE WA KAMATI YA
UTENDAJI –
Kanda ya 1 (Kagera, Geita)
           
1.
Kalilo Samson
2.
Salum Hamis Umande Chama
Kanda ya 2 (Mwanza, Mara)
1.
Jumbe Oddessa Magati
2.
Mugisha Galibona
3.
Samwel Nyalla
4.
Vedastus F.K Lufano
Kanda ya 3 (Shinyanga, Simiyu)
1.
Epaphra Swai
Kanda ya 4 (Arusha, Manyara)
1.
Elley Simon Mbise
2.
Omar Walii Ali  
Kanda ya 5 (Tabora, Kigoma)
1.
Ahmed Idd Mgoyi
2.
Yusuf Hamis Kitumbo
Kanda ya 6 (Rukwa, Katavi)
1.
Blassy Mghube Kiondo
2.
Seleman Bandiho Kameya (Kupitishwa kwake kutategemea matokeo ya uhakiki wa vyeti vyake)
Kanda ya 7 (Iringa, Mbeya)
1.
David Samson Lugenge
2.
John Exavery M. Kiteve
3.
Lusekelo E. Mwanjala
Kanda ya 8 (Ruvuma, Njombe)
1.
James Patrick Mhagama
2.
Stanley W. D Lugenge
Kanda ya 9 (Mtwara, Lindi)
1.
Athuman Kingome Kambi
2.
Francis Kumba Ndulane
3.
Zafarani Mzee Damoder
Kanda ya 10 (Dodoma,  Singida)
1.
Hussein Zuberi Mwamba
2.
Stewart Ernest Masima
Kanda ya 11 (Morogoro, Pwani)
1.
Riziki Juma Majala
2.
Twahil Twaha Njoki
Kanda ya 12 (Kilimanjaro, Tanga)
1.
Davis Elisa Mosha
2.
Khalid Abdallah Mohamed
3.
Kusianga Mohamed Kiata
Kanda ya 13 (Dar es salaam)
1.
Alex Crispine Kamuzelya
2.
Juma Abbas Pinto
3.
Muhsin Said Balhabou   
(b)    Waombaji uongozi wafuatao hawakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za TFF. Kamati ya Uchaguzi ya TFF imewaondoa kugombea nafasi walizoomba kama ilivyoonyeshwa hapa chini:

(i)                   Ndg. Omary Mussa Nkwarulo anayeonba kugombea nafasi ya Rais wa TFF hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya 9(7) kwa kutokuwa na ufahamu wa kuridhisha kuhusu majukumu na wajibu wa nafasi anayoomba na uwezo wa kutekeleza majukumu na malengo ya TFF.

(ii)                 Ndg. Michael Richard Wambura anayeonba kugombea nafasi ya Makamu wa Rais wa TFF hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kuwa Ndg. Michael Wambura alifungua kesi ya madai namba 100 ya 2010 kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es salaam dhidi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba akiwa ni mwanachama wa Klabu ya Simba, kinyume na Katiba ya Klabu ya Simba. Kwa kufanya hivyo, Ndg. Michael Wambura alivunja Katiba ya  Klabu ya Simba, alikiuka Katiba ya TFF na Katiba ya FIFA.

(iii)                Pia Kamati inaheshimu maamuzi yaliyotolewa na Kamati ya Rufaa ya TFF kuhusu uchaguzi mwaka 2008 kwamba Bw. Michael R. Wambura hakukidhi matakwa ya Ibara ya 29(7) ya Katiba ya TFF na Ibara ya 9 ya Kanuni za Uchaguzi za TFF. Kwa mujibu wa  Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi za TFF, Kamati  ya Uchaguzi ya TFF haina mamlaka ya kubadilisha maamuzi yaliyofikiwa na Kamati hiyo ya Rufaa. Maamuzi hayo yanaweza tu kubadilishwa na Mahakama ya usuluhishi wa masuala ya michezo (CAS).  

(iv)               Ndg. Abdallah Hussein Musa anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 1 (Kagera, Geita) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kutokuwa na ufahamu wa kuridhisha kuhusu majukumu na wajibu wa nafasi anayoomba na uwezo wa kutekeleza majukumu na malengo ya TFF.

(v)                 Ndg.  Mbasha Matutu anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 3 (Shinyanga, Simiyu)  hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kuwa aliingilia mchakato wa Uchaguzi kwa kushirikiana na waweka pingamizi dhidi ya mgombea mwenzake.

(vi)               Ndg. Charles Mugondo anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 4 (Arusha, Manyara) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF  kwa kuwa vyeti vyake vya Elimu ya Sekondari na cheti cha Ualimu vina utata.

(vii)              Ndg. Ayubu Nyaulingo anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na.  6 (Rukwa, Katavi) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 3  inayotaka awe na uzoefu wa uendeshaji wa Mpira wa Miguu uliothibitishwa wa angalau miaka mitano (5) na pia  hakukidhi Ibara ya 9(7) kwa kutokuwa na ufahamu wa kuridhisha kuhusu majukumu na wajibu wa nafasi anayoomba na uwezo wa kutekeleza majukumu na malengo ya TFF.

(viii)            Ndg. Nazarius A.M Kilungeja anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na.  6 (Rukwa, Katavi) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kuwa amekuwa sehemu ya migogoro ya muda mrefu mkoani Rukwa.

(ix)               Ndg. Eliud Peter Mvella anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na.  7 (Iringa, Mbeya) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kuwa si mwaminifu kwa kukiuka uamuzi wa pamoja wa Kamati ya Utendaji ya TFF  kuhusu mabadiliko ya Katiba.

(x)                 Ndg. Farid Nahdi anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 11 (Morogoro, Pwani) hakukidhi matakwa ya Katiba ya TFF na  Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(2) na (7) kwa kuwa maelezo ya umri wake na  vyeti vya elimu havikubaliani.

(xi)               Ndg. Hassan Othuman Hassan anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 11 (Morogoro, Pwani) hakukidhi matakwa ya Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 11(5) kwa kuwa  hakuhudhuria usaili.

(xii)              Ndg. Omary Isack Abdulkadir anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 13 (Dar es salaam) hakukidhi matakwa ya Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kuwa  alikaidi maagizo ya TFF ya kuahirisha uchaguzi wa chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania  (FRAT) na maagizo ya TFF kwa kuwa alienguliwa kwenye mchakato wa uchaguzi wa FRAT kwa kutotimiza matakwa ya Kanuni za uchaguzi za wanachama wa TFF.

(xiii)            Ndg. Shafii Kajuna Dauda anayeomba kugombea nafasi ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Kupitia Kanda Na. 13 (Dar es salaam) hakukidhi matakwa ya Kanuni za Uchaguzi za TFF ibara ya 9(7) kwa kuwa si mkweli: aliposhindwa kwenye uchaguzi wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es salaam (DRFA) alipotosha umma kuhusu ushiriki wake kwenye uchaguzi huo na mchakato mzima wa uchaguzi. Pia hana ufahamu kuhusu Katiba ya TFF na majukumu ya Kamati ya Utendaji ya TFF. 

3.       Usaili uliofanyika kwa waombaji uongozi ulizingatia pia taarifa zilizoifikia Kamati ya Uchaguzi ya TFF kupitia pingamizi zilizowasilishwa dhidi ya waombaji uongozi wa TFF na TPL Board.

4.       Uchaguzi wa TPL Board utafanyika tarehe 22 Februari 2013, na Uchaguzi wa TFF utafanyika tarehe 24 Februari 2013 jijini Dar es salaam.

Deogratias Lyatto
MWENYEKITI
KAMATI YA UCHAGUZI TFF

Friday, February 1, 2013

KUZIONA TAIFA STARS, CAMEROON BUKU TANO TU!


Kikosi cha Taifa Stars kinachotarajiwa kuivaa Cameroon Jumatano ijayo


KIINGILIO cha chini kwenye mechi ya FIFA Date kati ya Taifa Stars na Cameroon itakayochezwa Jumatano (Februari 6 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kitakuwa ni sh. 5,000 kwa viti vya kijani.
Viti vya bluu ni sh. 7,000 wakati viti vya rangi ya chungwa itakuwa sh. 10,000. Kwa viti vya VIP viingilio ni kama ifuatavyo; VIP C sh. 15,000, VIP B sh. 20,000 na VIP A sh. 30,000.
Tiketi zitaanza kuuzwa siku moja kabla ya mchezo katika vituo vya Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko Mtaa wa Ohia/Samora, kituo cha mafuta OilCom Ubungo, Dar Live Mbagala na kituo cha mafuta Buguruni.

FECAFOOT YATAJA NYOTA WAKE 21, ETO’O NDANI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Cameroon (FECAFOOT) limetaja msafara wake wa watu 36 wakiwemo wachezaji 21 wa timu yao ya Taifa Indomitable Lions) wakiongozwa na nahodha Samuel Et’oo Fils kwa ajili ya mechi dhidi ya Taifa Stars itakayochezwa Jumatano.
Kiongozi wa msafara wa timu hiyo itakayoanza kuingia nchini keshokutwa (Februari 3 mwaka huu) ni Mwakilishi wa Serikali ya Cameroon, Dieudone Wassi. Naibu kiongozi wa msafara wa Cameroon itakayofikia hoteli ya New Africa ni Makamu wa Rais wa FECAFOOT, John Ndeh.
Mbali ya Et’oo, wachezaji wengine waliomo kwenye msafara huo ni Charles Itandje, Benoit Assou Ekoto, Jehu Rustand Youthe (Union Douala), Fabrice Olinga Essono, Allam Nyam, Bouba Aminou, Benoit Angwa, Herve Tchami, Henri Bedimo, Nicolas Nkoulou, Jean Makoun, Jean Kana Biyick, Joel Matip, Vincent Aboubakar, Alexandre Song, landre Nguemo, Pierre Wome, Jean Nyontcha, Achille Emana na Charles Eloundou.
Wengine ni Andre Nguidljol Nlend (Mkurugenzi wa Utawala FECAFOOT), Jean Paul Akono (Kocha Mkuu), Martin Ndtouungou Mpile (Kocha Msaidizi), Jacque Songo’O (Kocha wa makipa), Dk. Baoubakary Sidiki (Daktari wa Timu) na Emmanuel Francis Ambane (Psychologist).
Pia wapo Tchonkontey Monkam (Fitness Trainer), Rigobert Song (Meneja wa Timu), Aoudou Mvotoung (Team Security), Fouda pascal Linus (Ofisa Habari FECAFOOT), Boubakar Ndou (Meneja Vifaa), Daniel Tcheuffa Tecky (Physiotherapist), Elias Kalaguem (Physiotherapist) na Justin Addo (Wakala wa Mechi).
Wakati huo huo, kikosi cha Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager kitaingia kambini kesho jioni (Februari 2 mwaka huu) kwenye hoteli ya Tansoma.

YANGA, MTIBWA SUGAR KAZI KWELIKWELI

Yanga na Mtibwa Sugar zinapambana kesho (Februari 2 mwaka huu) katika moja ya mechi za Ligi Kuu ya Vodacom. Mchezo huo utafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mwamuzi Ronald Swai kutoka Arusha ndiye atakayechezesha mechi hiyo inayotarajiwa kuwa na upinzani mkali, kwani wakati Yanga ikiongoza ligi hiyo, wapinzani wao Mtibwa Sugar katika mechi iliyopita walilala mbele ya Polisi Morogoro ambayo ni ya mwisho katika msimamo wa ligi kwa sasa.
Polisi Morogoro itakuwa mwenyeji wa African Lyon kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro wakati Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Mgambo Shooting na Ruvu Shooting inayofundishwa na Charles Boniface Mkwasa.
Keshokutwa (Jumapili) kutakuwa na mechi mbili. Simba itaumana na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku Tanzania Prisons ikiikabili Coastal Union katika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

VILLA SQUAD, MORO UNITED UWANJANI FDL

Villa Squad na Moro United zinaumana kesho (Februari 2 mwaka huu) Uwanja wa Karume, Dar es Salaam katika moja ya mechi za kundi B za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inayoanza mzunguko wa lala salama.
Kundi A litakuwa na mechi kati ya Mbeya City na Burkina Faso itakayochezwa Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, Majimaji na Kurugenzi katika Uwanja wa Majimaji mjini Songea, na Polisi Iringa dhidi ya Mkamba Rangers kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa.
Mechi nyingine ya Kundi B itakuwa Transit Camp na Ndanda itakayochezwa Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani. Kundi C ni Polisi Dodoma na Kanembwa JKT (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma), Morani dhidi ya Mwadui (Uwanja wa Kiteto, Manyara), Polisi Mara na Pamba (Uwanja wa Karume, Musoma), Polisi Tabora na Rhino Rangers (Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora).
Ligi hiyo inatarajiwa kumalizika mwishoni mwa Machi mwaka huu ambapo mshindi wa kila kundi atapanda daraja kucheza Ligi Kuu msimu ujao.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

AJALI MBAYA: WATANO WAFA 20 WAJERUHIWA MBEYA LEO

ASKARI WA USALAMA WA BARABARANI WAKIWA WAMEFIKISHA MAJERUHI PAMOJA NA WATU WALIO FARIKI HOSPITALINI HAPO
 RIPOTI IKIWA INATOLEWA JUU YA AJALI HIYO HUSSEIN KIF
MMOJA YA ABIRIA WALIOKUWEMO KATIKA AJALI HIYO

AJALI MBAYA IMETOKEA MAPEMA LEO MBALALI AMBAPO LORI LA MIZIGO AINA YA SCANIA ILIKUWA IMEBEBA WATU ZAIDI YA MIAMBILI (200) AMBAO WALIKUWA WANAELEKEA KATIKA KITONGOJI KIMOJA CHA MWEKEZAJI .

AJALI HIYO IMETOKEA BAADA YA LORI HILO LENYE NAMBA ZA USAJILI T 398 BSE KUANGUKA NA KUSABABISHA WATU 5 KUFARIKI DUNIA NA WENGINE 20 KUJERUHIWA VIBAYA.

HATA HIVYO MAJERUHI WOTE WANAKIMBIZWA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA ILIYOPO MBEYA MJINI MUDA HUU.

HIZI NI TAARIFA ZA AWALI TUU, HABARI NA PICHA ZOTE ZINAKUJA HAPA HAPA 

PICHA KWA HISANI YA MBEYA YETU BLOG