STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, April 17, 2014

Yanga yaiwinda Simba Kawe Beach, Mnyama aenda Zenji

Yanga
Simba
KLABU ya Yanga ambayo ilirejea jijini Dar es Salaam jana ikitokea Moshi ilikocheza mechi ya kirafiki dhidi ya Panone FC wakati ikiwa njiani kutokea Arusha, imeweka kambi yake Kawe Beach na imeelezwa kwamba huenda wakahamia Bagamoyo mkoani Pwani kwa ajili ya mechi yao ya kukamilisha ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya mahasimu wao Simba.
Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema jana kwamba aulizwe kuhusu kambi ya timu hiyo akishafika Dar es Salaam akitokea Moshi, lakini mara baada ya kutua walikwenda moja kwa moja Kawe Beach na habari kutoka ndani zilisema kwamba kambi hiyo inaweza ikahamia Bagamoyo.
Hata hivyo, mshambuliaji wa kimataifa kutoka Uganda, Emmanuel Okwi, yuko katika hatihati ya kujiunga na kambi hiyo kutokana na kuhitaji alipwe fedha zake za usajili anazoidai klabu hiyo.
Okwi aliyejiunga na Yanga Desemba mwaka jana anaidai klabu hiyo dola za Marekani 50,000 na imeelezwa kwamba juzi alikataa kupokea kiasi cha dola za Marekani 20,000 ambazo ilikuwa atanguliziwe.
Chanzo cha gazeti hili kilieleza kuwa Okwi aliambiwa apokee dola 20,000 ili arejee kundini kujiandaa na mechi dhidi ya Simba Jumamosi lakini Mganda huyo alikataa.
Habari zaidi kutoka Yanga zilieleza kuwa aliyekuwa mwenyekiti wa klabu hiyo, Francis Kifukwe, alimtaka Okwi akubali kiasi hicho na kuahidiwa kumaliziwa fedha nyingine zilizobakia mara baada ya viongozi wengine wa juu wa Yanga watakaporejea nchini.
Rafiki wa karibu wa Okwi aliliambia gazeti hili kwamba mshambuliaji huyo amegoma kupokea malipo hayo kwa mafungu ili kujiepusha na suala na kuja kusotea kiasi kilichobakia.
"Mechi hiyo ya Simba Jumamosi ndiyo ya mwisho, anajua asipolipwa sasa itakula kwake", alisema rafiki huyo ambaye alikuwa naye tangu alipokuwa anaichezea Simba.
Okwi hapatikani katika simu zake za mkononi na inaelezwa pia hata mahali anapolala amekuwa anabadilisha kulingana na atakavyojisikia siku hiyo.
Yanga tayari imeshavuliwa ubingwa na Azam FC na inachotaka katika mechi hiyo ya funga dimba ni kulinda heshima kwa wanachama na wapenzi wa timu hiyo.
Kwa kumaliza katika nafasi ya pili, Yanga itaiwakilisha nchi mashindano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho mapema mwakani.
Kocha wa timu hiyo, Mholanzi Hans van der Pluijm, alisema kuwa atawatumia wachezaji waliofanya mazoezi tu kwa ajili ya mechi hiyo ya Jumamosi.
Alisema kuwa hataki kuzungumzia mchezaji asiyekuwa pamoja na timu kwa sababu za kiutawala.
Wakati Yanga ikijichimbia Dar, wapinzani wao wamekimbilia Zanizbra kwa ajili ya kusaka ubani wa kuiua wana Jangwani siku ya Jumamosi Taifa.
Mwenyekiti wa Kamati ya usajili wa klabu hiyo, Zakaria Hanspope ndiye aliyeokoa jahazi timu kwenda kambini Zenji baada ya kudaiwa kuwapo kwa mgomo baridi kwa wachezaji kudai posho na mishahara waliyokuwa wanadai.
NIPASHE. 

'Mzee Gurumo kama alikiona kifo mapema hospitalini

Masheikh wakiendelea na kisomo cha kumuombea Mzee Gurumo katika safari yake ya Ahera

Mwili wa Mzee Gurumo ukitolewa kwenye nyumba yake ya Mabibo tayari kwa safari ya kwenda kuzikwa Masaki

Mzee Jangala na JB wakiteta kwenye msiba wa Mzee Gurumo, Mabibo

Juma Ubao akimuelezea Mzee Gurumo kwa waandishi wa Habari

Umma uliojitokeza Masaki

Kaburi alilozikiwa Mzee Gurumo

Shamsa Ford alikuwapo kumsindikiza Mzee Gurumo

Said Mabela kizungumza na wanahabari

Jeneza la mwili wa Mzee Gurumo likiswaliwa Mabibo
Mwili waq Gurumo ulitoka kuswaliwa msikiti wa kijijini kwao Masaki

HUWEZI kujua ni kitu gani kilimjia, lakini ukweli ni kwamba saa chache kabla ya kufariki, gwiji wa muziki wa dansi nchini, Muhidini Gurumo aliyefia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), alikiona kifo chake na kujaribu 'kukikwepa'.
Inaelezwa Gurumo asubuhi ya Jumapili, alitoroka hospitalini hapo kabla ya kushtukiwa na kurudishwa wodini huku akiieleza familia yake amechoka kukaa hapo na kutaka aende nyumbani.
Kwa mujibu wa mmoja wa wanafamilia, Gurumo alitaka akakae nyumbani japo siku mbili kisha arejee hospitalini kuendelea na matibabu.
"Huwezi kuamini alitoroka wodini na kukamatiwa getini, tulimweleza haoni aibu kama wanahabari wakijua alitaka kutoroka bila ruksa ya daktari, lakini alidai asingejali kwa vile amechoka kukaa hospitalini hapo," alisema mwanafamilia huyo anayedai ameoa nyumba moja na Gurumo.
Aliongeza walimbembeleza na kumuahidi kumuombea ruksa kwa daktari wake ili aende nyumbani kwa siku nne badala ya mbili alizotaka na kutulia.
"Niliachana naye saa 7:30 mchana akiridhika akijua mpango huo utafanyika Jumatatu, ila nilipofika Mbagala nilipigiwa simu amefariki, nahisi huenda alikiona kifo mapema ndiyo maana alitaka kuondoka hospitalini."
Naye mdogo wa marehemu, Yahya Mikole alisema mara kadhaa Gurumo alimsisitizia akifa asizikwe haraka ili kutoa nafasi watu kuhudhuria mazishi yake.
"Alidai asizikwe haraka kama Tx Moshi William, ndiyo maana tumezingatia wosia wake na kumzika Jumanne badala ya Jumatatu," alisema Mikole.

ELIMU
Siyo katika muziki tu, Gurumo japo hakubahatika kusoma sana elimu ya kawaida zaidi ya ile ya dini ya Kiislam, lakini alikuwa mdau mkubwa wa sekta ya elimu.
Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Fatma Lusindilo alifichua kwenye msiba wa Mzee Gurumo kijijini kwake Masaki wakati akitoa ubani wao wa Sh.400,000 kwa familia ya marehemu, akidai enzi za uhai wake Gurumo alijali na kuthamini elimu kwa kuchangia kila mara Mfuko wa Elimu wa wilaya hiyo.
"Kwa mchango wake kwa jamii, tunatoa mkono wa pole kwa familia kiasi cha Sh.400,000, tunawaomba muwe na subira katika kipindi hiki kigumu," alisema DC Fatma.

CHOKI
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki, mmoja wa waombolezaji waliojitolea kwa hali na mali katika msiba wa Gurumo kama ilivyokuwa kwa Ruge Mutahaba na Lady Jaydee waliotoa usafiri kusafirisha waombolezaji, alisema itamchukua muda mrefu kusahau msiba wa Gurumo.
Choki alisema yeye ni kati ya wanamuziki wachache na wa pekee kwa kizazi kipya kuimba na Gurumo akirejea albamu yao akiimba vyema wimbo wa Kassim wa Kutumia.
"Ni pigo kwa wadau wa muziki na familia nzima ya gwiji huyo, lakini kwangu ni pigo zaidi kwa vile ndiye pekee wa kizazi cha sasa niliyeimba naye kazi binafsi, ila nadhani ni mipango ya Mungu nami kubakiwa na kumbukumbu yake," alisema Choki ambaye aliurudia wimbo wa Gurumo wa 'Kassim', ambao Choki aliimba sauti ya gwiji huyo.

SIFA
Waombolezaji wakiwamo viongozi na wanamuziki wenzake walimmiminia sifa Gurumo wakidai alikuwa mfano Tanzania, kiasi cha Rais wa Shirikisho la Muziki Tanzania, Ado Novemba alidiriki kumtaja kama 'Nyerere wa Muziki'.
Said Mabela aliyechukuliwa na Gurumo kutoka Kurugenzi Jazz ya Arusha mwaka 1973, alisema hana cha kusema zaidi ya kumuombea safari njema na atamkumbuka kwa mengi hasa katika kupeleka mbele muziki wa Tanzania.
Shaaban Dede, Juma Ubao, Kassim Mapili, Jamhuri Kihwelu, Shem Ibrahim Kalenga, Mafumu Bilal 'Bombega' na wengine walisema Gurumo ameacha pengo katika fani ya muziki na michezo kwani enzi za uhai wake alikuwa shabiki wa Simba ya Dar es Salaam na Manchester United ya Uingereza bila kificho.
Waliohudhuria msiba wa Gurumo mbali na Makamu wa Rais, Dk Gharib Bilal ni DC wa Kinondoni, Jordan Rugimbana, Mbunge wa Ilala, Mussa Azzan, Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete, Makamu wa Rais wa zamani wa TFF, Nassib Ramadhan, MB Doggy, Dully Sykes, Omar Tamba, Idd Seleman, Chiki Mchoma na wengine.

MAZISHI
Gurumo muasisi wa miondoko na bendi za Msondo Ngoma, Sikinde na Ndekule' aliyezipigia pia Kilimanjaro Chacha, Kilwa Jazz na Orchestra Safari Sound (OSS), alifariki saa 9 ya Jumapili na kuzikwa saa 7:53 ya Jumanne  kijijini kwao.
Alisumbuliwa na maradhi ya mapafu na moyo kwa miaka zaidi ya miwili na kusababisha kustaafu muziki Septemba mwaka jana.
Safari ya maziko yake ilianza saa 2 asubuhi mwili wake kutolewa Muhimbili na kuletwa nyumbani kwake saa 2:45 na kupokewa na umati wa waombolezaji kabla ya kuswaliwa saa 4:38 na saa 4:57 kusafirishwa kwenda Kisarawe.
Msafara kuelekea kijijini uliongozwa na gari la kubebea wagonjwa la Hospitali ya Mwananyamala na kuwasili saa 7:09 kisha kuswaliwa tena msikiti wa kijiji hicho na kuzikwa saa 7:53 kuhitimisha safari yake ya miaka 74 duniani.
Marehemu Gurumo aliyezaliwa 1940 ameacha mjane Pili bint Said na watoto sita na enzi za uhai wake alitamba na nyimbo mbalimbali ukiwamo wa 'Kassim Na.1' na Na.2.