STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, May 24, 2013

Baada ya kung'ara Gor Mahia, Ivo Mapunda awindwa na Tusker

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgcOsm-7zdR8dd1_VaKXsG_pBGttOec_6nguW8rxdX0f25fGFel_h1i8t__5lKCqSGd3tP8YSGwX1MS8JUGnUEQ-6eDQgXlYYQaO-VxDlPnOlnnAqByjy6zuTcYxXENkjTNjtlTc7tBatOJ/s400/IVO-MAPUNDA.jpg
Ivo Mapunda
KIPA nyota wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Ivo Mapunda anayeidakia Gor Mahia ya Kenya, amesema yupo katika harakati ya kuhamia kwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Kenya, Tusker.
Hata hivyo kipa huyo aliyewahi kuichezea Bandari-Kenya kabla ya kutua Gor Mahia, alisema anasubiri kwanza kumalizika kwa mkataba wake mwishoni mwa mwaka huu kuamua hatma yake.
Alisema kocha wa Tusker, Robert Matano alimpigia simu mara baada ya kung'ara katika pambano la marudiano la Nusu Fainali ya 8 Bora ili kujua mkataba wake ukoje kabla ya kumvuta Tusker.
Mapunda aliyechaguliwa Mchezaji Bora wa pambano hilo lililoisha kwa suluhu ya kutofungana, lakini Tusker ikisonga mbele kwa ushindi wa bao 1-0 iliyopata katika mechi ya awali, alisema iwapo Tusker itamvutia kimasilahi atahamia kwa mabingwa hao wa ligi.
"Nitaangalia masilahi kwanza kama jamaa nibaki Gor Mahia au kujiunga na Tusker, ila nasubiri kwamba mkataba wangu na klabu yangu ya sasa uishe Desemba mwaka huu," alisema Mapunda.
Kuhusu mafanikio anayoyapata akiwa Kenya, kipa huyo aliyewahi kuidakia Prisons Mbeya na St George ya Ethiopia alisema yanamfariji mno baada ya kupuuzwa nyumbani akionekana kaisha.
"Nafurahia mno kupata mafanikio ugenini na kuthaminika naamini Mungu ataendelea kunisaidia zaidi na kutamba," alisema.
Mapunda ambaye amekuwa chaguo la kwanza katika kikosi cha Gor Mahia anatarajiwa kuiongoza timu yake Jumapili ikiwa ugenini katika mji wa Mumias dhidi ya Western Stima katika mechi ya Ligi.

No comments:

Post a Comment