STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, May 24, 2013

Yanga kujipima kwa Rayon kabla ya kwenda Darfur kutetea Kagame


Kikosi cha Yanga
MABINGWA watetezi wa mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), Yanga wanatarajia kucheza mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Rwanda, Rayon kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza mwezi ujao.
Akizungumza jana, Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako, alisema kuwa wamepokea barua ya mwaliko huo kutoka kwa mratibu wa mechi hiyo lakini bado hawajathibitisha hadi kocha Mholanzi Ernie Brandts atakapotoa maelekezo.
Mwalusako alisema kwamba mechi hiyo wakiipata itakuwa ni nzuri kwa kuwaandaa wachezaji kuelekea Sudan na vile vile ni nafasi kwa Yanga kuwapa heshima mashabiki wake wa kanda ya ziwa kuiona timu baada ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara.
"Ni kweli taarifa za mechi hiyo tunayo, lakini majibu rasmi hatutawapa na siku ya mchezo pia haijapangwa ila wamependekeza iwe mapema mwezi ujao," alisema Mwalusako.
Naye mmoja wa viongozi wa Rayon, Clever Kazungu, alithibitisha timu yake kupokea mwaliko huo na kusema kwamba wako tayari kuja nchini endapo watafikia makubaliano na waandaaji wa mchezo.
Kazungu alisema tayari wameambiwa kuwa watalipiwa gharama ya malazi, chakula na posho ya wachezaji kwa siku watakazokuwa hapa nchini.
Yanga itaanza kampeni za kutetea ubingwa wa Kombe la Kagame kwa kuivaa Express ya Uganda katika mechi ya kundi C itakayofanyika Juni 20 kwenye Uwanja wa Elfasher saa nane mchana wakati Simba iliyopangwa kundi A itashuka dimbani siku inayofuata kuivaa El Mereikh.
Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Bara watashuka tena dimbani Juni 22 mwaka huu kuikabili Ports na watakamilisha mechi za hatua ya makundi Juni 25 kwa kuvaana na Vital'O.
Simba watashuka tena kusaka ubingwa wa michuano hiyo Juni 23 kwa kupambana na APR na watamaliza dhidi ya Elman Juni 26.
Yanga pia huenda ikawavaa mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Zanzibar, KMKM, katika mechi nyingine ya kirafiki inayotarajiwa kufanyika hivi karibuni.

No comments:

Post a Comment