STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 13, 2013

ROCK CITY MARATHON 2013 KUZINDULIWA SEPT 19

 Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi, akikata utepe kuzindua Mbio za Rock City Marathon 2012, katika hafla iliyofanyika mwaka jana katika Hoteli ya New Africa jijini Dar es Salaam.
Wadhamini wa Mbio za Rock City Marathon 2012, pamoja na Mwenyekiti wa BMT, Dioniz Malinzi (wa tatu kulia), wakiwa katika picha ya pamoja katika hafla ya uzinduzi wa mbio hizo mwaka jana uliofanyika katika Hoteli ya New Africa Dar. 

DAR ES SALAAM, Tanzania

UZINDUZI wa msimu wa tano wa mbio za Rock City Marathon 2013 zilizoanza mwaka 2009, zikiwa na lengo la kukuza Utalii wa Ndani kupitia michezo, unatarajia kufanyika Septemba 19, kwenye Hoteli ya New Afrika, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mratibu wa mbio hizo, Mathew Kasonta, alisema kuwa pamoja na mambo mengine, mbio za mwaka huu za Rock City Marathon, zitakuwa kubwa na bora zaidi kulinganisha na miaka minne iliyotangulia.

“Tuko tayari kwa mbio za Rock City Marathon 2013, zitakzofanyika Oktoba 27. Kamati ya Maandalizi imeweka mikakati mizuri ili kuhakikisha mbio za mwaka huu zinakuwa bora na zenye mafanikio kulinganisha na misimu iliyopita,” alisema Kasonta.

Rock City Marathon zinaandaliwa na Kampuni ya Capital Plus International (CPI), kwa ushirikiano na Chama cha Riadha Tanzania (RT), pamoja na Chama cha Riadha mkoa wa Mwanza (MRAA), ambazo zimewavutia washiriki wengi wa ndani na nje ya nchi.

Kasonta aliongeza kwamba, mbio hizo zitakuwa na vipengele vitano kwa msimu huu, ambavyo ni mbio za kilometa 21 (wanawake na wanaume) na zile za kilometa tano kwa wakimbiaji kutoka makampuni mbalimbali.

Kategori nyingine za mbio hizo ni kilometa tatu kwa watu wenye ulemavu, kilometa tatu kwa watu wazima (zaidi ya miaka 55) na kilometa mbili kwa watoto walio kati ya miaka 7 mpaka 10.

Bw. Kasonta alisema kutokana na uzoefu wa mwaka jana kwa wanariadha wengi kujitokeza kushiriki, kamati ya maandalizi imeongeza idadi ya waongozaji watakaosaidia katika kuzifanikisha mbio hizo.

“Tunatarajia watu wengi kujitokeza mwaka huu, kwa kuwa tuna vitu vizuri kwa msimu huu. Tumejifunza kupitia mbio za mwaka jana, hivyo Kamati ya Maandalizi imekuja na mpango madhubuti utakaoboresha mbio zetu kwa mwaka huu,” alisema Kasonta.

No comments:

Post a Comment