STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, November 9, 2014

Kiatu cha Dhahabu chawatenganisha Mastrika Mtibwa Sugar

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjQad4Oq4g-LosmXTb_u2D2W037XzTTAhnkgQm9rGOGEPQLxgg6SZMSFKvvlaRSGqLHxEa6lX-ak7P3sWS9YjYiIiQnfFQuQm-q45k9wJtIbEhOURSVLd3D8haQg0ZxRD9UJp4hXZ28gIaQ/s1600/ALLY+SHOMARI+MTIBWA+NA+ISSA+RASHID+SIMBA+PIX+NO+1.JPG
Ali Shomari (kushoto) akichuana na Baba Ubaya
Ame Ally 'Zungu' akiwajibika siku ya mechi yao na Simba
WASHAMBULIAJI wawili nyota wanayoibeba kwa sasa Mtibwa Sugar, Ally Shomari 'Shiboli' na Ame Ally 'Zungu' kila mmoja amekuwa na mtazamo wake kuhusiana na kasi yao ya kufunga mabao katika Ligi Kuu Tanzania Bara mmoja akiota Kiatu cha Dhahabu mwengine akikipotezea ila akitaka kuipa Mtibwa ubingwa wake wa tatu katika historia ya kandanda la Tanzania.
Wakali hao ambao kila mmoja amefunga mabao matatu (japo Zungu jana alifunga wakati wa pambano lao na Kagera Sugar ambalo lilitarajiwa kurudiwa leo asubuhi kumaliza dakika 45 za mwisho) waliiambia MICHARAZO kwa nyakati tofauti kwamba wanachekelea kuendelea kufunga mabao ili kuisaidia Mtibwa kutimiza ndoto iliyoweka mara ya mwisho miaka 14 iliyopita.
Ame Ally amesema yeye anafurahia kufunga mabao mengi zaidi akiwa hana ndoto ya kuja kunyakua Kiatu cha Dhahabu tofauti na Shomari alisema anakitamani mno kiatu hicho ambacho kimekuwa mikononi mwa wachezaji wa kigeni kwa misili miwili mfululizo iliyopita akianza Kipre Tchetche wa Azam kabla ya Amissi Tambwe wa Simba kumpokea msimu uliopita.
"Kila mchezaji ana malengo yake, mimi nafurahia kufunga mabao kwa sababu ya kutaka kuisaidia Mtibwa, nataka kuibebesha taji baada ya kunyakua mara ya mwisho ubingwa mwaka 2000, suala la tuzo ya Mfungaji Bora labda lije tu kwa bahati mbaya," alisema Ame aliyetua Mtibwa msimu huu akitokea Chuoni inayoshiriki Ligi Kuu ya Zanzibar.
Kwa upande wa Shomari anayeichezea Mtibwa kwa msimu wa pili sasa baada ya kunyakuliwa mwaka juzi akitokea Polisi-Moro wakati ikishuka daraja, alisema anakitamani Kiatu cha Dhahabu na amepania kuwa Mfungaji Bora sambamba na kuisaidia Mtibwa kuwa bingwa mpya wa Tanzania.
"Nakitamani mno Kiatu cha Dhahabu kwa msimu huu, nitapambana kuhakikisha nafunga mabao mengi ili kurejesha kiatu hicho mikononi mwa wazawa, ingawa natambua ushindani utakuwa mkubwa kuliko ilivyokuwa msimu uliopita, ambapo Tambwe alitwaa kiatu hicho kwa mabao 19 huku anayemfuata akiwa na mabao 13," alisema.
Nyota hao wawili ambao wanakamata nafasi ya pili kwa sasa ya wafumania nyavu nyuma ya Didier Kavumbagu wa Azam mwenye mabao manne kwa ujumla wao wameifungia Mtibwa mabao sita, huku mengine yakiwekwa kimiani na Mussa Mgosi mwenye mabao mawili na Vincent Barnabas aliye na bao moja kati ya mabao 9 ya mabingwa hao wa zamani wa Tanzania waliopo kileleni kwa sasa.

No comments:

Post a Comment