STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, January 21, 2014

Uganda yakwama CHAN, tumaini la CECAF lipo kwa Burundi sasa

 
WAWAKILISHI wa CECAFA katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN) inayoendelea Afrika Kusini, Uganda The Cranes usiku wa kuamkia leo imejikuta ikikwama kusonga mbele kwa kulala 3-1 kwa Morocco.
Uganda waliokuwa wakipewa nafasi kubwa ya kutamba kwenye kundi lake, imejikuta ikiaga mashindano hayo kutokana na Zimbabwe kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Burkina Faso na kuifanya ifungane pointi tano sawa na Morocco na kufuzu.
The Cranes wamesalia na pointi zao nne na Morocco wamemaliza kama vinara wa kundi hilo wakifuatiwa na Zimbabwe.
Katika pambano hilo la Uganda na Morocco washindi walianza kupata bao la kwanza lililozamishw na Rafik Abdessamad katika dakika ya 29 akimaliza kazi nzuri ya Abdelkabir El Ouadi, bao lililodumu hadi mapumziko.
Kipindi cha pili kilianza kwa Uganda kurejesha bao hiulo kupitia mfungaji wake nyota, Yunus Sentamu katika dakika ya 60 kabla ya Nouhssine Iajour kuiongezea Morocco bao la pili dakika ya 77 na El Ouadi kupigilia msumari wa mwisho kwa kufunga bao la tatu kwenye dakika ya 90'+3.
Katika pambano jingine lililochezwa kwa wakati mmoja sawa na pambano hilo la Uganda na Morocco, goli pekee la Zimbabwe lilitupiwa kimiani na  Masimba Mambare katika ya 56 akimalimalizia kazi ya Kudakwashe Mahachi.
Morocco na Zimbabwe zimeunga na timu za Nigeria na Mali katika hatua ya robo fainali, huku washindi wengine wakitarajiwa kupatikana leo baada ya mechi za kundi C ambapo Ethiopia iliyokwisha yaaga mashindano hayo mapema itavaana na Ghana na Jamhuri ya Kongo kupepetana na Libya.
Mpaka sasa kundi hilo linaongozwa na Libya yenye pointi nne sawa na Ghana ila zinatofautiana mabao ya kufunga na kufungwa, kisha kufuatia Kongo yenye pointi 3.
Mechi nyiungine za mwisho za makundi zitakazokamilisha idadi ya timu nane za kucheza hatua hiyo ya mtoano zitachezwa kesho kwa michezo kati ya Burundi dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Mauritania itakayoumana na Gabon.
Tumaini pekee la Ukanda wa CECAFA katika michuano hiyo imesalia mikononi mwa Burundi wanaoongoza kundi D ambapo italazimika kushinda kesho  la sivyo ukanda huo utakuwa umepata aibu kwa timu zake zote tatu kuambulia patupu katika mashindano hayo yanayofanyika kwa mara ya tatu sasa.

Monday, January 20, 2014

News Alert! Ajali yaua 13 Singida


HABARI zilizotufikia hivi punde kutoka Singida zinasema watu 13 wamefariki dunia baada ya kutokea ajali ya magari mawili kugongana uso kwa uso eneo la Isuna mkoani humo.

Habari hiuzo zinasema ajali hiyo ilihusisha gari aina ya Toyota Noah na lori ambayo namba zake za usajili hazikupatikana mara moja. Watu 13 waliofariki walikuwa katika Noah iliyokuwa ikitokea Itigi na maiti zao zimehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Singida.

Baada ya ajali hiyo, dereva wa lori na msaidizi wake walitokomea kusikojulikana, ila habari zaidi zinaendelea kufuatiliwa.


Mashetani Wekundu waning'inizwa tena, Spurs yaua

Eto'o akishanglia moja ya mabao yake matatu aliyofunga akiiangamiza Mashetani Wekundu

http://news.bbcimg.co.uk/media/images/72380000/jpg/_72380954_tottenham-adebayorafp.jpg
Emmanuel Adebayor akifunga moja ya mabao yake mawili jana wakiiua Swansea City ikiwa kwao

WASHAMBULIAJI nyota toka barani Afrika, Emmanuel Adebayor na Samuel Eto'o jana waling'ara baada ya kuziwezesha timu zao za Tottenham Hotspur na Chelsea kuibuka videdea katika Ligi Kuu ya England.
Adebayor alifunga mabao mawili wakati Spurs wakiizamisha Swansea City nyumbani kwa mabao 3-1, naye Eto'o alifunga hat-trick wakati Mashetani Wekundu wakining'izwa 'darajani' na Chelsea.
Eto'o alifunga mabao mawili kipindi cha kwanza katika dakika ya 17 na 45 na jingine dakika ya nne baada ya kuanza kwa kipindi cha pili, huku bao la kufutia machozi ya Manchester United likifungwa na mtokea benchi Javier Hernandez 'Chicharito' dakika ya 78.
Beki tegemeo wa Man Utd Nemanja Vidic alionyeshwa kadi nyekundu dakika ya 90 na kuifanya Mashetani hao kuzidi kunyong'onyea kabisa.
Katika pambano la Spurs dhidi ya wenyeji Swansea City, Emmanuel Adebayor alifunga mabao yake katika kila kipindi la kwanza kifunga  dakika ya 35 kabla ya kuongeza jingine lililokuwa la tatu katika pambano hilo kwenye dakika ya 71.

Bao jingine lililoisaidia Spurs kupata ushindi huo mnono lilifungwa na Chico aliyejifunga dakika 53, na bao la kufutia machozi la Swansea lilifungwa na Wilfried Bony dakika ya 78.

Nigeria yaiduwaza Bafana Bafana na kutinga robo fainali

* Yaungana na Mali wakiwaacha wenyeji wakishangaa
* Uganda kibaruani kwa Morocco leo
http://dailypost.com.ng/wp-content/uploads/2014/01/Nigeria-vs-South-Africa-CHAN-2014.jpg

MABINGWA wa Afrika, Nigeria jana iliwaduwaza wenyeji wa michuano ya CHAN 2014 Bafana Bafana ya Afrika Kusini baada ya kuwakandika mabao 3-1 na kuitupa nje kwenye michuano hiyo, huku wenyewe wakifuzu robo fainali kutoka kundi A.
Nigeria iliyoanza kwa kipigo cha  mabao 2-1 kutoka Mali, ilibashiriwa ingekuwa na wakati mgumu katika mechi hiyo ya jana dhidi ya wenyeji,  lakini walifanya kisichotarajiwa kwenye  uwanja wa Cape Town baada ya kupata ushindi huo uliowafanya wakamate nafasi ya pili.
Mabao mawili  ya Uzoenyi katika dakika ya 22 na jingine la 64 na lile la mkwaju wa penati kupitia kwa Ede iliivusha Nigeria hatua ya mtoano sawia na vinara wa kundi hilo la A, Mali ambayo iliichapa Msumbiji mabao 2-1 na kufikisha pointi saba.
Bao la wenyeji lilifungwa na kinara wa mabao katika michuano hiyo Bernard Parker kwa mkwaju wa penati  na kumfanya asfikishe mabao manne mpaka sasa.
Katika mchezo wa Msumbiji na Mali ambao ulichezwa muda mmoja na pambano la Nigeria na Afrika Kusini, Msumbiji waliokuwa wa kwanza kuaga michuano hiyo  walianza kupata bao dakika ya 38 kupitia kwa Josemar aklimalizia kazi ya Mario..
Hata hivyo Sidibe alisawazisha bao hilo dakika tatu tangu kuanza kwa kipindi cjha pili kabla ya
Ibraouma Traore kufunga bao la ushindi dakika za nyongeza za pambano hilo na kuivusha Mali hadi robo fainali.
Michuano hiyo0 itaendelea leo kwa michezo ya kundi B ambapo timu nyingine mbili za kutinga robo fainali zitafahamika ambapo, Uganda the Cranes wanaoongoza kwa sasa katika kundi hilo watavaana na Morocco, huku Zimbabwe watapepetana na Burkina Faso.