STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 4, 2013

SARAH RAMADHAN AWATOA KIMASOMASO WATZ KILI MARATHON

Kocha wa timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) akimaliza mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon za Kilomita 21 zilizofanyika leo mjini Moshi. (Picha: Executive Solutions)

Meneja wa Bia ya Kiliamanjaro, Geogre Kavishe akimpongeza Edina Joseph mmoja wa washiriki wa Mashindano ya Kilimanjaro Marathon, yaliofanyika leo, Moshi Mkoa wa Kilimanjaro. (Picha: Executive Solutions)

MWANARIADHA wa Kitanzania, Sarah Ramadhani, jana aliibuka shujaa katika mashindano ya mwaka huu ya mbio ndefu za Kilimanjaro Premium Lager Marathon, baada ya kuibuka mshindi katika mashindano ya kilomita 21, (nusu marathon), kwa upande wa wanawake katika mbio zilizofanyika mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro.

 Sarah alishinda mbio hizo baada ya kukimbia kwa dakika 1:13:05 na kujipatia medali ya dhahabu baada ya kuwabwaga wenzake wakiwemo Wakenya ambao wamekuwa wakitawala mbio hizo katika miaka ya hivi karibuni.

 Katika mbio hizo ambazo mwaka huu zimeweka rekodi ya kuwa na washiriki zaidi ya 6,800, Vicoty Chepkemoi, kutoka Kenya alishika nafasi ya pili baada ya kukimbia kwa dakika 1:14:34, ambapo Mtanzania mwingine Failuna Matanga, alishika nafasi ya tatu kwa kukimbia kwa dakika 1:15:35.

Hata hivyo wakenya waliendeleza ubabe wao, baada ya wanariadha wake kushika nafasi ya kwanza katika mbio za kilomita 42 na kilomita 21 wanaume, pamoja na nafasi ya kwanza katika kilomita 42 upande wa wanawake.

Katika mbio za kilomita 42 wanaume, Kipsang Kipkemoi alishika nafasi ya kwanza kwa kukimbia dakika 2:14:56 na kufuatiwa na mkenya mwenzake Julius Kilimo, aliekimbia kwa dakika kwa dakika 2:15:44 ambapo mkenya mwingine Dominic Kiangor alishika nafasi ya tatu kwa kukimbia dakika 2:16:25.

Kwa upande wa wanawake, mkenya Edna Joseph, alishinda mbio hizo pale alipomaliza kwa dakika 2:39:05 na kufuatiwa na Eunice Muchiri, (Kenya), aliekimbia kwa dakika 2:41:00 na watatu alikuwa ni Fridar Too, aliekimbia kwa dakika 2:44:04.

Akiongea muda mfupi baada ya kuwazawadia washindi, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mukangara, aliahidi ushirikiano wa serikali katika kuendeleza michezo hapa nchini.

 “Nichukue nafasi hii kuwapongeza wadhamini wa mbio hizi, Kilimanjaro Premium Lager pamoja na wadhamini shirikishi mbalimbali wa mashindano haya wakiongozwa na mdhamini mkuu, kwani mbali na kuibua na kukuza vipaji vipya, mashindano haya yametokea kuwa mchango mkubwa katika kuitangaza Tanzania na kukuza uchumi wa Kilimanjaro na nchi kwa ujumla kutokana na kushirikisha watu wengi kutoka ndani na nje ya nchi”, alisema.

Aliwataja wadhamini wengine kuwa ni pamoja na Vodacom Tanzania, GAPCO, Tanga Cement, CFAO Motors, KK Security, Keys Hotel, TPC Sugar, Tanzanite One, New Arusha Hotel, UNFPA, Fastjet na Kilimanjaro Water.

Aidha alitoa changamoto kubwa kwa viongozi wa riadha nchini kuhakikisha wanariadha wa Tanzania wanaandaliwa vyema na mapema ili kuendeleza ushindi, ambapo alisema ushindi wa Sarah na Failuna Makanga na mfano mzuri wa matayarisho mema.

Kwa upande wake Meneja wa  Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe alisema kuwa mbio hizi zimeweza kuleta hamasa kwa watu mbalimbali kushiriki mchezo wa riadha kwani Kilimanjaro Marathon ni tukio pekee la kimichezo ambalo linatoa fursa kwa watu wote kushiriki. “Tutaendelea kuwekeza katika riadha kwa kadri tuwezavyo kwa sababu Kilimanjaro Marathon sio tu kwa sababu imeishakuwa tukio linalosubiriwa na wanariadha wetu kila mwaka lakini pia ni tukio ambalo limeendelea kuitangaza nchi yetu kimataifa”, alisema.

Kavishe alisema tangu mbio hizi zilipofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 2003, Kilimanjaro Premium Lager iliamua kudhamini tukio hili kwa kuzingatia umuhimu wake kwa nchi yetu katika kukuza na kuendeleza mchezo wa riadha na vilevile kuutangaza Mlima Kilimanjaro ambao ni fahari ya Watanzania kama ilivyo bia yao ya Kilimanjaro Premium Lager.

No comments:

Post a Comment