STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, July 15, 2013

Sikinde kutumia likizo kuandaa mpya

Wanamuziki wa Sikinde wakiwajibika jukwaani
BENDI kongwe ya muziki wa dansi Mlimani Park 'Wana Sikinde' imesema itatumia muda wa mapumziko kumalizia nyimbo zao za albamu mpya pamoja na kuwaandalia mashabiki wao 'zawadi' kwa ajili ya sikukuu ya Idd el Fitri.

Katibu wa bendi hiyo, Hamis Mirambo aliiambia MICHARAZO kwamba kama desturi yao wakati wa mfungo wa Ramadhani husimamisha maonyesho yao kwa ajili ya mapumziko, lakini haina maana kwamba wanakaa tu bila kufanya lolote.

Mirambo alisema bendi hiyo hutumia likizo hiyo ya mfungo wa Ramadhani kumalizia nyimbo za albamu yao ijayo ambayo tayari nyimbo mbili zimesharekodiwa za 'Jinamizi la Talaka' na 'Kukatika kwa Dole Gumba'.

"Tumesitisha maonyesho yetu kipindi hiki, lakini tutatumia mapumziko haya kumalizia nyimbo zetu pamoja na kuwaandalia zawadi mashabiki wetu ili wakati wa sikukuu ya Idd wapate burudani mpya kabisa," alisema Mirambo.

Mirambo alisema zawadi waliopanga kuwapa burudani mashabiki wao ni kuibuka na nyimbo mpya ambazo watazisikia kwa mara ya kwanza katika siku ya Idd.
"Sisi hatuna zawadi zaidi ya kuwapa vitu vipya mashabiki wetu, kwa sababu hiyo ndiyo burudani yao," alisema.

Sikinde na baadhi ya bendi za muziki wa dansi zimekuwa na utamaduni wa kujipa likizo ya mwezi mzima kila unapojiri mfungo wa Ramadhani.

No comments:

Post a Comment