STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, December 5, 2014

Ndanda kuanza kuiwinda Mbeya City Jumatatu Dar

Kikosi cha Ndanda Fc
TIMU ya Ndanda ya Mtwara inayoshiriki Ligi Kuu kwa mara ya kwanza msimu huu inatarajiwa kuanza kambi ya mazoezi keshokutwa jijini Dar es Salaam, huku uongozi wake ukiendelea kuficha majina ya wachezaji wapya iliyowasajili kwenye dirisha dogo.
Mkurugenzi na Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Edmund Njowoka aliliambia MICHARAZO mapema leo kuwa, kambi yao ya mazoezi kwa ajili ya kujiwinda na mzunguko wa nane wa ligi hiyo itaanza siku ya Jumatatu badala ya Desemba 4 kama walivyokuwa wametangaza awali na itakuwa jijini Dar es Salaam.
Njowoka alisema uongozi wao umeamua kuiweka kambi hiyo jijini Dar es Salaam ili kutoa nafasi nzuri kwa kocha wao Meja Abdul MIngange kuwanoa vizuri wachezaji wapya ambao wamenyakuliwa na klabu hiyo katika dirisha dogo.
Hata hivyo alipoulizwa juu ya wachezaji wapya iliowaongeza, Njowoka alisema hawezi kuwataka kwa madai ni mapema mno kwa sasa na atafanya hivyo baada ya kufungwa kwa dirisha hilo Jumatatu ijayo.
"Hatuwezi kuzungumza vitu nusu nusu, wapo tuliofanikiwa kuwanyakua na wengine tunamalizana nao, hivyo subirini tumalize usajili wote kisha tuutangaze umma kitu kilichokamilika," alisema Njowoka.
Hata hivyo tayari timu hiyo ilishamtangaza kumsajili kiungo mshambuliaji wa Mtibwa, Masoud Chile na ilikuwa mbioni kuwanyemelea nyota wengine toka Yanga akiwamo kipa Ally Mustafa 'Barthez'.
Timu hiyo iliyopanda msimu huu sambamba na timu za Stand United na Polisi-Moro inatarajiwa kuvaana na Mbeya City katika mechi yao ijayo na mpaka ligi inasimama waliwakuwa katika nafasi ya pili toka mkiani ikiwa na pointi 6, moja zaidi ya wanaoshika mkia Mbeya City.

No comments:

Post a Comment