STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, March 8, 2013

Mtebe aahidi kuendelea kufunga VPL kama Vermelien

Salvatory Venance Mtebe 'shujaa' mpya wa Mtibwa Sugar
 
BEKI mahiri wa timu ya soka ya Mtibwa Sugar, Salvatory Mtebe ambaye ameibuka kuwa shujaa wa klabu hiyo katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara, ameahidi kuendelea kufunga mabao kadri awezavyo ili kuhakikisha Mtibwa inamaliza ligi katika 3 Bora.
Mtebe aliyeitungia Simba wakati Mtibwa ilipopata ushindi wa bao 1-0 kwenye mechi ya marudiano na kurudia tena majuzi mjini Tanga alipofunga bao pekee katika mechi yao dhidi ya Mgambo JKT, alisema anajisikia faraja kuibeba timu yake.
Mchezaji huyo alisema kadri atakavyokuwa akipata nafasi atakuwa akifunga mradi timu yake ije kumaliza msimu wa ligi ikiwa katika nafasi tatu za juu kwa vile ubingwa kwao ni vigumu kutokana na kuachwa mbali na timu za Yanga na Azam.
"Kwa kweli nashukuru kwa kuweza kuifungia timu yao mabao muhimu na kuipa pointi muhimu, nitaendelea kufanya hivyo kila nipatapo nafasi mradi Mtibwa imalize kwenye Tatu Bora. Mashabiki wetu wala wasiwe na hofu na kudhani nabahatisha," alisema.
Mtebe alisema hata kwenye msimu uliopita aliweza kuwa miongoni mwa mabeki waliokuwa na mabao mengi kwa kufunga mabao matatu, hivyo siyo ajabu kuendelea kufanya hivyo msimu huu kwa sababu alishawahi kucheza kama mshambuliaji.
Beki huyo wa kati aliyewahi kuichezea timu ya Atletico ya Burundi, Azam na Kagera Sugar kabla ya kutua Mtibwa misimu mitatu iliyopita, alisema kwa hali ya ushindani uliopo katika ligi ya msimu huu ni vigumu kutabiri bingwa mapema kwa sasa.

IDFA yaipongeza Ashanti kurejea Ligi Kuu, ila yaionya


Bango la Ashanti United walipopanda Ligi Kuu msimu wa 2005-06



Katibu Mkuu wa IDFA, Daud Kanuti (aliyesimama)

CHAMA cha Soka Wilaya ya Ilala, IDFA, kimeipongeza klabu ya Ashanti United kwa kufanikiwa kurejea tena Ligi Kuu Tanzania Bara, lakini wakiitahadharisha kuwa, inapaswa kuhakikisha wanajipanga vema ili wadumu kuicheza ligi hiyo kwa muda mrefu.
Ashanti ni moja ya klabu mbili zilizopanda ligi kuu msimu ujao nyingine ikiwa ni Mbeya City, baada ya mwishoni mwa wiki iliyopita kupata sare ya mabao 2-2 dhidi ya Villa Squad na hivyo kujihakikisha uongozi wa kundi lake katika Ligi Daraja la Kwanza, FDL.
Katika Mkuu wa IDFA, Daud Kanuti aliiambia MICHARAZO asubuhi ya leo (Machi 8) kuwa wamefurahishwa na timu hiyo ya Ilala kurejea tena ligi kuu baada ya kusota tangu ilipoteremka msimu wa 2008-2009.
Kanuti, alisema IDFA inaamini kurejea kwa Ashanti katika ligi kuu itaongeza chachu kama ilivyowahi kufanya wakati ikishiriki kwa kuzihenyesha Simba na Yanga kabla ya kupoteza muelekeo na kuteremka daraja.
"IDFA kwa heshima na taadhima tunaipongeza klabu ya Ashanti kwa kututoa kimasomaso wana Ilala kwa kurejea Ligi Kuu, kitu cha muhimu tunaiomba ianze kujipanga mapema ili kuweza kuhimili mikikimikiki ya ligi hiyo msimu ujao," alisema Kanuti.
Kanuti alisema uongozi wa IDFA kama ulivyokuwa begabega kwa klabu hiyo pamoja na wawakilishi wengine wa Ilala katika ligi daraja la kwanza inayoelekea ukingoni ndivyo ambavyo watakuwa pamoja na uongozi wa Ashanti kuhakikisha wanajipanga vema.
Ashanti United ilishawahi kucheza ligi hiyo baada ya kupanda daraja msimu wa 2005 ikiwa pamoja na Kagera Sugar kabla ya kuteremka msimu wa msimu wa 2008-09 ikiwa imewaibua nyota kadhaa wanaoendelea kutamba nchini kama Ally Mustafa 'Barthez',
Juma Nyosso, Juma Jabu, Adam Kingwande,  Mohammed Kijuso na wengineo.