STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, November 12, 2011

Mwaikimba aahidi ubingwa Azam






SIKU moja tangu amwage wino wa kuichezea Azam kwa mechi za duru la pili la Ligi Kuu
Tanzania Bara, Mshambuliaji Gaudence Mwaikimba 'Andy Carroll' ameahidi kuipigania klabu hiyo ili iwe bingwa mpya wa soka nchini.
Mwaikimba aliyekuwa akiichezea Moro United, aliyotua mapema msimu huu akitokea Kagera Sugar, alisema anaamini ana deni kubwa la kulipa fadhila ya kuaminiwa na klabu ya Azam kiasi cha kumsajili, ila atakachofanya yeye ni kushirikiana na wenzake kuipa ubingwa msimu huu.
"Kwangu ni furaha kubwa kutua Azam, moja ya klabu zenye malengo na muono wa mbali
katika soka la Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Wajibu wangu kama mchezaji ni kuhakikisha naipigania ifanye vema ikiwemo kuwa mabingwa wapya nchini," alisema.
Mshambuliaji huyo anayeshikilia nafasi ya pili katika orodha ya wafungaji mabao msimu huu, alisema kwa vile karibu wachezaji anayeenda kukutana nao Azam amewahi kucheza nao katika klabu mbalimbali na timu ya taifa, Taifa Stars hana hofu ya kuelewana nao mapema.
"Kwa mfumo wa soka letu toka klabu moja hadi nyingine kufanana, naamini itanichukua
muda mfupi kuzoeana na wenzangu na kubwa nalopenda kuwaahidi mashabiki wa Azam
kwamba watarajie mambo makubwa katika duru lijalo," alisema.
Kuhusu suala la uhakika wa namba kwa nafasi anayocheza ambayo tayari ndani ya Azam
inayo wachezaji nyota kama John Bocco, Mwaikimba alisema hana tatizo lolote kwa vile
anajiamini yeye ni mchezaji mzuri na mwenye uwezo mkubwa ndio maana amesajiliwa Azam.
Nyota huyo aliyewahi kuwika na klabu za Tukuyu Stars, Yanga, Ashanti United na Prisons Mbeya ni mmoja wa wachezaji wapya waliotua Azam ambayo imewatema wachezaji wao wawili wa kimataifa kutoka Ghana, Wahabu Yahya na Nafiu Awudu.
Mwingine aliyesajiliwa Azam katika dirisha hilo dogo ni beki wa zamani wa kimataifa wa Simba, Joseph Owino na huku mshambuliaji Jerry Tegete wa Yanga ni miongoni mwa
wanaowindwa na klabu hiyo.

No comments:

Post a Comment