STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, November 12, 2011

TMK waumwa kichwa videoni




KUNDI la muziki wa kizazi kipya la TMK Wanaume Family, limeachia mtaani video yake mpya ya 'Kichwa Kinauma', ikiwa ni maandalizi ya kupakuliwa albamu mpya ya kundi hilo.
Aidha, kundi la Tip Top Connection kesho linatarajia kuadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake kwa wasanii waliowahi kupitia katika kundi hilo na waliopo sasa kujumuika pamoja katika onyesho litakalofanyika Maisha Club Masaki, jijini Dar es Salaam.
Meneja wa kundi la TMK Wanaume Family, Said Fella 'Mkubwa Fella', alisema video ya wimbo huo ulioimbwa na wasanii Mheshimiwa Temba na Said Chegge, ni kati ya maandalizi ya kundi lao.
Mkubwa Fella alisema kukamilika kwa video ya wimbo huo ni mwanzo wa maandalizi ya upigwaji video wa nyimbo nyingine zitakazokamilisha albamu yao itakayokuwa na vibao 10 ambayo hata hivyo, hakuweza kuitaja jina lake.
"Mkubwa tumekamilisha video ya wimbo wetu mpya wa 'Kichwa Kinauma' tukiwa mbioni kufyatua video za nyimbo zetu nyingine za kukamilisha albamu ijayo ya TMK," alisema.
Mkubwa aliongeza sambamba na hilo, upande wake albamu yake ya miondoko ya taarab ya 'Kunguni Kunguni', ipo katika hatua ya mwisho kuachiwa hadharani ikiwa na nyimbo sita.
Nyimbo za albamu hiyo ya Mkubwa Fella ni 'Kusonakusonona', 'Simuachi', 'Midomo Imewashuka', 'Mchakamchaka', 'Sijapopoa Dodo' na 'Kimodern Modern'.
Nalo kundi la Tip Top Connection, moja ya makundi yanayotamba nchini, kesho litafanya onyesho maalum la kuadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake ambalo litapambwa na burudani mbalimbali ikiwemo soka na muziki utakaotumbuizwa na wasanii mbalimbali.
Onyesho hilo litawajumuisha wasanii wote waliowahi kupitia kundi hilo na wale waliopo sambamba na wengine walioalikwa kuwapiga tafu katika maadhimisho hayo yatakayofanyika kwenye ukumbi wa Maisha Club, Masaki jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment