STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, November 12, 2011

Bundi wa Sikinde kupelekwa Studio

BENDI kongwe za muziki wa dansi nchini, Mlimani Park 'Sikinde' ipo mbioni kuingiza studio kibao kipya cha 'Bundi', ikiwa katika harakati za kufyatua albamu mpya itakayokuwa na nyimbo sita.
Kibao hicho kipya kimetungwa na Abdalla Hemba, mmoja wa waimbaji mahiri wa bendi hiyo ambayo kwa sasa inatamba na wimbo wa 'Jinamizi la Talaka', kinachodaiwa ni 'dongo' kwa mahasimu wao, Msondo Ngoma wanaotamba na kibao cha 'Suluhu'.
Mmoja wa viongozi wa Sikinde, Hamis Milambo, alisema kibao cha 'Bundi', kitarekodiwa wakati wowote kuanzia sasa sambamba na vingine vitakavyokuwa katika albamu yao mpya.
Milambo alisema mbali na Jinamizi la Talaka na Bundi, nyimbo nyingine za albamu hiyo zilizokamilika ni 'Asali na Shubiri' uliotungwa na Shukuru Majaliwa, 'Nitalipa Deni', uliotungwa na bendi mzima ya Sikinde, 'Kilio cha Kazi'-Hassani Bitchuka na 'Nisamehe'-Hemba.
Wakati Sikinde wakijiandaa kuhitimisha albamu yao hivyo, kwa upande wa mahasimu wao, Msondo Ngoma wameibuka na kibao kingine kipya kiitwacho 'La Kuvunda' utunzi wa mkali Shaaban Dede 'Mzee wa Loliondo' ambaye anatamba pia na kibao kiitwacho 'Suluhu'.
Msondo ambao wameanza kurekodi nyimbo zao mpya kwa ajili ya albamu yao mpya, imeachia kibao hicho kipya ikiwa ni maandalizi ya albamu ya mwaka ujao.
Albamu yao ya sasa wanaotarajia kuiingiza sokoni mara itakapokamilika kurekodiwa inatarajiwa kufahamika kwa jina la 'Nadhiri ya Mapenzi' ambayo ni jina la kibao kilichotungwa na Juma Katundu.
Nyimbo nyingine za albamu hiyo na watunzi wake kwenye mabao ni 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi (Huruka Uvuruge), Dawa ya Deni (Is'haka Katima 'Papa Upanga), LIpi Jema na Baba Kibene za Edmund Sanga 'Eddo Sanga' na 'Suluhu' (Shaaban Dede).

No comments:

Post a Comment