STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, November 12, 2011

Taifa Stars yatakata Chad



Na Maulidi Kitenge, Chad
USHIRIKIANO wa wachezaji waliotokea benchi, Nurdin Bakari na Thomas Ulimwengu katika dakika za lala-salama uliipa Taifa Stars mwanzo mzuri wa mechi za hatua ya mchujo za kuelekea kwenye hatua ya makundi ya kufuzu kwa fainali zijazo za Kombe la Dunia 2014 kufuatia ushindi wa 2-1 ugenini kwa Chad jana.
Kiungo wa Yanga, Nurdin, aliyeingia katika kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Abdi Kassim anayecheza soka la kulipwa nchini Vietnam, aliifungia Stars goli la ushindi katika dakika ya 82 akitumia pasi ya mshambuliaji wa TP Mazembe ya DRC, Ulimwengu, ambaye pia aliingia katika kipindi cha pili kuchukua nafasi ya nyota mwenzake wa klabu hiyo ya Congo, Mbwana Samatta.
Katika mechi hiyo iliyofanyika kwenye Uwanja wa Idriss Mahamat Ouya mjini N'djamena, Stars walitangulia kupata bao la mapema katika dakika ya 11 kupitia kwa Ngassa aliyemalizia kiufundi pasi ya kiungo anayecheza soka la kulipwa nchini Canada, Nizar Khalfan.
Hata hivyo, wenyeji walihitaji dakika moja tu kusawazisha goli hilo walilopata kupitia kwa mshambuliaji wao anayecheza soka la kulipwa katika Ligi Daraja la Pili Ufaransa (Ligue 2) ya Club Laval B, Mahamat Labbo katika dakika ya 12 na kufanya matokeo ya 1-1 hadi wakati wa mapumziko.
Wakati mechi ikielekea ukingoni na wenyeji wakiamini kwamba wangeweza kupata angalau sare, Nurdin aliifungia Stars goli la pili na la ushindi katika dakika ya 80 lililoeafanya mashabiki wa Chad waliokuwa wamejaa uwanjani kuanza kuondoka kimyakimya.
Stars itarejea kifua mbele kesho kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere lakini itahitaji kutoruhusu kipigo katika mechi yao ya marudiano Jumanne kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Kama Stars itasonga mbele, itatinga katika Kundi C la kuwania kufuzu kwa fainali zijazo za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwaka 2014 nchini Brazil, ambapo watajumuika timu ngumu za Ivory Coast, Morocco na Gambia.
Kocha wa Stars, Jan Poulsen aliwapongeza wachezaji wake baada ya mechi hiyo lakini alisema kazi bado haijamalizika na wanahitaji umakini mkubwa ili kusonga mbele.
Kikosi cha Stars jana kiliundwa na Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Idrisa Rajab, Agrey Morris, Juma Nyoso, Shaban Nditi, Henry Joseph, Abdi Kassim/ Nurdin Bakari, Nizar Khalfan, Mrisho Ngassa, Mbwana Samatta/ Thomas Ulimwengu.

No comments:

Post a Comment