STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, October 15, 2013

RAIS JAKAYA KIKWETE AKUTANA NA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA WENYE WABUNGE LEO


Rais akiwa na viongozi wa vyama vya upinzani  leo ambaye alikutana nao

Rais Jakaya Kikwete akisalimiana na Tundu Lisu  nyuma yake mwenyekiti wa NCCR James Mbatia

Rais akiwa viongozi ikulu leo

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MKUTANO kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa vyenye uwakilishi Bungeni umemalizika Ikulu, Dar Es Salaam, muda mfupi uliopita leo, Jumanne, Oktoba 15, 2013 kwa pande hizo mbili kukubaliana kama ifuatavyo:

Moja , kwamba  vyama vyote vya siasa nchini vyenye mawazo, maoni na mapendekezo ya kuboresha Sheria ya Kurekebisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba viwasilishe mapendekezo yao haraka Serikalini ili itafute namna ya kuyashirikisha mapendekezo hayo katika marekebisho ya Sheria hiyo.

Pili, kwamba vyama vya siasa nchini, kama wadau muhimu katika mchakato wa Katiba Mpya, viangalie namna ya kukutana na kujenga mfumo wa mawasiliano na maridhiano wa jinsi kwa pamoja vitakavyosukuma mbele mchakato huo kwa maslahi mapana ya nchi yao na mustakabali wa taifa. Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimepewa jukumu la kuratibu jambo hilo ikiwa ni pamoja na kuandaa mkutano wa vyama hivyo na wadau wengine nchini.

Viongozi wa vyama vyama vya siasa waliokutana na Mheshimiwa Rais Kikwete ni Mheshimiwa Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa CUF; Mheshimiwa Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CHADEMA na Mheshimiwa James Mbatia ambaye ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi.
Wengine ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Mheshimiwa Philip Mangula, Mheshimiwa Isaack Cheyo ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa Chama cha UDP Mheshimiwa John Cheyo na Mheshimiwa Nancy Mrikaria ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa TLP Mheshimiwa Augustine Mrema. Waheshimiwa John Cheyo na Mrema wako nje ya nchi.

Wengine ambao wameambatana na wenyeviti wao ni Mheshimiwa H. Mnyaa na Bwana Julius Mtatiro wa CUF, Waheshimiwa Tundu Lissu na John Mnyika wa CHADEMA na Bwana Martin Mng’ongo wa NCCR-Mageuzi.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

15 Oktoba, 2013

No comments:

Post a Comment