STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 25, 2013

Madhira amlilia Rais Kikwete




MUIGIZAJI mahiri wa filamu, Mbwana Salim 'Bessa' au Madhira, amemlilia Rais Jakaya Kikwete na kuomba kuonana naye ili aweze kumfikishia kilio chake na cha wasanii wenye ulemavu kama yeye.
Bessa ambaye pia ni mtunzi wa riwayana mchoraji, alisema kutokana na wasanii wenye ulemavu kutothaminika wala kutiwa moyo, angependa kuonana na Rais Kikwete akiamini anaweza kusikia kilio chao na kuwasaidia ili nao wawe na hadhi sawa na wasanii wengine nchini.
"Ningependa nipate nafasi ya kuonana na Rais Kikwete ili nimfikishie kilio tulichonacho sisi wasanii wenye vipaji vya sanaa, lakini tunadhalilika kwa sababu ya ulemavu wetu, tafadhali naomba unifikishie ujumbe wangu kwa mheshimiwa," alisema Bessa.
Msanii huyo ambaye ni mtunzi mkuu wa vichekesho na filamu za kampuni ya Al Riyamy alisema hali wanayotendwa wasanii wenye ulemavu nchini ikiwemo kunyonywa kimasilahi na kutothaminika hata kwa viongozi wanaosimamia sanaa inawakatisha tamaa, ilihali waliamua kujitegemea.
"Wapo watu wenye ulemavu kama sisi walikata tamaa na kuwa tegemezi, sisi tumeamua kutumia vipaji vyetu kujiajiri na kuwatia moyo wengine, lakini bado tunaangaliwa kama watu duni na kukatishwa tamaa, naimba serikali iliangalie hili," alisema msanii huyo.
Aliongeza kuwa, pamoja na juhudi anazozionyesha akiwa pia ni mwalimu wa chekechea, mchoraji na mtengenezaji wa chaki na batiki, alisema kuna haja wasanii waenye vipaji kama yeye watupiwe macho kuwafanya wapige hatua kimaendeleo na kuwahamasisha wengine kujitegemea.

Golden Bush yazidi kutoa dozi ikiisubiri Wahenga FC

Kikosi cha Golden Bush Veterani
SIKU chache kabla ya kuvaana na wapinzani wao, timu ya Golden Bush Veterani imeendelea kutoa dozi baada ya mwishoni mwa wiki kuinyuka Kibangu Veterani kwa mabao 4-1 kabla ya kuwakung'uta tena watoto zao Golden Bush Fc kwa magoli 2-0.
Mechi hizo za kujipima nguvu zilichezwa Jumamosi na Jumapili ikiwa ni maandalizi ya kuvaana na wapinzani wao, Wahenga Fc pambano litakalochezwa kwenye uwanja wa Tp Afrika, Sinza siku ya Pasaka.
Katika mechi yao dhidi ya Kibangu, Golden Bush walipata ushindi wao kupitia mabao ya Sadik Muhimbo aliyefunga mara mbili, Said Swedi 'Panucci' na Di Natale, huku bao la kufutia machozi la Kibangu liliwekwa kimiani na Daudi.
Katika mechi iliyochezwa jana, dhidi ya vijana wao wanaoshiriki Ligi ya TFF- Kinondoni, Wazee wa Golden walipata ushindi wa 2-0 na kuendeleza ubabe kwa watoto hao kwani wiki iliyopita waliwanyuka mabao 2-1.
Katika hatua nyingine, Mlezi wa Golden Bush Veterani, Onesmo Waziri 'Ticotico' ameamua kutangaza dau kwa wapinzani wao iwapo wataibuka na ushindi au kuambulia sare atakuwa tayari kuwapa papo hapo kitita cha Sh 200,000.
Mechi hiyo ya Golden Bush na Wahenga, inatarajiwa kuhudhuriwa na mgeni rasmi, Kamanda Thobias Andengenye na itachezwa majira ya saa 10 jioni ambnapo lineup ya Golden Bush, kwa mujibu wa msemaji wao itakuwa kama ifuatavyo;

Philemon, Said Swedi, Faraji, Majuto Komu, Wisdom Ndlovu, Godfrey Bonny, Onesmo Wazir 'Ticotico' (captain), Waziri Mahadhi  'Mandieta', Athumani Machupa 'Magoli', Herry Morris na Sadik Muhimbo.

Rais TFF kufungua semina Copa Coca Cola








Na Boniface Wambura
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga atakuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa semina elekezi ya michuano ya Copa Coca Cola itakayofanyika kesho (Machi 26 mwaka huu).

Semina hiyo inayoshirikisha makatibu wakuu wa vyama vya mpira wa miguu mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar itafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na itafunguliwa na Rais Tenga kuanzia saa 3 kamili asubuhi.

Washiriki wengine katika semina hiyo itakayokuwa na watoa mada kutoka TFF na wadhamini kampuni ya Coca Cola ni waratibu wa michuano ya Umoja wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA).

MAPINDUZI SIMBA YALIKUWA BATILI-TFF

Wanachama wa Simba walipokutana Machi 17

Na Boniface Wambura
MKUTANO Mkuu wa Dharura ulioitishwa na wanachama wa Simba, Machi 17 mwaka huu na kuuondoa uongozi wa klabu hiyo si halali kwa vile haukufuata taratibu, na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) halitambui Kamati za Muda.
Uamuzi huo umefikiwa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za
Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Machi 24 mwaka huu) jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa.
Kamati imebaini kuwa kwa mujibu wa Ibara ya 22(2) ya Katiba ya Simba, Mkutano Mkuu wa Dharura unaitishwa na Kamati ya Utendaji baada yawanachama wasiopungua 500 kuwasilisha ombi hilo kwa maandishi na kujiorodhesha. Mkutano huo haukuitishwa na Kamati ya Utendaji ya Simba.
Utaratibu huo haukufuatwa ambapo barua ya Mkutano huo iliandikwa kwa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo badala ya Kamati ya Utendaji ya Simba ambayo ndiyo matakwa ya Katiba ya Simba.
Kwa mujibu wa Katiba ya Simba, Kamati ya Utendaji ndiyo inayoitisha Mkutano Mkuu wa Dharura baada ya kuhakiki uhai na uhalali wa wanachama waliojiorodhesha kuomba mkutano huo.
Kamati imesisitiza kuwa Katiba za wanachama wote wa TFF hazina
kipengele cha kura ya kutokuwa na imani na uongozi (vote of no
confidence), ndiyo maana uko nyuma wanachama wa Yanga, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga (SHIREFA) na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA) walipiga kura hiyo, na TFF kutotambua uamuzi wao.
Hata Katiba ya Simba haitoi mamlaka kwa Mkutano Mkuu wa Dharura kufukuza uongozi uliochaguliwa.
Katiba za wanachama wote wa TFF zimezingatia katiba mfano za
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambazo zinasema
kiongozi ataingia madarakani kwa uchaguzi, na si kuteuliwa (Kamati ya
Muda).
Pia Kamati imesema endapo wanachama wa Simba wangefuata taratibu na uongozi ukakataa kuitisha mkutano, wanachama wangetuma ombi hilo TFF kupitia Kamati ya Sheria ili kutoa mwongozo kwa uongozi wa Simba .
TFF ina mamlaka ya kutoa adhabu kwa viongozi wa wanachama wake wanaokwenda kinyume cha Katiba zao. Pia Kamati imesisitiza kwa wanachama wa TFF kuitisha mikutano yao kwa mujibu wa taratibu na Katiba zao, na wale ambao muda umefika wafanye hivyo haraka.

TENGA APONGEZA WACHEZAJI, SERIKALI USHINDI WA STARS

Na Boniface Wambura
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga
ameipongeza wachezaji wa Taifa Stars na benchi lao la ufundi, washabiki, mdhamini na Serikali kwa kufanikisha ushindi wa jana.

Tenga amesema ushindi huo umetokana na ushirikiano kutoka kwa wadau wote, na hasa wachezaji walioonesha kiwango kikubwa kulinganisha na mechi zilizopita ikiwemo kiwango cha kujituma uwanjani.

Amesema Serikali ni mdau mkubwa wa mpira wa miguu katika miundombinu, usalama na idara zake mbalimbali ikiwemo Uhamiaji ambayo imefanikisha kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa mechi hiyo ambapo Taifa Stars iliifunga Morocco mabao 3-1.

MECHI YA TAIFA STARS YAINGIZA MIL 226/


Na Boniface Wambura
PAMBANO la mchujo la Kombe la Dunia  kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Morocco (Lions of the Atlas) lililochezwa jana (Machi 24 mwaka huu) na Stars kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 imeingiza sh. 226,546,000.

Fedha hizo zimepatikana kutokana na watazamaji 32,614 waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000, sh. 7,000, sh.10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 34,557,864.41, maandalizi ya mchezo sh. 28,450,000 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh.
8,625,641.88.

Nyingine ni bonasi kwa timu ya Taifa Stars sh. 28,798,220.34, asilimia 15 ya uwanja sh. 18,917,141.01, asilimia 20 ya gharama za mechi sh.25,222,854.67 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika
(CAF) sh. 6,305,713.67.

Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh.71,885,135.82 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 3,783,428.20 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.

Friday, March 22, 2013

Niyonzima 'atikisa' kiberiti Jangwani


Haruna Niyonzima
KIUNGO wa kimataifa wa Yanga, Haruna Niyonzima, amesema kuwa atakuwa tayari kusaini mkataba mpya wa kuichezea Yanga katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara endapo watampa dola za Marekani 150,000 (Sh. milioni 240).
Mkataba wa Niyonzima aliyejiunga na Yanga mwaka juzi akitokea APR ya Rwanda unamalizika mwezi Juni mwaka huu.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka kwao Kigali, Rwanda ambako amekwenda kuitumikia nchi yake inayokabiliwa na mechi dhidi ya Mali Jumapili, Niyonzima, alisema hataki kurudia makosa aliyofanya mwaka jana.
Niyonzima alisema anaamini kuwa hicho kiwango cha fedha ndiyo dau lake kwa sasa au zaidi na ameamua kuwaambia Yanga kutokana na hatua yao ya kukataa kumruhusu mwaka jana kujiunga na El Mereikh ya Sudan iliyokuwa imekubali kumlipa kiasi hicho.
Kiungo huyo ambaye ni nahodha wa timu ya taifa lake (Amavubi), aliongeza kuwa hivi sasa kazi ya kuzungumzia mkataba wake itafanywa na wakala wake.
"Mambo nahitaji yafanyiwe kazi kabla sijaamua kuendelea kubaki Yanga, ikiwamo kuongezewa mshahara,'' alisema Niyonzima.
Kiungo huyo kipenzi cha mashabiki wa Yanga aliongeza kuwa hataki kupoteza nafasi kama ilivyokuwa miaka ya nyuma wakati alipokuwa akiichezea APR ambao hawakuwa tayari kumruhusu kirahisi kuondoka ndani ya timu hiyo inayotetea ubingwa wake wa ligi Kuu ya Rwanda.
Akizungumzia matakwa hayo ya Niyonzima, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Seif Ahmed, alisema jana kuwa wako katika mipango ya kuwapa mikataba mipya wachezaji wao wote wanaowahitaji kuendelea kuwa nao kabla ya kumalizika kwa ligi.
Hata hivyo, Ahmed alisema hawawezi kusema ni lini watakamilisha kazi hiyo kwani hiyo ni mipango ya viongozi wa klabu kwa kushirikiana na benchi kao la ufundi.
Niyonzima na Mrisho Ngassa wa Simba waliivutia El Mereikh baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika mashindano ya Kombe la Chalenji yaliyofanyika mwaka jana nchini Uganda lakini Ngassa aliamua kuikacha timu hiyo kwa madai kwamba anazingatia maslahi yake na siyo kukimbilia kucheza nje. Nafasi ya nyota hao ilichukuliwa na Selemani Ndikumana kutoka Interclub ya Burundi.


CHANZO:NIPASHE.

Rais Kikwete azindua Complex ya Azam na kuzipiga 'dongo' Simba, Yanga


 Rais Jakaya Kikwete akizindua rasmi Jiwe la Msingi wa Uwanja wa Azam Complex. (Picha na Habari Mseto Blog)
Rais Jakaya Kikwete akiwa kwenye Uwanja mwingine wa Azam ambao bado upo kwenye matengenezo
 Rais Jakaya Kikwete akikata utepe,wakati wa uzinduzi rasmi wa uwanja wa Azam Complex.
 Rais Jakaya Kikwete akiwapungia mkono  mashabiki wa Azam waliokuja kushuhudia uzinduzi rasmi wa uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi uwanja huo.
 Rais Jakaya Kikwete,akiwa kwenye chumba cha kufanyia mazoezi kwenye Uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi.
 Rais Jakaya Kikwete,akiwa kwenye chumba cha kufanyia mazoezi kwenye Uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi.
Rais Jakaya Kikwete akiwa kwenye Uwanja mwingine wa Azam ambao bado upo kwenye matengenezo.
 
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete alipigwa na butwaa baada ya kufika katika makao makuu ya klabu ya Azam yaliyopo Mbande jijini Dar es Salaam jana na kujionea uwekezaji mkubwa uliofanywa katika kujenga miundombinu ya kisasa ya timu hiyo.
Rais Kikwete ambaye alikuwa amefuatana na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, mkewe Mama Salma Kikwete na viongozi mbalimbali wa serikali, aliweka jiwe la msingi kuashiria kuzinduliwa rasmi kwa uwanja wa klabu hiyo wa uitwao Azam Complex, kisha akatembezwa kuiona miradi mbalimbali ya wawakilishi hao pekee wa Tanzania waliobaki mwaka huu katika michuano ya klabu ya Afrika.
Akizungumza baada ya kuzindua uwanja huo na kuona utekelezaji wa mipango ya Azam ikiwamo ya kulea vijana wenye vipaji vya soka, rais Kikwete aliupongeza uongozi wa klabu hiyo na kuzipa changamoto klabu kongwe za Simba na Yanga kujifunza kutoka kwao.
Kikwete pia aliipongeza Azam kwa kuwa timu pekee ya Tanzania iliyobakik katika michuano ya kimataifa baada ya Simba na Jamhuri kutolewa katika hatua ya kwanza ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika huku timu hiyo iliyokamata mnafasi ya pili msimu uliopita ikifuzu kwa raundi ya tatu ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
"Azam wamekuwa na mchango mkubwa katika kuendeleza soka nchini na timu yao sasa ni timu kigogo. Simba na Yanga sasa wanalazimika kujipanga zaidi wanapocheza na timu hii," alisema Kikwete.Akieleza zaidi kuhusu Simba Yanga, rais Kikwete alisema kuwa licha ya kuwa 'mnazi' wa mojawapo miaka iliyopita, klabu hizo zinakabiliwa na matatizo mengi yakiwamo ya tuhuma za ushindi wa kununua, imani za kishirikiana na kukosa viongozi makini.
"Klabu hii (Azam) haina wanachama wengi kama baadhi ya klabu nyingine ambazo wanachama wake wanagombana kila kukicha. Viongozi wa Azam msibweteke kama hawa jamaa kwa kutegemea kamati za ufundi (ushirikina)… hakuna uchawi katika mpira. Kama uchawi ungelikuwa unacheza mpira, Afrika tungelikuwa tumeshatwaa Kombe la Dunia. Ni upuuzi kuwekeza kwenye kamati za ufundi," alisema Kikwete.
"Wapo watu wanawekeza kwenye kusajili wachezaji kila mwaka. Ukifuatilia vizuri, wachezaji wanasajiliwa si kwa sababu wanahitajika, bali wasichukuliwe na timu nyingine, mpira hauko hivyo. Wekeza kwa vijana kwa kuhakikisha wanakula na kulala vizuri. Unakuta kiongozi hajui mchezaji anakula nini na analala wapi.
"Timu hii (Azam) inaendeshwa bila kutegemea wanachama wanaokimbilia kupiga kura kwa kuhongwa. Itakuwa timu kubwa sana, labda mshindwe wenyewe kwa kuamua kutumiwa. Mkikubali kuwa kivuli cha timu yoyote ili kuisaidia, mtashindwa."
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kampuni za Bakhresa (SBB) wanaomiliki Azam, Aboubakar Bakhresa, alimshukuru rais kwa kukubali kushiriki uzinduzi wa uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 7,000.
Alisema imewagharimu Sh. milioni 800 kulinunua eneo walilojenga uwanja huo, ofisi na hosteli za wachezaji na kwamba awamu ya kwanza ya ujenzi wa miundombinu hiyo tayari imeshawagharimu takriban Sh. bilioni tatu.
Azam ilianzishwa mwaka 2004 ikiwa na muungano wa timu za viwanda vitatu vya SSB. 2005 ilipanda dara la tatu, daraja la pili (2006), la kwanza (2007) na ilitinga Ligi Kuu ya Tanzania Bara 2008.
Hivi sasa, Azam ambayo haijawahi kushuka daraja tangu ipande ligi kuu, inakamata nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, ikiwa na pointi 37 baada ya kucheza mechi 19, pointi 11 nyuma ya vinara Yanga walioshuka dimbani mara 20.
Novemba mwaka jana, mshindi mara tatu wa zamani wa tuzo ya mwanasoka bora wa Afrika, Abedi Pele alipigwa butwaa pia alipofika Mbande na kukiri kuwa amevutiwa mno na jitihada za klabu hiyo katika kukuza soka la vijana.